Hamia kwenye habari

Ndugu Jovidon Bobojonov

NOVEMBA 18, 2020
TAJIKISTAN

Ndugu Jovidon Bobojonov Ameachiliwa Huru kwa Msamaha wa Rais wa Tajikistan

Ndugu Jovidon Bobojonov Ameachiliwa Huru kwa Msamaha wa Rais wa Tajikistan

“Yehova amenisaidia niendelee kuwa na imani yenye nguvu,” Ndugu Jovidon Bobojonov alisema maneno hayo baada ya kuachiliwa huru Novemba 1, 2020. Siku moja kabla, Rais wa Tajikistan alitoa msamaha kwa Jovidon, pamoja na wafungwa wengine 377. Tayari Jovidon alikuwa ametumikia kifungo cha miezi tisa ya hukumu ya miaka miwili gerezani kutokana na kukataa utumishi wa jeshi kwa sababu ya dhamiri.

Oktoba 4, 2019, wanajeshi walimteka Jovidon, aliyekuwa na umri wa miaka 19 wakati huo, kutoka nyumbani kwao na kumweka kizuizini katika ofisi ya kuandikisha utumishi wa jeshi. Katika kipindi cha miezi kadhaa iliyofuata, alihamishwa kutoka kambi moja baada ya nyingine za jeshi. Kwenye kila Mahabusu ya Muda (TDF) ya jeshi, Jovidon alihitaji kueleza kwa nini alikataa kutumikia jeshi. Jovidon anasema hivi: “Makamanda na wanajeshi kadhaa waliniuliza maswali yasiyopatana na akili, na wote walitaka niache dini yangu. Walitumia maswali ili kunikasirisha. Pindi nyingine waliniamsha usiku na kisha wakaniuliza maswali yaleyale tena na tena, wakidai kwamba niwaeleze sababu kwa nini ninakataa kujiunga na jeshi.”

“Hata hivyo, sala ilinisaidia sana. Nilipokuwa katika kambi ya jeshi, mchana na usiku nilisali huku nikitokwa na machozi, nikimwomba Yehova anisaidie niendelee kuvumilia, nisimwache, na nijibu inavyofaa hata ninapochokozwa.

“Yehova aliushika mkono wangu kwa nguvu . . . Nilishuka moyo sana nilipojihisi mpweke. Lakini Yehova kupitia uumbaji wake, alinichochea na kuniimarisha. Kila siku asubuhi nilipoamka, nilisikia sauti za ndege wakiimba. Usiku, nilitazama mwezi na nyota. Zawadi hizo kutoka kwa Yehova ziliniletea furaha na kunitia moyo.”

Jovidon alihukumiwa Aprili 2, 2020, na kuhamishwa kutoka katika Mahabusu ya Muda (TDF) na kupelekwa gerezani. Hakuruhusiwa kupokea barua yoyote. Hata hivyo, ndugu na dada walimpelekea chakula na kumwandikia andiko la kila siku katika mfuko waliotumia kubeba mahitaji hayo. “Jambo hilo lilinisaidia kutohisi mpweke, na nilijionea upendo wa rafiki zangu,” anasema Jovidon.

Jovidon anathamini sana kwamba aliweza kukumbuka maandiko ya Biblia kama vile Waroma 8:37-39 yaliyomtia moyo sana. Anasema hivi: “Nilipokuwa gerezani, maneno ya andiko hilo yalitimia kikweli. Hakuna jaribu lolote lililoweza kunitenga na upendo wa Yehova. Yehova aliimarisha imani yangu.”

Kielelezo cha Jovidon kimewatia moyo wazazi wake. Baba yake, Abdujamol anasema hivi: “Imani yetu iliimarishwa na sala na mfano mzuri wa mwana wetu aliyeendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova chini ya jaribu hilo. Ndugu na dada zetu wa kiroho ulimwenguni pote walitutegemeza sana. Tunathamini sana sala zao. Tunathamini sana kwamba Yehova ametupatia ndugu na dada wanaotupenda na kutujali.”

Katika siku hizi za mwisho, tunatarajia kupata “majaribu makali.” (1 Petro 4:12) Hivyo, Jovidon anamalizia kwa kusema hivi: “Kwa kuwa sasa niko huru, ninapanga kutumia uhuru wangu kuongeza ujuzi wangu na kujitayarisha zaidi kwa ajili ya majaribu yoyote ya wakati ujao. Kwa yeyote yule ambaye bado hajakabili majaribu makali, ni jambo la muhimu kwamba utumie uhuru ulio nao kikamili kwa kujifunza kumhusu Yehova kwa kusoma Neno lake na machapisho yetu.”