Hamia kwenye habari

Ninataka Kufa​—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Ikiwa Ninawazia Kujiua?

Ninataka Kufa​—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Ikiwa Ninawazia Kujiua?

Jibu la Biblia

 Ndiyo! Biblia inatoka kwa “Mungu, ambaye huwafariji wale waliovunjika moyo.” (2 Wakorintho 7:6) Ingawa Biblia si kitabu kuhusu tiba ya akili, imewasaidia wengi kukabiliana na hisia za kujiua. Ushauri wake unaofaa unaweza kukusaidia pia.

 Biblia inatoa ushauri gani unaofaa?

  • Waeleze wengine jinsi unavyohisi.

     Biblia inasema hivi: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”—Methali 17:17.

     Maana: Tunahitaji msaada kutoka kwa wengine tunapokuwa na mawazo yenye kutuhangaisha.

     Ukifungia hisia zako, unabeba mzigo ambao unaweza kukushinda kubeba. Lakini ukiwaeleza wengine hisia zako, unaweza kuanza kujihisi vizuri zaidi na kuanza kuona hali yako kwa njia nzuri zaidi.

     Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mtu leo, labda mtu wa familia au rafiki unayemwamini. a Pia unaweza kujieleza kwa kuandika hisia zako.

  • Mwone daktari.

     Biblia inasema hivi: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.”—Mathayo 9:12.

     Maana: Tunapaswa kumwona daktari tunapokuwa wagonjwa.

     Mawazo ya kujiua yanaweza kuwa dalili ya ugonjwa wa akili au wa kihisia. Kama tu magonjwa mengine, hupaswi kuaibika. Ugonjwa wa akili au wa kihisia unaweza kutibiwa.

     Jaribu kufanya hivi: Tafuta msaada wa daktari anayefaa haraka iwezekanavyo.

  • Kumbuka kwamba Mungu anajali.

     Biblia inasema hivi: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado Mungu hamsahau hata mmoja. . . . Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”—Luka 12:6, 7.

     Maana: Wewe ni mwenye thamani kwa Mungu.

     Huenda ukahisi kwamba hakuna anayekujali, lakini Mungu anaona mambo unayokabili. Anakujali—hata ikiwa wewe unahisi kwamba hutaki kuendelea kuishi. “Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaukataa,” inasema Zaburi 51:17. Mungu anataka uendelee kuishi kwa sababu anakupenda.

     Jaribu kufanya hivi: Chunguza uthibitisho kutoka katika Biblia kwamba Mungu anakujali. Kwa mfano, ona sura ya 24 ya kitabu cha kujifunzia Biblia Mkaribie Yehova.

  • Sali kwa Mungu.

     Biblia inasema hivi: ‘Mtupieni Mungu mahangaiko yenu yote, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

     Maana: Mungu anakukaribisha umweleze waziwazi na kwa unyoofu kuhusu chochote kinachokuhangaisha.

     Mungu anaweza kukupa amani ya akili na nguvu za kuendelea kuvumilia hali yako. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Kwa njia hiyo, yeye huwategemeza wale wanaomwomba msaada.—Zaburi 55:22.

     Jaribu kufanya hivi: Sali kwa Mungu leo. Tumia jina lake, Yehova, na umweleze hisia zako. (Zaburi 83:18) Mwombe akusaidie uvumilie hali unazokabili.

  • Tafakari tumaini la wakati ujao linalotajwa katika Biblia.

     Biblia inasema hivi: “Tuna tumaini hilo kama nanga ya uhai wetu, likiwa hakika na imara.”—Waebrania 6:19, maelezo ya chini.

     Maana: Hisia zako huenda zikapanda na kushuka kama vile meli inayokabili dhoruba, lakini tumaini linalotajwa katika Biblia linaweza kukusaidia uwe na usawaziko.

     Tumaini hilo si ndoto tu bali linategemea ahadi ya Mungu ya kuondoa chanzo cha maumivu yetu.—Ufunuo 21:4.

     Jaribu kufanya hivi: Jifunze mengi zaidi kuhusu tumaini la Biblia kwa kusoma somo la 5 la broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!

  • Fanya kitu unachofurahia.

     Biblia inasema hivi: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”—Methali 17:22.

     Maana: Tunapofanya mambo yanayotuletea shangwe, tunaweza kuboresha afya yetu ya akili na ya kihisia.

     Jaribu kufanya hivi: Fanya kitu ambacho kwa kawaida unafurahia. Kwa mfano, sikiliza muziki unaokuburudisha, soma jambo lenye kutia moyo, au fanya utendaji unaopendezwa nao. Pia utaongeza furaha yako ukiwasaidia wengine, hata kwa njia ndogo.—Matendo 20:35.

