Ona video zinazopatikana

Tukio la Maana Sana!

Kutolewa kwa Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya

Tukio la Maana Sana!

Tarehe 24 Mwezi wa 8, 2018, kulikuwa tukio la maana sana: Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ilitolewa mu Swahili (Congo).

Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ni tafsiri yenye kupendeza juu haina makosa na inatafsiri kwa uaminifu ujumbe wa Mungu wenye uliongozwa na roho yake. (2 Timoteo 3:16) Tafsiri hii imeepuka muelekeo gani wenye haufae wenye unatumiwa mu tafsiri za sasa za Biblia? Ni nani waliitafsiri? Na ni nini inaweza kukuhakikishia kama Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ni ya kutumainika?

Je, Biblia yangu haina makosa?

Declan Hayes, Profesa wa Biashara ya Kimataifa aliandika: “Biblia njo kitabu chenye watu wanauza sana kila mwaka.” Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kwa sababu watu wanatamani tu kuchapisha kitabu chenye kitauzwa sana, ile inafanya wasihangaikie sana kama Biblia yao iko na makosa ao hapana. Kwa mufano, Biblia moja inatosha maandiko yenye wachapishaji wake wanaona kuwa “haipendeze.” Biblia ingine inabadilisha maneno ao misemwa yenye inaweza kuuzi wasomaji wa leo. Kwa mufano, inatafuta kuvutia watu fulani kwa kumuita Mungu “Baba-Mama.”

Pengine muelekeo wenye haufae kabisa ni ule wenye unahusu jina la pekee la Mungu, ni kusema, Yehova. (Watu fulani wenye elimu mingi wanatafsiri ile jina kuwa “Yahweh.”) Mu kopi za zamani za Biblia, jina la Mungu liliandikwa kwa konsonanti ine za Kiebrania zenye zinaweza kutafsiriwa YHWH ao JHVH. Jina hili lenye linamutofautisha na miungu ingine linapatikana mara 7 000 mu Maandiko ya Kiebrania * peke yake. (Kutoka 3:15; Zaburi 83:18) Basi, ni wazi kama, Muumbaji wetu alipenda waabudu wake wajue na watumie jina lake!

Lakini, mu miaka mingi yenye ilipita, kuogopa mambo ya ushirikina ilifanya Wayahudi waache kutaja jina la Mungu. Kisha, Wakristo pia walifikia kuambukizwa na ile mawazo ya ushirikina. (Matendo 20:29, 30; 1 Timoteo 4:1) Leo, watafsiri mingi wa Biblia wanatosha jina la Mungu na kutia jina la cheo “Bwana” pa nafasi yake. Biblia fulani za leo za Swahili (Congo) hazitaje hata neno “jina” mu Yohana 17:6, kwenye Yesu alisema: “Nimejulisha jina lako.” Biblia Habari Njema inatafsiri ile mustari hivi: “Nimekufanya ujulikane.”

Watu fulani wenye elimu mingi wanasema kama wanatoshaka jina la Mungu na kutia “Bwana” pa nafasi yake juu tu ya kufuata desturi. Wengine wanasema kama wanaamuaka kufanya vile ili watu wauze sana Biblia zao. * Lakini Yesu alilaumu tabia ya kufuata desturi zenye zinamukosea Mungu heshima. (Matayo 15:6) Zaidi ya ile, wazo la kutosha jina la Mungu na kutia jina la cheo pa nafasi yake halina musingi mu Maandiko. Yesu Kristo iko na majina mingi ya cheo, kwa mufano, anaitwa “Neno la Mungu” na “Mufalme wa wafalme.” (Ufunuo 19:11-16) Je, jina la Yesu linapaswa kutoshwa na kutia moja ya majina yake ya cheo pa nafasi ya jina lake?

Lakini, jambo la maana hapa haiko tu elimu mingi. Fikiria maneno hii yenye mushauri moja wa India wa mambo ya kutafsiri Biblia alisema kuhusu kutosha jina la Mungu mu Biblia: “Wahindu hawapendezwe na jina la cheo la Mungu; wanataka kujua jina la pekee la Mungu, na kama hawajue ile jina hawawezi kuwa na uhusiano na mwenye ile jina.” Ni vile kabisa kuhusu wale wote wenye wanamutafuta Mungu. Kujua jina la Mungu ni jambo la maana juu ya kufahamu kwamba yeye ni Mutu wa kweli kabisa, hapana nguvu fulani tu yenye haina utu. (Kutoka 34:6, 7) Njo maana Biblia inasema: “Kila mutu mwenye anaitia jina la Yehova ataokolewa.” (Waroma 10:13) Waabudu wa Mungu wanapaswa kabisa kutumia jina lake!

