Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

UIGE IMANI YAO | YOSEFU

“Mimi Niko Mahali pa Mungu?”

“Mimi Niko Mahali pa Mungu?”

YOSEFU alikuwa anasimama katika bustani yake wakati jua lilikuwa limeshuka. Pengine alikuwa anaangalia miti ya ngazi na miti mingine ya matunda, visima vyenye mimea yenye kuota katika maji, na nyuma tu ya ukuta alikuwa anaona nyumba ya Farao. Wazia sauti zenye Yosefu alikuwa anasikia zinatoka katika nyumba yake wakati Manase, mutoto wake wa kwanza, alikuwa anachekesha mudogo wake Efraimu. Yosefu anawazia mambo yenye kufanyika katika nyumba, wakati bibi yake anacheka kwa kuona watoto wake wanacheza pamoja. Yosefu anacheka pia. Alijua kama Mungu alikuwa amemubariki.

Yosefu alipatia mutoto wake wa kwanza jina la Manase kwa sababu lilimaanisha mutu mwenye kusahaulisha. (Mwanzo 41:51) Mungu alikuwa amemubariki katika miaka yenye ilikuwa tu imepita. Baraka hizo zilituliza uchungu wenye alikuwa nao kwa sababu ya kukumbuka nyumbani kwao, ndugu zake, na baba yake. Ndugu zake wakubwa walimuchukia, na hilo lilibadilisha maisha yake. Walimushambulia, wakapanga kumuua, na kisha wakamuuzisha kwa wafanya-biashara wenye kusafiri ili akuwe mutumwa. Tangu wakati huo, maisha yake yalikuwa na mabadiliko mengi. Kwa miaka 12 hivi, alikuwa mutumwa na alifungwa katika gereza, hata wakati fulani alikuwa katika vifungo vya chuma. Lakini sasa ni yeye alikuwa na cheo cha pili katika inchi ya Misri kisha tu Farao! *

Kwa miaka mingi, Yosefu aliona mambo yanafanyika namna Yehova alikuwa ametabiri. Misri ilikuwa katika kipindi cha miaka saba ya chakula kingi, na Yosefu ndiye alisimamia kazi ya kukusanya chakula katika magala (dépôts). Wakati huo, yeye na Asenathi bibi yake walikuwa wamezaa watoto wawili. Lakini mara nyingi alikumbuka familia yake yenye ilikuwa mbali sana, zaidi sana Benyamini mudogo yake, na Yakobo baba yao mupendwa. Inawezekana Yosefu alikuwa anajiuliza ikiwa wote ni wazima na wako salama. Pengine alijiuliza pia ikiwa ndugu zake wakubwa walikuwa wamebadilisha tabia yao ya kukosa huruma ao ikiwa angeweza tena kupatana na familia yake na kuungana tena nao.

Ikiwa wivu, usaliti ao chuki vimefanya amani ya familia yako ipotee, wewe pia uko katika hali kama ya Yosefu. Kwa kuona namna Yosefu alisaidia familia yake, namna gani tunaweza kuiga imani yake?

‘MUENDE KWA YOSEFU’

Yosefu alikuwa na mambo mengi ya kufanya kila siku, na miaka ilipita mbio. Kama vile Yehova alimuonyesha Farao katika ndoto, kulikuwa miaka saba ya chakula kingi, na kisha miaka hiyo mambo yalibadilika sana. Mimea haikutoa chakula! Njaa ilianza kupiga inchi zenye kuwa karibu na Misri. Lakini kama vile Biblia inasema, ‘mukate ulipatikana katika inchi yote ya Misri.’ (Mwanzo 41:54) Bila shaka Wamisri walifaidika kwa sababu ya mambo yenye Yosefu alitabiri kwa musaada wa roho takatifu, na kwa sababu alisimamia mambo muzuri.

Kwa sababu Yosefu aliendelea kuwa munyenyekevu, Yehova aliendelea kumutumikisha

Inawezekana Wamisri walikuwa wenye shukrani kwa Yosefu na walimusifu kwa sababu alijua kusimamia mambo muzuri. Lakini Yosefu alipenda sifa yote imuendee Yehova Mungu wake. Ikiwa tuko na uwezo fulani na tunautumia ili kumutumikia Mungu kwa unyenyekevu, anaweza kutusaidia tutumie uwezo huo kwa njia yenye hatukuwazia.