  • Tunza afya yako.

     Biblia inasema hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.”—1 Timotheo 4:8.

     Maana: Tunapata manufaa tunapofanya mazoezi, kulala vya kutosha, na kula chakula chenye lishe.

     Jaribu kufanya hivi: Jaribu kutembea haraka, hata ikiwa ni kwa dakika 15 tu.

  • Kumbuka kwamba hisia na mambo mengine maishani hubadilika.

     Biblia inasema hivi: “Hamjui jinsi maisha yenu yatakavyokuwa kesho.”—Yakobo 4:14.

     Maana: Tatizo lenye kusumbua—ambalo huenda ukafikiri halitaisha—linaweza kuwa la muda.

     Hata ikiwa hali yako inaonekana kuwa mbaya sana leo, inaweza kubadilika kesho. Kwa hiyo, tafuta njia za kukabiliana nayo. (2 Wakorintho 4:8) Hali yako yenye kuhuzunisha inaweza kubadilika kadiri muda unavyopita, lakini huwezi kubadili chochote unapojiua.

     Jaribu kufanya hivi: Soma masimulizi ya Biblia kuhusu watu waliovunjika moyo sana hivi kwamba walitaka kufa, uone jinsi hatimaye maisha yao yalivyobadilika na kuwa mazuri—hata katika njia ambazo hawakuwazia. Fikiria mifano kadhaa.

 Je, Biblia inatuambia kuhusu watu waliotaka kufa?

 Ndiyo. Biblia inatueleza kuhusu watu fulani ambao walisema, “Ninataka kufa.” Mungu hakuwashutumu, badala yake aliwapa msaada. Anaweza kukusaidia wewe pia.

Eliya

  •  Alikuwa nani? Eliya alikuwa nabii mwenye ujasiri. Lakini yeye pia alivunjika moyo. “Eliya alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu,” inasema Yakobo 5:17.

  •  Kwa nini alitaka kufa? Pindi moja, Eliya alijihisi akiwa peke yake, akiwa na woga, na kwamba hafai. Kwa hiyo, akamsihi Mungu hivi: “Yehova, niue.”—1 Wafalme 19:4.

  •  Ni nini kilichomsaidia? Eliya alimweleza Mungu hisia zake. Mungu alimtiaje moyo? Mungu alionyesha kwamba anamjali na akamwonyesha Yeye ana nguvu kadiri gani. Pia alimhakikishia Eliya kwamba bado ana thamani na akampa msaidizi anayejali na mwenye uwezo.

  •  Soma kumhusu Eliya: 1 Wafalme 19:2-18.

Ayubu

  •  Alikuwa nani? Ayubu alikuwa mwanamume tajiri mwenye familia na ambaye alimwabudu Mungu wa kweli.

  •  Kwa nini alitaka kufa? Maisha ya Ayubu yalibadilika upesi na kuwa mabaya. Alipoteza mali zake zote. Watoto wake wote walikufa katika dhoruba. Alishikwa na ugonjwa mbaya sana. Na alishutumiwa vibaya na kwa uwongo kwamba alijisababishia matatizo yaliyompata. Ayubu alisema hivi: “Ninachukia maisha yangu; sitaki kuendelea kuishi.”—Ayubu 7:16.

  •  Ni nini kilichomsaidia? Ayubu alisali kwa Mungu na akazungumza na wengine. (Ayubu 10:1-3) Alitiwa moyo na rafiki mwenye hisia-mwenzi, Elihu, ambaye alimsaidia kuona hali yake kwa njia inayofaa. Zaidi ya yote, Ayubu alikubali mashauri na msaada kutoka kwa Mungu.

  •  Soma kumhusu Ayubu: Ayubu 1:1-3, 13-​22; 2:7; 3:1-13; 36:1-7; 38:1-3; 42:1, 2, 10-13.

Musa

  •  Alikuwa nani? Musa alikuwa kiongozi wa Israeli la kale na nabii mwaminifu.

  •  Kwa nini alitaka kufa? Musa alikuwa na kazi nyingi, alichambuliwa kila wakati, na alihisi kuwa amechoka. Kwa hiyo, alimwambia Mungu hivi: “Tafadhali niue sasa hivi.”—Hesabu 11:11, 15.

  •  Ni nini kilichomsaidia? Musa alimwambia Mungu jinsi alivyohisi. Mungu alimsaidia Musa kupunguza kazi yake ili apunguze mkazo.

  •  Soma kumhusu Musa: Hesabu 11:4-6, 10-17.

a Ikiwa hisia zako za kujiua ni nyingi na watu unaowaamini hawako karibu, piga simu kwenye shirika linaloshughulika na kutoa msaada wa dharura katika eneo lenu.