Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Ufahamu wa Mutu Hakika Unapunguza Hasira Yake’

‘Ufahamu wa Mutu Hakika Unapunguza Hasira Yake’

Mwalimu wa kikundi cha masomo cha muchezo wa basketi alifukuzwa kwenye kazi kwa sababu ya hasira yake isiyozuiliwa. Mutoto analalamika kwa hasira kwa sababu mambo hayafanywe vile anataka. Mama anaanza kutukanana na kijana wake mwanaume kwa sababu chumba chake ni kichafu.

SISI wote tumeona watu wanakasirika, na bila shaka sisi wenyewe tumekasirika wakati fulani. Hata ikiwa tunaona kuwa hasira ni mbaya na kuwa tunapaswa kuiepuka, mara nyingi tunajisikia kuwa tuna sababu ya kukasirika, zaidi sana wakati mutu fulani anaonekana kuwa anavunja haki yetu. Habari fulani ya Shirika la Saikolojia la Amerika inaonyesha hata kuwa “hasira ni namna ya mutu kujisikia moyoni iliyo ya kawaida kabisa na yenye kufaa mara nyingi.”

Mawazo kama hayo yanaweza kuonekana kuwa yenye kufaa wakati tunafikiria mambo mutume Mukristo Paulo aliandika akiongozwa na roho ya Mungu. Paulo alikubali kuwa watu wanaweza kukasirika wakati fulani. Alisema hivi: ‘Iweni na gazabu [ao hasira], lakini musitende zambi; jua lisitue mukiwa katika hali ya kuchokozeka.’ (Waefeso 4:26) Kwa sababu ya hilo, je, tunapaswa kujiacha tukasirike, ao tunaweza kufanya yote tunaweza ili kuzuia hasira yetu?

UNAPASWA KUKASIRIKA?

Wakati Paulo alitoa shauri hilo juu ya hasira, labda alikumbuka maneno ya mutunga-zaburi aliyeandika hivi: ‘Mufazaike, lakini musitende zambi.’ (Zaburi 4:4) Lakini, Paulo alitoa shauri hilo kwa kusudi gani? Alisema tena hivi: ‘Uchungu wote wenye uovu na hasira na gazabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.’ (Waefeso 4:31) Kupitia maneno hayo, Paulo aliwatia moyo Wakristo waepuke kujiacha wakasirike. Jambo lenye kupendeza ni kwamba habari tuliyotaja ya Shirika la Saikolojia la Amerika inasema tena hivi: “Wachunguzi wamevumbua kama ‘kuachia hasira nafasi’ kunaongeza hasira na ukali na hakukusaidie . . . kubadilisha hali.”

Kwa hiyo, namna gani tunaweza ‘kuondoa’ hasira na matokeo yote mabaya yanayoletwa na hasira? Mufalme Sulemani mwenye hekima wa Israeli ya zamani aliandika hivi: ‘Ufahamu wa mutu hakika unapunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita [ao anaposamehe] kosa.’ (Methali 19:11) Namna gani ‘ufahamu wa mutu’ unasaidia wakati hasira inamupanda?

 NAMNA UFAHAMU UNAPUNGUZA HASIRA

Ufahamu ni uwezo wa kuelewa hali fulani. Kuwa na ufahamu kunamaanisha kuona zaidi ya mambo yanayoonekana kwa inje. Namna gani hilo linasaidia wakati mutu fulani anatuchokoza ao anatukasirisha?

Wakati tunaona ukosefu wa haki, tunaweza kukasirika. Lakini, ikiwa tunafuata namna tunajisikia na kutenda kwa ukali, tunaweza kujiumiza wenyewe ao kuumiza mutu mwengine. Moto usiozuiliwa unaweza kuunguza nyumba, vilevile mulipuko wa hasira unaweza kuharibisha sifa ya muzuri ao uhusiano wa mutu pamoja na wengine, na hata pamoja na Mungu. Kwa hiyo, ukisikia hasira inaanza kukupanda, ni wakati wa kufikiria kwa uzito hali inayokuletea hasira. Kuelewa hali hiyo muzuri zaidi kutatusaidia kabisa tuzuie hasira yetu.