Lakini kisha wakati fulani, Wamisri pia walipigwa na njaa. Wakati walimulilia Farao ili kumuomba musaada, aliwaambia: ‘Muende kwa Yosefu. Lolote atakalowaambia, mufanye.’ Kwa hiyo Yosefu akaanza kufungua magala ya chakula, na watu walikuwa wanakuja kununua.—Mwanzo 41:55, 56.

Lakini katika inchi za pembeni, watu hawakuwa na chakula. Familia ya Yosefu yenye ilikuwa inaishi mbali katika inchi ya Kanaani ilikuwa inateseka. Muzee Yakobo alisikia kuwa kuna chakula katika Misri, kwa hiyo alituma watoto wake katika inchi hiyo waende kununua chakula.—Mwanzo 42:1, 2.

Yakobo alituma watoto wake kumi, lakini hakutuma Benyamini, mutoto wake wa mwisho. Yakobo alikumbuka muzuri wakati alituma Yosefu mutoto wake mupendwa yeye peke yake, ili kuona ndugu zake wakubwa. Hiyo ndiyo ilikuwa mara yake ya mwisho kumuona. Ndugu wakubwa wa Yosefu walirudi nyumbani na nguo ya muzuri ya Yosefu yenye baba yake alimupatia ili kumuonyesha upendo. Walikuwa wamepasua-pasua nguo hiyo na kuijaza damu. Walimufanya muzee huyo mwenye huzuni aamini kama wanyama wa pori walimukula Yosefu.—Mwanzo 37:31-35.

“YOSEFU AKAKUMBUKA”

Kisha kusafiri kwa muda murefu, watoto wa Yakobo wakafika Misri. Wakati waliuliza juu ya kuuza chakula, waliambiwa waende kumuona mukubwa fulani wa serikali mwenye cheo cha juu aliyeitwa Zafenath-panea. (Mwanzo 41:45) Wakati walimuona, walijua kama yeye ni Yosefu? Hapana. Walimuona kuwa tu mutawala wa Misri mwenye cheo cha juu, mwenye angewasaidia. Ili kumuonyesha heshima, walifanya jambo fulani la kawaida, ni kusema, ‘walimuinamia kifudifudi.’—Mwanzo 42:5, 6.

Yosefu alitambua ndugu zake? Ndiyo, aliwatambua mara moja! Zaidi ya hilo, wakati aliona wanamuinamia, alikumbuka mara moja wakati alikuwa kijana. Biblia inatuambia kuwa, “Yosefu akakumbuka ndoto alizoota,” ndoto zenye Yehova alimuonyesha wakati alikuwa kijana. Ndoto hizo zilionyesha kuwa wakati fulani ndugu zake watamuinamia; na ni vile walikuwa wanafanya sasa! (Mwanzo 37:2, 5-9; 42:7, 9) Yosefu atafanya nini sasa? Atakumbatia ndugu zake? Ao atalipiza kisasi?

Yosefu alijua kama hakupaswa kutenda bila kufikiri. Ni wazi kuwa Yehova alikuwa anaongoza mambo yote yenye yalikuwa yanatendeka kwa sababu yalihusu kusudi lake. Alikuwa ameahidi kuwa atafanya watoto wa Yakobo wakuwe taifa kubwa. (Mwanzo 35:11, 12) Ikiwa ndugu za Yosefu bado walikuwa bila huruma, wenye kujipenda wenyewe na wanafiki, tabia hizo zingekuwa na matokeo mabaya sana kwa muda murefu! Tena, ikiwa Yosefu alitenda bila kufikiri angeumiza watu wengine wa familia yake wenye walibaki nyumbani. Pengine hata angetia baba yake na pia Benyamini katika hatari. Na pengine alijiuliza hata ikiwa walikuwa wangali wazima. Kwa hiyo, Yosefu hakujitambulisha kwa ndugu zake ili awajaribu na kuona ikiwa walikuwa wamebadilika. Kisha angejua sasa mambo yenye Yehova alipenda afanye.

Pengine hautajikuta katika hali kama hiyo. Lakini katika ulimwengu wa leo kukosa kuelewana na kutengana katika familia ni mambo yenye kuenea sana. Kwa sababu ya hali yetu ya zambi, tunaweza kutaka tu kufuata mawazo yetu na kutenda bila kufikiri wakati tunapambana na magumu. Ni jambo la hekima sana kufuata mufano wa Yosefu na kujikaza kutambua namna Yehova anapenda tushugulikie mambo. (Methali 14:12) Kumbuka kuwa ni jambo la maana kufanya amani pamoja na watu wa familia, lakini ni jambo la maana hata zaidi kufanya amani pamoja na Yehova na Mwana wake.—Mathayo 10:37.

