Hamia kwenye habari

Je, Kuna “Dhambi Saba Nzito”?

Je, Kuna “Dhambi Saba Nzito”?

Jibu la Biblia

 Biblia haitaji kihususa “dhambi saba nzito.” Hata hivyo, inafundisha kwamba kutenda dhambi nzito kutamzuia mtu asipate wokovu. Kwa mfano, Biblia inataja dhambi nzito kama uasherati, ibada ya sanamu, kuwasiliana na pepo, milipuko ya hasira, na ulevi, kuwa ni “matendo ya mwili.” Kisha inasema hivi: “Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”​—Wagalatia 5:19-21. a

Je, Biblia haiorodheshi ‘vitu saba ambavyo ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu’?

 Ndiyo, inafanya hivyo. Kulingana na Biblia Habari Njema, Methali 6:16 inasema hivi: “Kuna vitu anavyochukia Mwenyezi-Mungu; naam, vitu saba ambavyo ni chukizo kwake.” Hata hivyo, dhambi zinazoorodheshwa baada ya hapo katika Methali 6:17-19 si orodha kamili. Badala yake inafafanua vitengo vya msingi vinavyowakilisha aina zote za makosa, kutia ndani, mawazo, maneno, na matendo. b

Kuna tofauti gani kati ya “dhambi ambayo huleta kifo” na “dhambi ambayo haileti kifo”?

 Biblia inaonyesha wazi kwamba dhambi zote huongoza kwenye kifo. Hata hivyo, tunaweza kuokolewa kutokana na dhambi na kifo kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Waroma 5:12; 6:23) Hivyo, “dhambi ambayo huleta kifo” ni ile ambayo haiwezi kufunikwa na fidia ya Kristo. (1 Yohana 5:16) Mtu ambaye hufanya dhambi ya aina hii ameazimia kabisa kufanya dhambi hivi kwamba hawezi kubadili mtazamo au mwenendo wake. Pia Biblia huirejelea kuwa aina ya dhambi ambayo haiwezi kusamehewa.​—Mathayo 12:31; Luka 12:10.

a Orodha ya mambo 15 yanayofanyiza dhambi nzito zinazopatikana kwenye Wagalatia 5:19-21 haijakusudiwa kuwa orodha ya dhambi zote, kwa kuwa baada ya orodha hiyo Biblia inaongezea maneno “mambo ya namna hiyo.” Kwa hiyo, msomaji wa Biblia anatiwa moyo atumie utambuzi kufahamu mambo ambayo hayajaorodheshwa lakini ambayo ni kati ya “mambo ya namna hiyo.”

b Methali 6:16 inatumia msemo wa Kiebrania unaokazia namba ya pili kwa kuitofautisha na ya kwanza. Misemo ya aina hiyo inapatikana mara nyingi katika Maandiko.​—Ayubu 5:19; Methali 30:15, 18, 21.