Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Sikupenda Kufa!

Sikupenda Kufa!
  • ALIZALIWA MWAKA WA: 1964

  • INCHI: UINGEREZA

  • ALIKUWA: MAMA KIJANA MWENYE TABIA ZA MUBAYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI

Nilizaliwa katika Paddington, sehemu fulani yenye watu wengi sana ya muji wa Londres, Uingereza. Niliishi na mama yangu na pia dada zangu watatu. Baba yangu aliondoka na kurudi nyumbani mara kwa mara kwa sababu ya pombe.

Wakati nilikuwa mutoto, mama yangu alinifundisha kusali kila usiku. Nilikuwa na Biblia ndogo yenye ilikuwa na nyimbo za kitabu cha Zaburi tu, zenye nilipanga katika namna yenye ingenisaidia kuimba. Nakumbuka siku moja nilisoma maneno haya katika kitabu fulani: “Siku moja hakutakuwaka kesho.” Maneno hayo yalibakia katika akili yangu na yalifanya nikose usingizi usiku wote na kuanza kuwaza juu ya wakati wenye kuja. Niliwaza, ‘Maisha yanapaswa kuwa na kusudi fulani. Sababu gani niko duniani?’ Sikupenda kufa!

Nilianza kupenda kujua mambo ya mashetani. Nilijaribu kuzungumuza na wafu, kutembelea makaburi pamoja na marafiki wangu wa masomo, na kuangalia filme zenye kuogopesha sana pamoja nao. Tuliona kama kufanya hivyo kulifurahisha na pia kulileta woga.

Nilianza kuwa na tabia za mubaya wakati nilikuwa na miaka 10 tu. Nilianza kuvuta tumbako, na bila kukawia nikakuwa mutumwa wa tumbako. Kisha wakati fulani, nikaanza kuvuta bangi yenye kuitwa marijuana. Wakati nilieneza miaka 11, nikaanza kunywa pombe. Hata kama sikupenda onjo ya pombe, nilifurahia matokeo ya ulevi. Nilipenda pia muziki na kucheza. Nilienda kwenye mahali pa kunywa pombe usiku (boîtes de nuit) na kwenye karamu wakati wowote ningeweza kufanya hivyo. Nilizoea kuondoka usiku kwa siri na kurudia kwa siri mbele ya asubui. Kwa sababu ya kuchoka, nilikuwa ninafanya kama vile ninaenda kwenye masomo lakini sikuwa ninaingia ndani. Mara nyingi wakati niliingia katika masomo, nilikuwa ninakunywa pombe wakati mwalimu alikuwa anafundisha.

Nilipata alama za chini sana katika mwaka wangu wa mwisho wa masomo. Mama yangu alivunjika moyo na kukasirika sana kwa sababu hakujua namna nilikuwa na tabia ya mubaya. Tulikosana naye, na nikatoka nyumbani. Kwa muda fulani, niliishi na rafiki yangu mwanaume mwenye kuitwa Tony. Rafiki huyo alikuwa rasta. Alikuwa anafanyia wengine mambo mabaya yenye haikuonekana waziwazi na alijulikana kuwa mukali sana. Kisha wakati kidogo, nikapata mimba, na wakati nilikuwa na miaka 16 tu nikazaa mutoto wetu mwanaume.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU

 

Nilikutana na Mashahidi wa Yehova mara ya kwanza wakati nilikuwa ninaishi katika nafasi moja yenye kuwa kama hoteli kwa ajili ya mama wenye hawajaolewa na watoto wao. Wakubwa wa eneo walikuwa wamenipatia chumba moja. Dada wawili Mashahidi wa Yehova walizoea kutembelea mama fulani vijana. Siku moja nilijiunga katika mazungumuzo yao. Nilikuwa na kusudi la kuonyesha kama Mashahidi wanafundisha uongo. Lakini walinijibia kila ulizo langu kwa upole na kwa njia yenye kuwa wazi wakitumia Biblia. Walikuwa wema na wenye kufurahia wengine; hilo lilinivutia kwao. Kwa hiyo, nilikubali waanze kunifundisha Biblia.