‘MUTAJARIBIWA’

Ili kujua namna mioyo ya ndugu zake ilikuwa, Yosefu alitumia njia mbalimbali ili kuwajaribu. Kwanza alitumia mutafsiri ili kuzungumuza nao kwa ukali; aliwashitaki kuwa wapelelezi. Ili kujitetea, walimuelezea juu ya familia yao; hata walimuambia habari ya maana sana. Walimuambia kama walikuwa na mudogo yao wa mwisho aliyebaki nyumbani. Yosefu alijikaza ili wengine wasione namna alijisikia moyoni. Kweli mudogo yake alikuwa angali muzima? Sasa Yosefu alijua jambo la kufanya. Alisema hivi: ‘Hivyo ndivyo mutajaribiwa,’ kisha akawaambia kama ni lazima aone mudogo yao wa mwisho. Kisha wakati fulani, alikubali kuwaacha warudi kwao ili wamuletee mudogo yao wa mwisho ikiwa tu mumoja kati yao atakubali kubaki Misri kama mufungwa.—Mwanzo 42:9-20.

Wakati ndugu za Yosefu walikuwa wanazungumuzia mambo hayo, walijilaumu kwa sababu ya zambi kubwa yenye walifanya miaka 20 mbele ya hapo. Hawakujua kama Yosefu alikuwa anaelewa mazungumuzo yao. Walisema hivi: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu, kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza. Ndiyo sababu taabu hii imetupata.” Yosefu alielewa mambo yenye walikuwa wanasema. Kwa hiyo, aligeuka na kuenda pembeni ili wasione machozi yake. (Mwanzo 42:21-24) Alijua kuwa toba ya kweli haiko tu kuhuzunika juu ya matokeo ya matendo mabaya. Kwa hiyo akaendelea kuwajaribu.

Aliwaacha warudi nyumbani kwao lakini alibakia na Simeoni kama mufungwa. Pia aliambia watumishi wake wafiche feza katika mifuko yenye walitumia kubeba chakula nyumbani. Ndugu za Yosefu walirudi nyumbani na walifanya yao yote ili Yakobo akubali kuwaruhusu warudi Misri na Benyamini mutoto wake mupendwa. Wakati walifika Misri, walimuambia waziwazi mutumishi wa Yosefu kuwa walikuta feza katika mifuko yao ya chakula, na walikuwa tayari kurudisha feza hizo zote. Hilo lilikuwa jambo la muzuri, lakini Yosefu alipenda kujua hali yao ya kweli ya moyoni. Aliwaalika kula chakula na alifanya yake yote ili wasione namna alikuwa anajisikia kwa sababu ya kumuona Benyamini. Kisha, aliwapatia tena chakula cha kubeba nyumbani, lakini sasa akaficha kikombe cha feza katika mufuko wa Benyamini.—Mwanzo 42:26–44:2.

Yosefu akatumia mutego huo ili kuwajaribu. Aliambia watumishi wake wawafuate, wawakamate, na kuwashitaki kuwa wameiba kikombe hicho. Wakati kilipatikana katika mufuko wa Benyamini wote walirudishwa tena kwa Yosefu. Wakati huo Yosefu alikuwa na nafasi ya kujua ndugu zake ni watu wa namna gani. Yuda ndiye alisema kwa ajili yao wote. Alimuomba sana Yosefu awahurumie na hata alisema kuwa wote 11 wako tayari kuwa watumwa huko Misri. Yosefu alijibia kama ni Benyamini tu ndiye atakuwa mutumwa lakini wengine walipaswa kurudi nyumbani.—Mwanzo 44:2-17.

Yuda alisema maneno yenye kuonyesha mambo yenye kuwa katika moyo wake. Alisema hivi: ‘Yeye tu ndiye aliyesalia [aliyebaki] wa mama yake, na baba yake anamupenda.’ Bila shaka maneno hayo yalimugusa Yosefu kwa sababu alikuwa mutoto wa kwanza wa Raheli, bibi mupendwa wa Yakobo, aliyekufa wakati alikuwa anazaa Benyamini. Kwa kweli, Yosefu na Yakobo waliendelea kumukumbuka Raheli. Pengine ni jambo hilo lilifanya Yosefu amupende sana Benyamini.—Mwanzo 35:18-20; 44:20.

