Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | WAZAZI

Jinsi ya Kutoa Mwongozo Kama Mzazi

Jinsi ya Kutoa Mwongozo Kama Mzazi

 Mambo unayopaswa kujua

 Katika tamaduni fulani leo, watoto huwa na uhusiano wa karibu na wazazi nao huzungumza na wazazi wao ili kupata mwongozo. Na katika tamaduni nyingine, watoto hutafuta mwongozo kwa vijana wenzao.

 Watoto wanapotafuta mwongozo kwa vijana wenzao, hupunguza mamlaka ya wazazi wao. Isitoshe, watoto hao wanapokuwa matineja, wazazi wao wanaweza kuhisi kwamba hawawezi kuwashauri kabisa. Hilo halishangazi! Watoto wanapotumia muda mwingi sana pamoja na watoto wenzao, ni kana kwamba wanajilea wenyewe badala ya kulelewa na wazazi wao.

 Kwa nini ni rahisi sana kwa watoto kuwa na uhusiano wa karibu sana na marafiki wao na kupoteza mawasiliano na wazazi wao? Fikiria hali zifuatazo.

  •   Shule. Watoto wanapotumia muda mwingi sana pamoja na watoto wengine wanakuwa na urafiki wa karibu sana hivi kwamba wanathamini zaidi kukubaliwa na marafiki wao kuliko na wazazi wao. Mtazamo huo huwa na nguvu zaidi watoto wanapokuwa matineja.

    Watoto wanapaswa kujali maoni ya wazazi wao zaidi ya maoni ya wanafunzi wenzao

  •   Kutumia muda mchache pamoja. Katika familia nyingi, watoto wanaporudi kutoka shuleni, hawapati mtu yeyote nyumbani, labda kwa sababu mzazi au wazazi wote wako kazini.

  •   Mitindo ya ujana. Wanapokaribia utineja, vijana huzama katika mitindo yao ya maisha ambayo ina sheria za kufuata kutia ndani jinsi ya kuvaa, kuzungumza na kufanya mambo. Mara nyingi maoni ya vijana kuhusu mitindo hiyo ni muhimu zaidi kwao kuliko maoni ya wazazi wao.

  •   Matangazo ya biashara. Biashara nyingi zimekusudiwa kuvutia hasa vijana. Bidhaa na burudani nyingi zinafanya mapendezi ya watoto yatofautiane na ya wazazi wao. Dkt. Robert Epstein anasema hivi, “Ikiwa mitindo ya ujana ingepotea, viwanda vikubwa vinavyotengeneza pesa nyingi vingekufa.” a

 Mambo unayoweza kufanya

  •   Siku zote hakikisha una uhusiano imara na mtoto wako.

     Biblia inasema hivi kwenye Kumbukumbu la Torati 6:6 na 7: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako, nawe lazima uyakazie kwa wanao na kuongea kuyahusu unapoketi nyumbani mwako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”

     Vijana wengine wanaweza kuwa marafiki, lakini hawapaswi kuchukua nafasi yako kama mzazi. Habari njema ni kwamba, wataalamu wanasema kuwa watoto na vijana wengi huheshimu wazazi wao na wanataka wawafurahishe. Ikiwa utadumisha uhusiano wa karibu na watoto wako, utakuwa na uvutano mkubwa juu yao.

     “Unapaswa kutumia muda na watoto, mkifanya mambo ya kila siku pamoja, kama vile kupika, kufanya usafi na hata kazi za shule. Fanyeni mambo yanayofurahisha pamoja—chezeni michezo, tazameni sinema au televisheni. Usifikiri kwamba unahitaji tu kutumia muda fulani pamoja nao—yaani saa chache-chache. Hata iwe umetumia muda vizuri pamoja nao, ni lazima utumie muda mwingi zaidi!”—Lorraine.

  •   Usitegemee urafiki wa vijana wengine tu.

     Biblia inasema hivi kwenye Methali 22:15: “Ujinga umefungwa katika moyo wa mtoto.” Maelezo ya chini.

     Baadhi ya wazazi huridhika wanapoona watoto wao wana marafiki wengi. Lakini uwe makini, ijapokuwa urafiki na vijana wengine unaweza kufanya ionekane ni kana kwamba mtoto anaishi vizuri na watu, vijana hao hawawezi kuwasaidia wawe na urafiki na watu wa aina mbalimbali. Nao hawawezi kuwapa mwongozo ambao kijana anahitaji na ambao mzazi mpendwa anaweza kuutoa vizuri zaidi.

     “Vijana wengine wanaweza kuwa na ujuzi kuhusu mambo fulani, lakini hawana ustadi wa maisha, uzoefu, na hekima ya kuwasaidia vijana wengine kufanya maamuzi mazuri. Vijana wanapowategemea wazazi, wao hukua na kukomaa kulingana umri wao.”—Nadia.

  •   Toa mwongozo wenye hekima.

     Biblia inasema hivi kwenye Methali 13:20: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima.”

     Hata wanapokuwa watu wazima, watoto wanaweza kunufaika sana wanapotumia muda pamoja nawe. Uwe mfano mzuri.

     “Mifano mizuri zaidi kwa watoto ni wazazi wao. Watoto wanapofundishwa kuwathamini na kuwaheshimu wazazi wao, watakuwa kama wao watakapokuwa watu wazima.”—Katherine.

a Kitabu Teen 2.0—Saving Our Children and Families From the Torment of Adolescence.