Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAZUNGUMUZO YA BIBLIA PAMOJA NA JIRANI

Sababu Gani Tuchunguze Biblia?

Sababu Gani Tuchunguze Biblia?

Habari inayofuata ni mufano wa mazungumuzo ambayo Shahidi wa Yehova fulani anaweza kuwa nayo pamoja na jirani yake. Kwa mufano, Shahidi fulani anayeitwa Benjamin anazungumuza na mwanaume anayeitwa Eric.

BIBLIA INA HISTORIA YA KWELI

Eric: Ninaweza kukuambia kuwa sipendezwe sana na dini. Kwa hiyo, siwaze kuwa tuna mengi ya kuzungumuza.

Benjamin: Ninafurahi kusikia hivyo. Lakini, jina langu Benjamin. Na wewe jina lako nani?

Eric: Eric.

Benjamin: Ninafurahi kukutana na wewe, Eric.

Eric: Na mimi pia.

Benjamin: Nilitaka kukuuliza, ulikomalia katika familia yenye kupenda dini?

Eric: Ndiyo. Lakini wakati nilitoka nyumbani na kuenda kusoma masomo ya juu, niliachana na mambo ya dini.

Benjamin: Ninakuelewa. Ulijifunza nini kwenye masomo ya juu?

Eric: Nilijifunza Elimu ya jamii na historia. Tangu zamani ninapendezwa na historia, kwa sababu historia inaonyesha namna watu waliendelea katika dunia.

Benjamin: Historia inaweza kupendeza. Kama vile unajua, Biblia ni kitabu cha historia. Umekwisha kufanya uchunguzi juu ya Biblia pia?

Eric: Hapana kabisa. Ninajua kuwa ni kitabu kizuri, lakini sijafikiria hata siku moja kuwa Biblia ni kitabu cha historia.

Benjamin: Unaonekana kuwa mutu mwenye kuwa tayari kukubali mawazo ya mupya. Ikiwa uko na dakika fulani, ningependa kukuonyesha mifano kidogo inayoonyesha kuwa Biblia iko na historia ya kweli.

Eric: Sawa. Lakini sina Biblia.

Benjamin: Hakuna shida. Ninaweza kukuonyesha katika Biblia yangu. Mufano wa kwanza ni huu katika andiko la 1 Mambo ya Nyakati sura ya 29, mustari wa 26 na wa 27. Mistari hiyo inasema hivi: “Naye Daudi mwana wa Yese, akatawala juu ya Israeli yote; na siku alizotawala juu ya Israeli zilikuwa miaka 40. Katika Hebroni alitawala miaka 7, na katika Yerusalemu alitawala miaka 33.”

Eric: Namna gani mufano huo unaonyesha kuwa Biblia ina historia ya kweli?

Benjamin: Wakati fulani wachambuzi walisema kuwa Mufalme Daudi hakuishi hata siku moja.

Eric: Kweli? Sababu gani walikuwa na mashaka kuwa aliishi?

Benjamin: Isipokuwa tu Biblia, hawakupata ushuhuda mwingi katika maandishi mengine ulioonyesha kuwa alikuwa mutu wa kweli. Lakini, katika mwaka wa 1993, kikundi cha wachimbuaji wa vitu vya zamani kilivumbua jiwe la zamani sana lenye kuwa na maandishi juu yake yanayotafsiriwa “Nyumba ya Daudi.”

Eric: Hilo ni jambo lenye kupendeza.

Benjamin: Mutu mwingine anayezungumuziwa katika Biblia mwenye walishakia kuwa aliishi ni Pontio Pilato, gavana aliyetawala wakati wa Yesu. Anatajwa hapa katika andiko la Luka sura ya 3, mustari wa 1, ni mumoja kati ya wakubwa wa serikali wa wakati huo.

Eric: Ndiyo, ninaelewa. Mustari huo unasema juu ya wakati ‘Pontio Pilato alikuwa gavana wa Yudea, na Herode alikuwa mutawala wa wilaya ya Galilaya.’

