Hamia kwenye habari

Juu kushoto: Barua ya Machi 15, 2023, kutoka kwa waziri wa elimu. Chini: Baadhi ya wanafunzi Mashahidi ambao walifukuzwa shuleni na wazazi wao

MEI 1, 2023
RWANDA

Wizara ya Elimu Nchini Rwanda Yatetea Haki ya Watoto wa Shule ya Uhuru wa Ibada

Wizara ya Elimu Nchini Rwanda Yatetea Haki ya Watoto wa Shule ya Uhuru wa Ibada

Mnamo Machi 15, 2023, waziri wa elimu wa Rwanda aliamuru shule nchini kote kurudisha shuleni watoto Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wamefukuzwa kwa sababu ya kukataa kushiriki katika desturi za kidini ambazo zilikiuka imani yao ya kidini. Kulikuwa na watoto 80 hivi ambao walikuwa wamefukuzwa shuleni.

Waziri huyo wa elimu aliamuru watoto wasifukuzwe tena katika barua yake aliyowaandikia meya wa wilaya zote na maofisa wanaoshughulikia shule nchini Rwanda. Akirejelea Katiba ya Jamhuri ya Rwanda, alisema hivi: “Kila Mnyarwanda ana haki ya kupata elimu. Isitoshe, serikali imemhakikishia uhuru wa kufikiri, dhamiri, dini, ibada, na uhuru wa kuzungumza kuhusu mambo hayo.” Pia aliandika kwamba yeyote anayemzuia mtoto kusoma “anatenda isivyo haki na anapaswa kuadhibiwa.” Aliwakumbusha maofisa wa shule kwamba “hakuna mwanafunzi anayepaswa kufukuzwa shuleni kwa sababu ya mawazo au kufikiri kwake, dhamiri, dini au ibada . . . Kwa hiyo, wasimamizi wa shule wanapaswa kukomesha mwenendo huo mbaya na kuwarudisha shuleni wanafunzi waliofukuzwa.”

Miongoni mwa wanafunzi waliokuwa wamefukuzwa ni Dada Jeanette Niyonkuru. Anaeleza hivi: “Baada ya kufukuzwa nilikaa nyumbani kwa mwaka mmoja. Ingawa nilipata shule ambayo hatimaye ilinikubali, ilinibidi nitembee kwa muda wa saa mbili kila siku ili kufika shuleni.” Wale ambao hawakuweza kusafiri kwenda shule za mbali walilazimika kuacha masomo yao.

Watoto watatu wa Ndugu na Dada Hakizimana walifukuzwa shuleni baada ya kukataa kushiriki katika mambo ya kidini waliyolazimishwa. Ndugu Hakizimana anasema: “Tulimwandikia mwalimu mkuu wa shule hiyo, lakini hakujibu. Hata tulipanga tukutane na msimamizi wa shule. Aliwasikiliza watoto wetu wakieleza msimamo wao wakitumia Biblia, lakini suala hilo halikusuluhishwa. Tulifurahi tuliposikia maagizo ya waziri. Baadaye, tulikutana na wakuu wa wilaya, kisha watoto wetu wakaruhusiwa kurudi shuleni.”

Tunathamini sana maagizo hayo yaliyotolewa na waziri wa elimu kwa sababu yanatetea haki za watoto wetu wa shule nchini Rwanda. Vijana hawa wamedumisha “dhamiri njema,” huku wakililetea jina la Yehova heshima.​—1 Petro 3:16.