Bila kukawia, nilijifunza jambo moja katika Biblia lenye lilibadilisha maisha yangu. Tangu nilikuwa kijana, nilikuwa ninaogopa kufa. Lakini sasa nilivumbua mafundisho ya Yesu juu ya ufufuo! (Yohana 5:28, 29) Tena, nilijifunza kwamba Mungu ananihangaikia. (1 Petro 5:7) Zaidi sana maneno ya andiko la Yeremia 29:11 yalinigusa moyo. Maneno hayo yanasema hivi: ‘Kwa maana mimi najua vema mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi, asema Yehova, mawazo ya amani, wala si ya musiba, ili kuwapa ninyi wakati ujao na tumaini.’ Nilianza kuamini tumaini la kuishi milele katika dunia Paradiso.—Zaburi 37:29.

Mashahidi wa Yehova walionyesha kwamba wananipenda kwelikweli. Wakati nilienda kwenye mikutano yao kwa mara ya kwanza, niliona hali ya muzuri sana, kila mutu alinikaribia! (Yohana 13:34, 35) Hilo lilikuwa tofauti kabisa na namna kanisa fulani la eneo letu lilinitendea. Mashahidi walinikaribisha bila kuangalia hali yangu. Walipitisha wakati pamoja na mimi, walinihangaikia, na pia walinisaidia kwa njia ya kimwili. Nilijisikia kuwa katika familia kubwa yenye upendo.

Mambo yenye nilijifunza katika Biblia yalifanya nione kwamba ninapaswa kufanya mabadiliko katika maisha yangu ili kuishi kulingana na kanuni za juu za Mungu. Haikuwa mwepesi kuacha kuvuta tumbako. Na nilitambua kwamba, miziki fulani ilikuwa inaongeza tamaa yangu ya kuvuta marijuana, kwa hiyo, niliacha kuisikiliza. Kwa sababu sikupenda kulewa, niliacha kuenda kwenye karamu mbalimbali na mahali watu wanakunywa pombe usiku. Kisha nilitafuta marafiki wengine wenye walikuwa na tabia ya muzuri yenye ingenisaidia.—Methali 13:20.

Wakati huohuo, Tony alikuwa pia ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu Mashahidi walikuwa wanajibu maulizo yake kwa kutumia Biblia, alifikia pia kuamini kabisa kweli yenye alikuwa anajifunza. Alifanya mabadiliko makubwa sana katika maisha yake: akaacha marafiki wake wenye jeuri, kufanyia wengine mambo mabaya yenye haikuonekana waziwazi, na pia akaacha kuvuta marijuana. Ili kumufurahisha Yehova kabisa, sisi wawili tuliona kama tulipaswa kubadilisha mwenendo mubaya na kutolea mutoto wetu nafasi salama ya kukomalia. Tulioana katika mwaka wa 1982.

“Sikose tena kulala usiku kwa sababu ya kuwaza juu ya wakati wenye kuja ao juu ya kifo”

Nakumbuka namna nilikuwa ninatafuta habari mbalimbali katika Munara wa Mulinzi na Amuka! * zenye zilizungumuzia watu wenye walifikia kufanya mabadiliko yenye nilipenda kufanya. Mifano ya watu hao ilinitia moyo sana! Ilinitia nguvu ya kuendelea kujikaza, bila kuchoka. Niliendelea kusali kwa Yehova ili asiniache. Mimi na Tony tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova Mwezi wa 7, 1982.

FAIDA YENYE NIMEPATA

Niko muzima leo kwa sababu nilifanya urafiki pamoja na Yehova Mungu. Mimi na Tony tumejionea musaada wa Yehova wakati wa magumu mengi yenye tumepata. Tumejifunza kumutegemea Mungu wakati wa magumu, na tumeona kwamba anaendelea kila mara kusaidia familia yetu.—Zaburi 55:22.

Nimefurahi kusaidia watoto wetu, mwanaume na mwanamuke, wamujue pia Yehova kama vile mimi. Na sasa nafurahi pia kuona watoto wao wakiendelea kujifunza juu ya Mungu.

Sikose tena kulala usiku kwa sababu ya kuwaza juu ya wakati wenye kuja ao juu ya kifo. Mimi na Tony tuko na kazi ya kutembelea makutaniko mbalimbali ya Mashahidi wa Yehova kila juma ili kuwatia moyo. Tunajiunga nao ili kufundisha watu wengine kwamba, ikiwa wanamuamini Yesu, wao pia wanaweza kufurahia uzima wa milele.

^ fu. 18 Inachapishwa pia na Mashahidi wa Yehova.