Benjamin: Sawa. Kwa miaka mingi, watu fulani wenye elimu walikuwa na mashaka kuwa Pontio Pilato aliishi kwelikweli. Kisha, miaka karibu 50 iliyopita, jiwe moja lilipatikana katika Mashariki ya Kati ambako jina hilo lilikuwa linachorwa waziwazi.

Eric: Hmm. Nilikuwa sijasikia maelezo hayo.

Benjamin: Ninafurahi kuzungumuzia mambo hayo na wewe.

Eric: Kusema kweli, sikuzote ninaiheshimia Biblia, ninaiona kama vitabu vingine tu, lakini sijafikiri hata siku moja kuwa ina maana yoyote wakati wetu. Inaweza kuwa na historia ya kweli, lakini siwazie kuwa ina faida yoyote.

BIBLIA NI KITABU CHA ZAMANI LAKINI PIA CHA SASA

Benjamin: Watu wengi watakubaliana na maneno hayo. Lakini mimi siamini hivyo. Sababu ni hii: Mambo ya musingi watu wako nayo lazima hayajabadilika tangu mwanzo mupaka leo. Kwa mufano, sikuzote tuko na lazima ya chakula, mavazi, na makao. Sikuzote tumekuwa na lazima ya kuzungumuza na wengine na kuwa na familia yenye furaha. Sisi wote tunaona mambo hayo kuwa ya maana, sivyo?

Eric: Ndiyo.

Benjamin: Biblia inaweza kutusaidia katika mambo hayo yote. Ndiyo sababu tunasema kama Biblia ni kitabu cha zamani lakini pia cha sasa.

Eric: Unataka kusema nini?

Benjamin: Katika maneno mengine, Biblia ina kanuni za musingi zilizo za maana leo kama vile zilikuwa wakati ziliandikwa mamia ya miaka iliyopita.

Biblia ina kanuni za musingi zilizo za maana leo kama vile zilikuwa wakati ziliandikwa mamia ya miaka iliyopita

Eric: Sawa. Katika mambo gani?

Benjamin: Katika mambo kama vile kuwa na mawazo yenye kufaa juu ya feza ao maisha ya familia yenye furaha ao kuwa rafiki muzuri, kanuni za Biblia zinaweza kutuongoza. Kitabu hiki ni kama karte inayotuongoza kwenye maisha ya muzuri. Kwa mufano, si jambo jepesi kuwa bwana muzuri na kichwa cha jamaa katika siku hizi, sivyo?

Eric: Ndiyo, ninakubaliana na wewe. Mimi na bibi yangu tumeoana kumepita karibu mwaka moja, na kila wakati haiko vyepesi kuelewana katika mambo yote.

Benjamin: Ni hivyo kabisa. Lakini Biblia ina kanuni nyepesi zinazosaidia. Kwa mufano, fungua kitabu cha Waefeso sura ya 5. Tusome mustari wa 22, 23, na 28. Ikiwa unapenda, unaweza kusoma mistari hiyo.

Eric: Sawa. Inasema hivi: ‘Wake [bibi] na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha muke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko, yeye akiwa mwokozi wa mwili huu.’ Kisha, mustari wa 28 unasema hivi: ‘Vivyo hivyo waume [bwana] wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayemupenda muke wake anajipenda mwenyewe.’

Benjamin: Sawa. Aksanti. Ni kweli, ikiwa bibi na bwana wanajaribu kutumia shauri hilo nyepesi, maisha ya familia yatakuwa ya muzuri, sivyo?

Eric: Ndiyo, ninafikiri hivyo. Lakini ni vyepesi kusema hivyo kuliko kufanya.

Benjamin: Kwa kweli; hakuna mutu mukamilifu. Lakini, katika sura hiyo ya Biblia kuna mustari unaotuchochea tujue mipaka yetu. * Katika kila uhusiano, ni jambo la lazima kuwa na usawaziko na kuelewana. Mimi na bibi yangu tumetambua kama Biblia inaweza kutusaidia kuwa na usawaziko huo.

Eric: Hilo linaeleweka.

