Hamia kwenye habari

FEBRUARI 28, 2022
JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA KONGO

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Kipende

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Kipende

Februari 20, 2022, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ilitolewa katika lugha ya Kipende kwenye programu iliyorekodiwa awali. Ndugu Nicolas Hifinger, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Kongo (Kinshasa), alitoa toleo la kielektroni la Biblia, kwa wasikilizaji 10,000 hivi. Nakala zilizochapishwa zitapatikana Aprili 2022.

Historia ya Mashahidi wa Yehova katika lugha ya Kipende, ilianza katika miaka ya 1960 hivi, wakati mwanamume mmoja aliyeitwa Makanda Madinga Henri, alipopewa nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi. Baada ya kusoma gazeti hilo, alisadiki kwamba habari alizosoma zilikuwa za kweli na akaanza kuwaambia wengine mambo aliyokuwa akijifunza. Hatimaye, alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Baadaye, kutaniko la kwanza la lugha ya Kipende lilianzishwa huko Kiefu katika mwaka wa 1979.

Ofisi ya utafsiri ya Kipende iliyo Kikwit, kilometa 500 hivi kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Kinshasa

Tafsiri hii itawasaidia ndugu na dada zetu katika funzo lao la kibinafsi na wanapohubiri habari njema. Kwa mfano, Ndugu Hifinger alieleza kwamba toleo hili jipya “ni sahihi na linaloeleweka” na “linarudisha jina la Yehova kila mahali lilipopatikana katika hati za awali.”

Tunasali kwamba toleo hili la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya litawasaidia akina ndugu kuendelea “kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.”—Wakolosai 1:10.