Yuda aliendelea kumuomba Yosefu asimufanye Benyamini kuwa mutumwa. Hata alisema kuwa yeye iko tayari kuwa mutumwa pa nafasi ya Benyamini. Kisha alimalizia kwa kusema maneno haya yenye kutoka moyoni: ‘Kwa maana ninawezaje kwenda kwa baba yangu bila yeye nisije nikautazama musiba utakaomupata baba yangu!’ (Mwanzo 44:18-34) Ilikuwa wazi kabisa kuwa Yuda alikuwa amebadilika. Alionyesha moyo wa toba, lakini pia alionyesha moyo muzuri wa huruma, kuhangaikia wengine na kujitia pa nafasi ya wengine.

Yosefu aliona kuwa ndugu zake walihuzunika kwa sababu ya mambo yenye walimufanyia

Yosefu hakuweza tena kujizuia. Alipaswa kufunua namna alikuwa anajisikia katika moyo. Kisha kuambia watumishi wake wote waondoke, alilia kwa sauti kubwa. Sauti yake ilifika hata kwenye nyumba ya Farao. Mwishowe alijitambulisha kwa ndugu zake: “Mimi ni Yosefu ndugu yenu.” Walishangaa sana, na Yosefu aliwakumbatia na kuwaambia kuwa amewasamehe kutoka moyoni mambo yote yenye walimufanyia. (Mwanzo 45:1-15) Kwa kufanya hivyo, alifuata mufano wa Yehova ambaye iko tayari kusamehe. (Zaburi 86:5) Sisi pia tuko tayari kusamehe wengine?

“UNGALI HAI”!

Wakati Farao alisikia mambo yenye yalifanya makelele yakuwe katika nyumba ya Yosefu, alimuambia alete baba yake mwenye kuzeeka na familia yake yote Misri. Kisha siku kidogo, Yosefu alionana tena na baba yake mupendwa. Yakobo alilia na kusema hivi: “Sasa niko tayari kufa, kwa kuwa nimeuona uso wako, kwa maana ungali hai [muzima].”—Mwanzo 45:16-28; 46:29, 30.

Hata hivyo, Yakobo aliishi tena miaka 17 katika inchi ya Misri, mupaka wakati aliwaambia watoto wake 12 maneno ya kuwabariki yenye kuwa na maana ya unabii. Alimupatia Yosefu mutoto wake wa 11 sehemu mbili za baraka; kwa kawaida ni mutoto wa kwanza ndiye alipaswa kupokea sehemu mbili. Yakobo alisema kuwa Yosefu atakuwa baba wa makabila mbili ya Israeli. Lakini Yuda, mutoto wake wa ine mwenye alionyesha moyo wa toba kuliko ndugu zake wengine alipata nini? Alipata baraka kubwa: Masiya angezaliwa katika kizazi chake!—Mwanzo, sura ya 48 na 49.

Wakati Yakobo alikufa na miaka 147, ndugu za Yosefu waliogopa kama Yosefu mwenye mamlaka atalipiza kisasi. Lakini Yosefu aliwatuliza kwa upendo. Alikuwa anasema kama, kwa sababu ni Yehova alipenda familia yao ihamie Misri, ndugu zake walipaswa kuacha kujisikia mubaya kwa sababu ya mambo yenye yalitokea zamani. Sasa aliongezea ulizo hili la maana sana: “Mimi niko mahali pa Mungu?” (Mwanzo 15:13; 45:7, 8; 50:15-21) Yosefu alimuona Yehova kuwa Muamuzi mukamilifu. Yosefu alikuwa nani ili ahukumu watu wenye Yehova alikuwa amesamehe?—Waebrania 10:30.

Kuna wakati unaona kuwa ni vigumu kusamehe? Inaweza kuwa vigumu zaidi sana kusamehe mutu mwenye ametukosea kimakusudi. Lakini ikiwa tunasamehe watu wenye wanatuomba musamaha kutoka moyoni, tutasaidia watu wengi kupona vidonda vya moyoni; sisi pia tutapona vidonda vyetu. Tena tutaiga imani ya Yosefu na mufano wa Yehova, Baba yake mwenye kusamehe.

^ fu. 4 Soma habari zenye kichwa “Uige Imani Yao” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 8, 2014; tarehe1 Mwezi wa 11, 2014; na tarehe 1 Mwezi wa 2, 2015.