Benjamin: Mashahidi wa Yehova wako na adresi ya Internete yenye kuwa na habari za muzuri juu ya ndoa na maisha ya familia. Ikiwa uko na dakika fulani, ninaweza kukuonyesha mifano kidogo ya habari hizo.

Eric: Hakuna shida. Ninaweza kuwa na dakika kidogo.

Benjamin: Muzuri. Adresi hiyo ya Internete ni www.mt711.com. Huu ndio ukurasa wa mwanzo.

Eric: Ninafurahia picha hizi.

Benjamin: Hizo ni picha fulani za kazi ya kuhubiri tunayofanya duniani pote. Hapa kuna kichwa “Vichapo.” Chini ya kichwa hicho, kuna magazeti mapya na vichapo vingine vyenye kuzungumuzia habari mbalimbali kutia ndani maisha ya familia. Kwa mufano, acha tuchunguze broshua Habari Njema Inayotoka kwa Mungu! Somo moja katika broshua hii lina kichwa “Unaweza Kufanya Nini ili Familia Yako Iwe Yenye Furaha?”

Eric: Hilo ni ulizo lenye kupendeza. Ningependa nijue jibu!

Benjamin: Habari hii inazungumuzia mambo mengi yanayoweza kukusaidia ukuwe na furaha katika ndoa yako. Ona fungu hili chini ya ulizo la 2. Eric, ungependa kusoma misemwa miwili ya mwisho?

Eric: Ndiyo. Inasema hivi: “Bwana na bibi wanapaswa kupendana na kuheshimiana. Kwa sababu mwanaume na mwanamuke wote wawili si wakamilifu, kujua kusamehe mwengine ni jambo la lazima sana ili kuwa na furaha katika ndoa.” Hmm, ninakubaliana na mambo hayo.

Benjamin: Aksanti kwa usomaji wako. Kati ya maandiko yanayotajwa kuna Waefeso 5:33. Tafazali, unaweza kusoma andiko hilo katika Biblia yangu?

Eric: Linasema hivi: ‘Kila mutu mumoja-mumoja kati yenu na amupende hivyo muke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, muke anapaswa kumuheshimu sana mume wake.’

Benjamin: Umetambua kuwa wanakazia kutoa kile kila mumoja alitazamia kupokea?

Eric: Sijue kabisa unataka kusema nini.

Benjamin: Sawa, ni kweli kama mwanaume anataka ajisikie kuwa mwenye kuheshimiwa na bibi yake, bibi naye anataka kuwa hakika kama bwana yake anamupenda kabisa, sivyo?

Eric: Ndiyo, ni hivyo.

Benjamin: Ikiwa bwana anatafuta mara nyingi njia za kumuonyesha bibi yake upendo, itakuwa vyepesi kwa bibi kumuheshimia, sivyo?

Eric: Ndiyo.

Benjamin: Hata ikiwa andiko lenye tumesoma katika Biblia liliandikwa kumepita karibu miaka 2 000, linazungumuzia mahitaji ya bibi na bwana katika ndoa na linatoa shauri la muzuri lenye, ikiwa linatumiwa, linasaidia kabisa.

Eric: Ninakubali kama Biblia iko na mambo mengi yenye sikuwazia.

Benjamin: Eric, ninafurahi kusikia hivyo. Ningependa kurudia ili kujua mawazo yako juu ya ulizo la 3, lenye kusema “Je, unaruhusiwa kumuacha bibi yako ao bwana yako ikiwa ndoa yenu ina matatizo?” Ulizo hilo linapatikana katika somo hilohilo kwenye adresi yetu ya Internete. *

Eric: Sawa. Mimi na bibi yangu tutalichunguza pamoja.

Una ulizo fulani juu ya habari za Biblia ambalo umekwisha kujiuliza? Unapenda kujua mengi juu ya mambo Mashahidi wa Yehova wanaamini ao juu ya mambo fulani wanayofanya? Ikiwa jibu ni ndiyo, usisite kuuliza ulizo hilo wakati utakutana na Shahidi wa Yehova. Atafurahi kuzungumuzia mambo hayo pamoja na wewe.

^ fu. 63 Ili kupata habari zaidi, soma sura ya 14 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.