Tafsiri ya Biblia yenye inaheshimia jina la Mungu

Ilikuwa tukio la maana sana mu mwaka wa 1950 wakati chapa ya Kiingereza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilichapishwa mara ya kwanza. Mu miaka kumi yenye ilifuata, Maandiko ya Kiebrania ilichapishwa hatua kwa hatua. Mu mwaka wa 1961, Biblia yote ilitolewa mu buku moja mu Kiingereza. Jambo la kupendeza ni kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mupya inatumia jina “Yehova” kila mahali kwenye linapatikana mu Agano la Kale, karibu mara 7 000. Ya kupendeza tena zaidi ni kurudisha jina la Mungu mara 237 mu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.” *

Kurudisha ile jina kunamuletea Mungu heshima na pia kunatusaidia tuelewe mambo muzuri zaidi. Kwa mufano, tafsiri mingi zinatafsiri hivi Matayo 22:44: “Bwana alimuambia Bwana wangu.” Lakini, ni nani mwenye anasema na mwingine? Tafsiri ya Ulimwengu Mupya inataja bila makosa andiko la Zaburi 110:1 wakati inatafsiri ile mustari hivi: “Yehova alimuambia Bwana wangu.” Ile inasaidia wasomaji waone tofauti kubwa yenye iko kati ya Yehova Mungu na Mwana wake.

Ni nani waliitafsiri?

Tafsiri ya Ulimwengu Mupya inachapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society, shirika la kisheria lenye linawakilisha Mashahidi wa Yehova. Mu zaidi ya miaka mia moja, Mashahidi wa Yehova wamechapisha na kugawanya Biblia mu dunia yote. Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ilitayarishwa na kikundi cha Mashahidi wa Yehova chenye kinajulikana kwa jina la Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya Ulimwengu Mupya. Kuliko kujitafutia sifa, washiriki wa ile halmashauri waliomba majina yao isitajwe, hata kisha kifo yao.​—1 Wakorinto 10:31.

Juu ya nini tafsiri hii inaitwa Tafsiri ya Ulimwengu Mupya? Maneno ya utangulizi ya toleo la 1950 ilieleza kwamba ile jina inaonyesha uhakika wenye nguvu wa kwamba wanadamu wako “ku mulango wa ulimwengu mupya” wenye uliahidiwa mu 2 Petro 3:13. Kama vile ile halmashauri iliandika, mu “hii wakati ya kutoka mu ulimwengu wa zamani na kuingia mu ulimwengu mupya wa haki,” inaomba tafsiri za Biblia ziache “kweli safi ya Neno la Mungu” iangaze kabisa.

Tafsiri yenye haina makosa

Jambo la kwanza lenye lilihangaikiwa sana ni kutoa tafsiri yenye haina makosa. Watafsiri wa toleo la Kiingereza walitafsiri moja kwa moja kutoka mu luga ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki, wakitumia maandishi ya muzuri zaidi yenye ilipatikana. Uangalifu wa pekee ulitumiwa juu ya kutafsiri maandishi ya zamani kwa uaminifu kadiri iliwezekana​—lakini mu luga yenye wasomaji wa leo wanaweza kuelewa muzuri.

Kwa hiyo haishangaze kwamba watu fulani wenye elimu mingi wamesifu Tafsiri ya Ulimwengu Mupya juu ya uaminifu wake na juu haina makosa. Profesa Benjamin Kedar, mutu mwenye elimu mingi ya luga ya Kiebrania mu inchi ya Israeli, alisema hivi mu mwaka wa 1989: “Mu utafiti wangu wa luga kuhusiana na Biblia ya Kiebrania na tafsiri mbalimbali, mara mingi ninachunguzaka toleo la Kiingereza lenye kuitwa New World Translation (Tafsiri ya Ulimwengu Mupya). Kwa kufanya vile, ninapata uhakikisho zaidi na zaidi kwamba tafsiri hii ilifanywa kwa uaminifu juu ya kutokeza maandishi yenye haina makosa kadiri iliwezekana.”

Kufanya Biblia ipatikane mu luga mingi

Kwa kufaa kabisa, Mashahidi wa Yehova wamefanya Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ipatikane pia mu maeneo kwenye watu hawazungumuze Kiingereza. Kwa sasa inachapishwa, ikiwa nzima ao ikiwa sehemu, mu luga 169. Juu kazi ikuwe mwepesi, walitokeza njia ya kutafsiri Biblia yenye inachanga kujifunza maneno ya Biblia na teknolojia ya ordinatere. Biro ya kusimamia kazi za kutafsiri ilianzishwa juu ya kusaidia watafsiri. Baraza Lenye Kuongoza la Mashahidi wa Yehova linasimamia kwa ukaribu kazi ya kutafsiri Biblia kupitia Halmashauri ya Uandikaji. Lakini kazi hii inafanywa namna gani kabisa?

Kwanza, Wakristo wenye kubatizwa wanachaguliwa juu ya kufanyiza timu ya kutafsiri. Uzoefu umeonyesha kwamba wakati watafsiri wanatumika pamoja wakiwa kikundi wanatoa tafsiri ya muzuri zaidi, yenye usawaziko, kuliko wakati kila mutu anatumika peke yake. (Mezali 11:14) Kwa kawaida, kila mushiriki wa ile timu iko na uzoefu kwa sababu ni mutafsiri wa vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Kisha, timu inapata mazoezi ya kufaa kuhusu kanuni za musingi za kutafsiri Biblia na namna ya kutumia programu za ordinatere zenye zimefanywa juu tu ya kutafsiri Biblia.

