Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Rafiki Muzuri Ni Nani?

Rafiki Muzuri Ni Nani?

Tarehe 25 Mwezi wa 12, 2010, mwanamuke mwenye miaka 42 katika Uingereza aliweka kwenye adresi ya kupashana habari na watu yenye kujulikana sana ya Internete ujumbe wa kutafuta kujiua. Ujumbe huo ulikuwa wa kuomba musaada. Hata ikiwa alikuwa na “marafiki” zaidi ya 1 000 kwenye adresi hiyo, hakuna mutu aliyemusaidia. Kisha siku moja polisi ilimupata akiwa amekufa. Alikuwa ametumia dawa mingi sana ambayo ilimuua.

Leo, teknolojia inatuwezesha kupata “marafiki” wengi kwenye Internete kwa kuongeza tu majina yao kwenye hesabu ya watu tunaopashana nao habari. Na ikiwa tunataka kukata ‘urafiki’ na watu hao, tunazima tu majina yao. Lakini habari ambayo tumezungumuzia juu ya mwanamuke katika inchi ya Uingereza inaonyesha kwamba watu wengi hawana marafiki wa kweli. Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba hata ikiwa tunakuwa na marafiki wengi, hesabu ya marafiki wa kweli kabisa imepunguka.

Kama watu wengi, pengine unakubali kwamba ni lazima kuwa na marafiki wazuri. Labda unakubali pia kwamba kuwa rafiki wa kweli si rahisi kama vile tu kufungua viunganishi kwenye ordinatere ao telefone ya hali ya juu. Unataka rafiki awe mutu wa namna gani? Unaweza kufanya nini ili uwe rafiki muzuri? Inaomba kufanya nini ili urafiki uendelee?

Fikiria kanuni 4 zinazofuata, na ona namna mashauri ya Biblia yanaweza kukusaidia uwe rafiki muzuri.

1. Onyesha Kwamba Unahangaikia Kabisa Wengine

Ili kufanya urafiki wa kweli, inaomba kila mumoja ajitoe kwa mwengine. Ni kusema, rafiki muzuri anatambua kwamba ana daraka kuelekea mwenzake, na anamuhangaikia kabisa. Kila mumoja anapaswa kujitoa kwa mwengine, na hilo linaomba kujikaza sana na kujinyima mambo fulani kwa ajili ya mwenzako. Lakini, kufanya hivyo kunaleta faida. Jiulize, ‘Je, niko tayari kujitolea, kutoa wakati wangu, na mali yangu ili kusaidia rafiki yangu?’ Kumbuka kwamba ili kupata rafiki muzuri, ni lazima wewe kwanza uwe rafiki muzuri.

WATU WANATAKA RAFIKI WA NAMNA GANI?

Irene: “Kama ilivyo kuhusu kulima bustani nzuri, ili kufanya urafiki muzuri inaomba wakati mwingi na pia kuendelea kutunza urafiki huo. Inaomba kwanza uwe na nia ya kuwa rafiki muzuri. Uwe mwema na upendezwe na wengine. Uwe tayari kutumia wakati wako wengine wanapokuwa na lazima yako.”

Luis Alfonso: “Ulimwengu wa leo unachochea watu wajifikirie wenyewe kuliko kuwafikiria wengine. Inafurahisha sana wakati mutu anapendezwa kabisa na wewe bila kutazamia jambo fulani kwako.”

BIBLIA INASEMA NINI?

‘Kama vile munavyotaka watu wawatendee ninyi, muwatendee wao vivyo hivyo. Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.’ (Luka 6:31, 38) Katika andiko hili, Yesu anatutia moyo tusiwe wachoyo lakini tuwe tayari kupatia wengine. Hilo linafanya urafiki ukuwe nguvu. Ikiwa uko tayari kuwasaidia marafiki bila kutazamia jambo fulani kwao, bila shaka watakufurahia.

2. Zungumuza Nao

Urafiki wa kweli unaendelea ikiwa watu wanazungumuza kwa ukawaida. Kwa hiyo, muzungumuzie pamoja mambo ambayo munafurahia. Sikiliza mawazo ya mwenzako, na uyaheshimu. Wakati inafaa, umupongeze na kumutia moyo. Wakati fulani, rafiki anaweza kuhitaji kushauriwa ao kukaripiwa, na mara nyingi si rahisi kufanya hivyo. Hata hivyo, rafiki muzuri hataogopa kuambia waziwazi rafiki yake kosa lake nzito na kumupatia mwongozo kwa hekima.