Mufalme Daudi, Baba ya Sulemani, alikuwa karibu kumwaga damu ya mwanaume anayeitwa Nabali, lakini aliepuka jambo hilo kwa sababu alisaidiwa kuchunguza hali hiyo kwa undani kabisa. Daudi na watu wake walikuwa wanachunga kondoo za Nabali katika jangwa la Yudea. Wakati wa kukata manyoya ya kondoo ulipofika, Daudi aliomba Nabali chakula kidogo. Nabali alimujibia hivi: ‘Je, nichukue mukate wangu na maji yangu na nyama yangu ambayo nimewachinjia wakataji-manyoya wangu na kuwapa watu ambao sijue hata wanatoka wapi?’ Alimutukana Daudi kabisa! Wakati Daudi alisikia maneno hayo, yeye, pamoja na wanaume 400 hivi, walijitayarisha ili kuenda kumuua Nabali na watu wa nyumba yake.—1 Samweli 25:4-13.

Abigaili, Bibi ya Nabali, alisikia jambo lililotokea na akaenda kumuona Daudi. Wakati alimukuta Daudi na watu wake, alianguka kwenye miguu yake na kusema hivi: ‘Tafazali umuache kijakazi wako aseme masikioni mwako, na wewe uyasikilize maneno ya kijakazi wako.’ Kisha, akamuelezea Daudi namna Nabali alikuwa mupumbavu kabisa na akamuonyesha kuwa atahuzunika ikiwa analipiza kisasi na kumwaga damu.—1 Samweli 25:24-31.

Daudi alipata ufahamu gani kupitia maneno ya Abigaili yaliyomusaidia kupunguza hasira katika hali hiyo? Kwanza, aliona kuwa Nabali alikuwa mupumbavu tangu kuzaliwa, na pili, aliona kuwa angekuwa na deni la damu ikiwa angejilipizia kisasi. Kama Daudi, kitu fulani kinaweza kukukasirisha. Unaweza kufanya nini? Habari moja ya Hopitali ya Mayo juu ya namna ya kuzuia hasira inasema hivi: “Chukua wakati kidogo ili kuvuta pumuzi na uhesabie mupaka 10.” Kwa kweli, acha kwanza mambo unayofanya na ufikiri ili kujua ni nini ilileta tatizo na matokeo ya mambo unayotaka kufanya yanaweza kuwa gani. Acha ufahamu upunguze hasira yako, ao hata kuimaliza.—1 Samweli 25:32-35.

Vilevile, watu wengi leo wamesaidiwa kuzuia hasira yao. Sebastian alieleza namna alijifunza kuzuia hasira na chuki yake kupitia funzo la Biblia. Wakati huo alikuwa na miaka 23 akiwa mufungwa katika gereza la Polandi. Alisema hivi: “Kwanza, ninawaza juu ya tatizo. Kisha, ninajikaza kutumikisha shauri la Biblia. Nimetambua kama Biblia ni kitabu kizuri cha muongozo.”

Kutumikisha mashauri ya Biblia kunaweza kukusaidia kuzuia hasira kali

Setsuo alifanya pia hivyo. Alisema hivi: “Nilizoea kufokea wengine wakati walinikasirisha kwenye kazi. Sasa kwa kuwa nimejifunza Biblia, kuliko kufoka ninajiuliza hivi: ‘Kosa ni la nani? Haiko mimi ndiye ninaleta tatizo?’” Kuwaza juu ya maulizo kama hayo kulimusaidia apunguze hasira yake, na alikuwa na uwezo wa kuzuia hasira kali iliyopanda katika moyo wake.

Hasira inaweza kuwa yenye nguvu sana, lakini mashauri ya Neno la Mungu ni yenye nguvu zaidi. Kwa kutumia shauri la hekima la Biblia na kusali ili kuomba musaada wa Mungu, wewe pia unaweza kuacha ufahamu upunguze ao hata kuzuia hasira yako.