Timu ya kutafsiri inaombwa itafsiri Biblia yenye haina makosa lakini yenye watu wa kawaida wataelewa kwa njia yenye kuwa mwepesi. Timu inapaswa kutafsiri neno kwa neno wakati inawezekana, na wakati ileile, haipaswe hata kidogo kubadilisha maana ya maandishi ya kwanza. Ile inafanywa namna gani? Fikiria hii Biblia mupya yenye imetolewa. Timu ya kutafsiri ilianza kwa kuchagua maneno ya Swahili (Congo) yenye inatafsiri maneno yote ya maana yenye kutumiwa mu Tafsiri ya Ulimwengu Mupya ya Kiingereza. Programe ya ordinatere yenye kuitwa Mufumo wa Watchtower wa Kutafsiri ilionyesha maneno ya Biblia yenye kufanana na pia maneno yenye kuwa na maana moja. Pia ilionyesha maneno ya Kigiriki ao ya Kiebrania yenye maneno ya Kiingereza ilitokana nayo juu mutafsiri aweze kuchunguza namna ile maneno ya Kigiriki ao ya Kiebrania ilitafsiriwa fasi ingine mu tafsiri ya Kiingereza. Ile yote ilisaidia sana kuchagua maneno ya Swahili (Congo). Wakati timu ya kutafsiri ilikubaliana juu ya ile maneno, walianza kutafsiri Biblia, wakitumia ordinatere juu ya kuona maneno ya Swahili (Congo) wakati walikuwa wanatafsiri kila mustari.

Lakini, kutafsiri haiko tu kubadilisha maneno kutoka mu luga moja mupaka luga ingine. Kazi mingi ilifanywa juu ya kuhakikisha kwamba maneno yenye ilichaguliwa ya Swahili (Congo) ilitoa bila kukosea wazo lenye kupatana na Maandiko mu kila habari. Pia watafsiri walihakikisha kwamba sarufi na mutiririko wa maneno uko muzuri na unaeleweka. Basi, kazi kubwa yenye ilifanywa juu ya kutafsiri Biblia hii inaonekana wazi. Toleo la Swahili (Congo) la Tafsiri ya Ulimwengu Mupya linatafsiri Neno la Mungu mu njia yenye kuwa mwepesi kusoma, yenye kuwa wazi, yenye kueleweka, na yenye kufuata kwa uaminifu maandishi ya zamani. *

Tunakutia moyo uchunguze wewe mwenyewe Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya. Unaweza kuisoma ku Enternete ao mu JW Library, ao unaweza kupata kopi yake mu kutaniko la Mashahidi wa Yehova la karibu na kwenye unaishi. Uisome na uko hakika kwamba inatafsiri bila makosa maneno ya Mungu mu luga yako mwenyewe. Bila shaka, utakubali kama kutolewa kwa Biblia​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya mu Swahili (Congo) ni tukio la maana sana!

 

Mambo ya maana ya Tafsiri ya Ulimwengu Mupya

 

Habari Fulani za Kujifunza Katika Neno la Mungu: Iko na maandiko ya Biblia yenye inajibia maulizo 20 juu ya mafundisho ya musingi ya Biblia

Tafsiri yenye haina makosa: Uangalifu mukubwa ulifanywa juu ya kutafsiri maneno ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki mu Kiingereza na kisha mu Swahili (Congo) bila makosa na kwa uaminifu kadiri iliwezekana

Referanse za pembeni: Zinapeleka musomaji ku maandiko yenye inapatana

Nyongeza A: Inafasiria sehemu za tafsiri hii mupya yenye ilirekebishwa, sawa vile muundo wake wa maneno na maneno yenye ilibadilika na namna inatafsiri jina la Mungu

Nyongeza B: Ndani ya nyongeza hii muko sehemu 15 za rangi mbalimbali zenye ziko na karte na michoro

^ fu. 7 Watu mingi wanaiita kuwa Agano la Kale.

^ fu. 9 Kwa mufano, muratibu wa mupango wa kutafsiri New International Version aliandika hivi: “Yehova ni jina la Mungu lenye linamutofautisha na miungu ingine na kusema kweli tunapaswa kulitumia. Lakini tulitia dola milioni 2. 25 mu mupango wa kutafsiri Biblia hii na njia ya kupoteza zile feza ni kutafsiri kwa mufano, Zaburi 23 kwa kusema, ‘Yahweh ni muchungaji wangu.’ Kama tu tunafanya vile, pale tutakuwa tumefanya kazi ya kutafsiri bure.”

^ fu. 12 Watu mingi wanaiita kuwa Agano Jipya.

^ fu. 24 Juu ya kupata habari zaidi kuhusu kanuni za kutafsiri Biblia na mambo ya maana ya toleo la Swahili (Congo), tafazali soma habari zenye zinapatikana mu nyongeza A1 na A2 ya Tafsiri ya Ulimwengu Mupya.