Hamia kwenye habari

Je, Pesa Ndio Chanzo cha Uovu Wote?

Je, Pesa Ndio Chanzo cha Uovu Wote?

Jibu la Biblia

 Hapana. Biblia haisemi kwamba pesa ndio chanzo cha mambo yote mabaya. Watu wengi hutumia usemi “pesa ndio chanzo cha uovu wote,” lakini usemi huo si nukuu kamili la Biblia na unaopotosha. Biblia inasema “kupenda sana fedha ni chanzo cha uovu wote.” a1 Timotheo 6:10, Biblia Habari Njema.

 Biblia inasema nini kuhusu pesa?

 Biblia inaonyesha kwamba pesa zinapotumiwa kwa hekima, zinaweza kuwa na faida, hata zinaweza kuwa “ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Isitoshe, Biblia inawapongeza wale wanaowaonyesha wengine ukarimu, huenda kwa kuwapa pesa.—Methali 11:25.

 Wakati huohuo, Biblia inaonya dhidi ya kutanguliza pesa maishani. Inasema hivi: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.” (Waebrania 13:5) Jambo kuu ni kuwa na usawaziko kuhusu pesa na kutofuatilia utajiri. Badala yake, lengo letu linapaswa kuwa kuridhika na vitu tunavyohitaji hasa, kama vile chakula, mavazi, na makao.—1 Timotheo 6:8.

 Kwa nini Biblia inatuonya tusipende pesa?

 Watu wenye pupa hawatapata uzima wa milele. (Waefeso 5:5) Sababu moja ni kwamba pupa ni aina fulani ya ibada ya sanamu, au ya uwongo. (Wakolosai 3:5) Sababu nyingine ni kwamba watu wenye pupa wanapojitahidi kupata wanachotamani, mara nyingi wanafanya mambo mabaya. Methali 28:20 inasema kwamba wale ‘wanaoharakisha kupata utajiri hawatabaki bila hatia.’ Huenda hata wakashawishika kujihusisha katika uhalifu, kama vile, kuwatisha wengine, kujihusisha katika unyang’anyi, ulaghai, utekaji-nyara, au uuaji.

 Hata ikiwa kupenda pesa hakutaongoza kwenye tabia mbaya, kunaweza kuwa na madhara mengine. Biblia inasema kwamba “wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka kwenye majaribu, na mtego, na tamaa nyingi za kijinga zenye kudhuru.”—1 Timotheo 6:9.

 Tunaweza kunufaikaje kutokana na ushauri wa Biblia kuhusu pesa?

 Ikiwa hatutalegeza viwango vya kimaadili na vya kiroho ili tu kupata pesa, tutaendelea kujiheshimu na tutapata kibali na utegemezo wa Mungu. Mungu anawaahidi hivi wale ambao wanajitahidi kumpendeza: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” (Waebrania 13:5, 6) Pia anatuhakikishia kwamba “mtu mwaminifu atapata baraka nyingi.”—Methali 28:20.

a Mstari huo umetafsiriwa pia kuwa: “Kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina.”