WATU WANATAKA RAFIKI WA NAMNA GANI?

Juan: “Rafiki muzuri hapaswe kuogopa kutoa mawazo yake, lakini hapaswe pia kukasirika wakati mawazo yake yanapingwa.”

Eunice: “Ninapenda sana marafiki ambao wako tayari kupitisha wakati na mimi na ambao wananisikiliza, zaidi sana wakati nina magumu.”

Silvina: “Marafiki wa kweli wanakuambia kweli yote, hata ikiwa wanajua hautafurahi kuisikia, kwa sababu wanakutakia mema.”

BIBLIA INASEMA NINI?

‘Kila mutu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Kwa kawaida, rafiki muzuri anafurahi wakati mutu anamusikiliza. Ikiwa unaendelea kuzungumuza bila kumuachia nafasi ya kusema, hilo linaonyesha kama unafikiri mawazo yako ndiyo ya maana kuliko yake. Kwa hiyo, sikiliza wakati rafiki yako anakuelezea mawazo yake ya moyoni na mambo yanayomuhangaisha. Na usikasirike ikiwa anakuelezea mambo waziwazi. Methali 27:6 inasema hivi: ‘Vidonda vinavyosababishwa na mupenzi ni vya uaminifu.’

3. Usitafute Ukamilifu kwa Marafiki

Kadiri tunakuwa marafiki sana na mutu, ndivyo tunajua uzaifu mbalimbali alio nao. Marafiki wetu hawakamilike, na sisi pia. Kwa hiyo, tusitazamie hata kidogo ukamilifu kwa marafiki wetu. Ni vizuri tupendezwe na sifa zao nzuri na kuepuka kuangalia sana makosa yao.

WATU WANATAKA RAFIKI WA NAMNA GANI?

Samuel: “Mara nyingi, tunatazamia mengi kwa wengine kuliko yale tunayotazamia kwa sisi wenyewe. Ikiwa tunatambua kwamba sisi wenyewe tunakosea na kwamba tunahitaji kusamehewa, tutakuwa tayari kuwasamehe wengine.”

Daniel: “Utazamie kwamba rafiki zako watafanya makosa. Matatizo yanapotokea, ni vizuri kuyamaliza haraka na kujikaza kusahau.”

BIBLIA INASEMA NINI?

Uko tayari kusamehe?​—Wakolosai 3:13, 14

‘Sisi wote tunajikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwae katika neno, huyo ni mutu mukamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.’ (Yakobo 3:2) Kutambua ukweli huo kunaweza kutusaidia tuwaelewe marafiki wetu. Pia, kutatuwezesha tusiangalie sana makosa madogo-madogo na uzaifu mbalimbali ambao unaweza kutukasirisha. Bible inasema hivi: ‘Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. . . . Lakini, zaidi ya mambo haya yote, mujivike upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’​Wakolosai 3:13, 14.

4. Ongeza Hesabu ya Marafiki

Kweli kabisa, ni lazima tuchague vizuri watu ambao tunapenda wawe marafiki wetu. Lakini hilo halimaanishe kwamba tunapaswa tu kuchagua marafiki wa miaka yetu ao walio na elimu fulani. Kupendezwa na watu wa miaka yote, watu wa desturi na inchi mbalimbali, kunaweza kabisa kufanya maisha yetu yawe yenye kupendeza.

WATU WANATAKA RAFIKI WA NAMNA GANI?

Unai: “Kufanya urafiki tu na watu wa miaka yako na ambao wanapendezwa na mambo unayopendezwa nayo, ni kama vile kuvaa nguo ya rangi moja kila siku. Hata upende sana rangi hiyo, siku moja itakuchokesha.”

Funke: “Kuongeza hesabu ya marafiki kumenifanya nikomae. Nimejifunza kuishi na watu wa miaka yote na desturi zote, na hilo limenifanya niwe mutu mwenye urafiki zaidi na tayari kujiambatanisha na hali. Na rafiki zangu wanapendezwa kabisa na hilo.”

Unajikaza kufanya urafiki na watu wa namna zote?—2 Wakorintho 6:13

BIBLIA INASEMA NINI?

‘Kwa hiyo, yakiwa kama malipo—mimi nasema kana kwamba ni kwa watoto. Ninyi, pia, mupanuke.(2 Wakorintho 6:13) Biblia inatutia moyo tufanye urafiki na watu wa namna zote. Kufanya urafiki na watu wa namna zote kunaweza kukusaidia ujue namna mbalimbali za maisha, na pia kutafanya wengine wakupende.