Hamia kwenye habari

Kushoto: Ndugu Nathan H. Knorr na Frederick Franz wakiwatembelea ndugu na dada jijini Bogotá mwaka wa 1946. Kulia: Wamishonari nchini Kolombia (safu ya juu, kuanzia kushoto kwenda kulia) Olaf Olson, James Webster, Quin Dale Lauderdale; (safu ya chini, kuanzia kushoto kwenda kulia) Anne Lauderdale, Helen Langford, na Jewel Harper

APRILI 12, 2022
KOLOMBIA

Miaka Mia Moja ya Utendaji wa Kitheokrasi Nchini Kolombia

Miaka Mia Moja ya Utendaji wa Kitheokrasi Nchini Kolombia

Kufikia 2022, Mashahidi wa Yehova wametimiza miaka 100 tangu walipoanza kuhubiri nchini Kolombia. a

Heliodoro Hernández

Katika mwaka wa 1922, Heliodoro Hernández, ambaye alipenda sana kusoma Biblia, aliazima nakala kadhaa za gazeti la Mnara wa Mlinzi kutoka kwa rafiki yake ambaye hakuwa Shahidi wa Yehova. Heliodoro alitambua haraka kwamba alikuwa amepata kweli na hivyo akaanza kuwaeleza watu wengine habari alizojifunza. Baada ya kuhubiri kwa miaka miwili, alikutana na Juan Estupiñán, ambaye alijiunga naye kuhubiri habari njema. Wote wawili walibatizwa mwaka wa 1932.

Juan Estupiñán

Baadaye, Watchtower Society iliwatumia Ndugu Hernández na Ndugu Estupiñán mashine ambayo ingeweza kucheza hotuba zilizorekodiwa. Hivyo, walichezea watu walioishi katika Milima ya Andes hotuba kama vile “Ukweli Kuhusu Utatu” na “Mwisho wa Ulimwengu.” Mara nyingi, walikabili upinzani kwa sababu maeneo hayo yana uvutano mkubwa wa Kanisa Katoliki.

Wamishonari kutoka Shule ya Gileadi walitumwa Kolombia mwaka wa 1945. Ndugu Olaf Olson, mmoja wa Wamishonari hao, alisema hivi baadaye katika simulizi la maisha yake: “Kuna kondoo wengi wa Yehova huku, na tunafurahi kwamba Yehova ametutuma sisi kuwatafuta na kuwalisha.”

Mei 1, 1946, ofisi ya tawi ilianzishwa nchini Kolombia ili kusimamia kazi. Ndugu Arthur Green, aliyekuwa mtumishi wa kwanza wa ofisi ya tawi, aliandika hivi: “Kwa msaada wa roho ya Yehova yenye nguvu, msingi wa ibada safi unawekwa nchini Kolombia.”

Leo kuna zaidi ya Mashahidi 190,000 wa Yehova wanaohubiri kwa bidii habari njema nchini Kolombia.

Kolombia inajulikana kwa ardhi yake yenye rutuba nyingi na mawe ya thamani yanayovutia. Lakini umaridadi wa kweli wa nchi hiyo unaonekana kwenye “vitu vyenye thamani,” yaani, watu ambao Yehova anaendelea kuwavuta kwake. Tunashangilia kuona Yehova akiendelea kubariki kazi ya kuhubiri ambayo ‘inajaza nyumba yake utukufu.’​—Hagai 2:7.

a Mwaka 1931, Wanafunzi wa Biblia walianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova.