Hamia kwenye habari

Je, Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?

Je, Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?

Jibu la Biblia

 Wengi wanaona msalaba kuwa alama ya Ukristo. Hata hivyo, Biblia haisemi lolote kuhusu mti ambao Yesu alitundikwa juu yake, kwa hiyo hakuna mtu anayejua kihususa jinsi ulivyokuwa. Pamoja na hayo, Biblia ina ushahidi unaoonyesha kwamba Yesu alitundikwa katika nguzo au mti ulionyooka.

 Kwa kawaida, Biblia hutumia neno la Kigiriki stau·rosʹ inaporejelea mti uliotumiwa kumtundika Yesu. (Mathayo 27:40; Yohana 19:17) Ijapokuwa tafsiri nyingi hutafsiri neno hilo kuwa “msalaba,” wasomi wengi wanakubaliana kwamba kimsingi linamaanisha “mti ulionyooka.” a Kulingana na kitabu cha Kiingereza kinachoitwa (A Critical Lexicon and Concordance to the English and Greek New Testament), neno stau·rosʹ “halimaanishi hata kidogo vipande viwili vya mbao vilivyounganishwa pamoja upande wowote ule.”

 Biblia hutumia pia neno la Kigiriki xyʼlon likiwa kisawe cha neno stau·rosʼ. (Matendo 5:​30; 1 Petro 2:​24) Neno hilo linamaanisha “ubao,” au “mti.”? b Hivyo, tafsiri ya The Companion Bible inafikia mkataa huu: ‘Hakuna jambo lolote katika lugha ya Kigiriki ya Agano Jipya linalodokeza vipande viwili vya mbao.’

Je, Mungu anakubali matumizi ya msalaba katika ibada?

Neno crux simplex katika lugha ya Kilatini linatumiwa kumaanisha mti mmoja uliotumiwa kutundika wahalifu

 Bila kujali Yesu alikufa juu ya nini, ukweli na mistari ifuatayo ya Biblia inaonyesha kwamba hatupaswi kutumia msalaba katika ibada.

  1.   Mungu anakataa ibada inayohusisha sanamu au mifano, kutia ndani msalaba. Mungu aliwaamuru Waisraeli kutotumia “umbo la mfano wowote” katika ibada. Wakristo pia wanaambiwa ‘waikimbie ibada ya sanamu.’​—Kumbukumbu la Torati 4:​15-​19; 1 Wakorintho 10:14.

  2.   Wakristo wa karne ya kwanza hawakutumia msalaba katika ibada. c Mafundisho na mfano wa mitume ni kielelezo ambacho Wakristo wote wanapaswa kufuata.​—2 Wathesalonike 2:​15.

  3.   Wapagani ndio walioanzisha matumizi ya msalaba katika ibada. d Mamia ya miaka baada ya kifo cha Yesu, makanisa yalipokuwa yameacha mafundisho yake, washiriki wapya wa makanisa “waliruhusiwa kwa kiasi kikubwa kuendelea kutumia mifano na sanamu zao za kipagani,” kutia ndani msalaba. (The Expanded Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words) Hata hivyo, Biblia hushutumu matumizi ya mifano ya kipagani ili kugeuza watu imani.​—2 Wakorintho 6:​17.

a Tazama New Bible Dictionary, Toleo la Tatu la D. R. W. Wood, ukurasa wa 245; Theological Dictionary of the New Testament, Buku la 7, ukurasa wa 572; The International Standard Bible Encyclopedia,Toleo Lililosahihishwa, Buku la 1, ukurasa wa 825; na The Imperial Bible-Dictionary, Buku la 2, ukurasa wa 84.

b Tazama The Expanded Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words, ukurasa wa 1165; A Greek-English Lexicon, kilichoandikwa na Liddell na Scott, Toleo la Tisa, ukurasa wa 1191-​1192; na Theological Dictionary of the New Testament, Buku la 5, ukurasa wa 37.

c Tazama Encyclopædia Britannica, 2003, chini ya kichwa “Cross”; The Cross​—Its History and Symbolism, ukurasa wa 40; na The Companion Bible, Oxford University Press, nyongeza ya 162, ukurasa wa 186.

d Tazama The Encyclopedia of Religion, Buku la 4, ukurasa wa 165; The Encyclopedia Americana, Buku la 8, ukurasa wa 246; na Symbols Around Us, ukurasa wa 205-​207.