Hamia kwenye habari

Je, Unabii wa Kimasihi Unathibitisha Kwamba Yesu Alikuwa Ndiye Masihi?

Je, Unabii wa Kimasihi Unathibitisha Kwamba Yesu Alikuwa Ndiye Masihi?

Jibu la Biblia

 Ndiyo. Alipokuwa dunia, Yesu alitimiza unabii mwingi kuhusu “Masihi aliye Kiongozi,” yule ambaye angekuwa “mwokozi wa ulimwengu.” (Danieli 9:25; 1 Yohana 4:14) Na hata baada ya kifo chake, Yesu aliendelea kutimiza unabii wa Kimasihi.​—Zaburi 110:1; Matendo 2:34-36.

 Ni nini maana ya neno “Masihi”?

 Neno la Kiebrania Ma·shiʹach (Masihi) na neno la Kigiriki linalofanana nalo Khri·stos (Kristo) yote yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Hivyo, “Yesu Kristo” linamaanisha “Yesu Mtiwa-Mafuta,” au “Yesu Masihi.”

 Katika nyakati za Biblia, mara nyingi mtu alitiwa mafuta kwa kumiminiwa mafuta kichwani alipowekwa rasmi kuchukua jukumu la pekee lenye mamlaka. (Mambo ya Walawi 8:12; 1 Samweli 16:13) Yesu aliwekwa rasmi na Mungu kuwa Masihi​—cheo kilicho na mamlaka kubwa. (Matendo 2:​36) Hata hivyo, badala ya kumtia Yesu mafuta kwa kutumia mafuta halisi, Mungu alimweka rasmi kwa roho takatifu.​—Mathayo 3:16.

 Je, mtu zaidi ya mmoja angeweza kutimiza unabii wa Kimasihi?

 Hapana. Kama vile alama za vidole zinavyomtambulisha mtu mmoja tu, ndivyo utimizo wa unabii wa Biblia unavyoelekeza kwa Masihi mmoja tu, au Kristo. Hata hivyo, Biblia inaonya kwamba “Kristo wengi wa uwongo na manabii wa uwongo watatokea na kufanya ishara kubwa na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.”​—Mathayo 24:24.

 Je, Masihi angeweza kutokea wakati ujao?

 Hapana. Biblia ilitabiri kwamba Masihi angekuwa mzao wa Mfalme Daudi wa Israeli. (Zaburi 89:​3, 4) Hata hivyo, rekodi za ukoo wa Kiyahudi kurudi nyuma hadi wakati wa Daudi zimepotea, huenda ziliharibiwa Waroma waliposhinda Yerusalemu katika mwaka wa 70 W.K. a Tangu wakati huo, haijawezekana kwa yeyote kuthibitisha kwamba yeye ni mzao wa familia ya kifalme ya Daudi. Tofauti na hilo, rekodi hizo za ukoo zilikuwepo wakati wa Yesu, na hata maadui wake hawakufaulu kupinga dai lake la kuwa mzao wa Daudi.​—Mathayo 22:41-​46.

 Ni unabii mwingi kadiri gani wa Kimasihi unaopatikana katika Biblia?

 Haiwezekani kutoa idadi hususa inayoonyesha ni unabii mwingi kadiri gani wa Kimasihi ambao umewahi kutolewa. Kwa mfano, mbinu ya hesabu unabii inaweza kutofautiana hata kuhusu masimulizi ambayo kwa wazi yanazungumza kumhusu Masihi. Simulizi la Isaya 53:2-7 linataja mambo kadhaa ya kinabii kumhusu Masihi. Huenda watu fulani wakasema unabii huo unapaswa kuhesabiwa kama unabii mmoja, ilhali wengine wakaona kila jambo kuwa unabii tofauti.

 Baadhi ya unabii wa Kimasihi ambao Yesu alitimiza

Unabii

Unapopatikana

Utimizo

Mzao wa Abrahamu

Mwanzo 22:17, 18

Mathayo 1:1

Mzao wa Isaka mwana wa Abrahamu

Mwanzo 17:19

Mathayo 1:2

Alizaliwa katika kabila la Yuda la Israeli

Mwanzo 49:10

Mathayo 1:​1, 3

Angetoka katika ukoo wa kifalme wa Mfalme Daudi

Isaya 9:7

Mathayo 1:1

Angezaliwa na bikira

Isaya 7:​14

Mathayo 1:​18, 22, 23

Angezaliwa Bethlehemu

Mika 5:2

Mathayo 2:​1, 5, 6

Angeitwa kwa jina Imanueli b

Isaya 7:​14

Mathayo 1:​21-​23

Angelelewa katika familia maskini

Isaya 53:2

Luka 2:7

Watoto wachanga wangeuawa baada ya kuzaliwa kwake

Yeremia 31:15

Mathayo 2:​16-​18

Angeitwa kutoka Misri

Hosea 11:1

Mathayo 2:​13-​15

Angeitwa Mnazareti c

Isaya 11:1

Mathayo 2:​23

Angetanguliwa na mjumbe

Malaki 3:1

Mathayo 11:​7-​10

Angetiwa mafuta kuwa Masihi mwaka wa 29 W.K. d

Danieli 9:​25

Mathayo 3:​13-​17

Alitambulishwa na Mungu kuwa Mwana wake

Zaburi 2:7

Matendo 13:33, 34

Angekuwa na bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu

Zaburi 69:9

Yohana 2:​13-​17

Angetangaza habari njema

Isaya 61:1

Luka 4:​16-​21

Huduma ya hadharani kule Galilaya nuru kubwa

Isaya 9:​1, 2

Mathayo 4:​13-​16

Angefanya miujiza kama Musa

Kumbukumbu la Torati 18:15

Matendo 2:​22

Kama Musa, angesema alichoagizwa na Mungu

Kumbukumbu la Torati 18:18, 19

Yohana 12:49

Angeponya magonjwa mengi

Isaya 53:4

Mathayo 8:​16, 17

Asingejielekezea fikira

Isaya 42:2

Mathayo 12:17, 19

Angewahurumia wanaoteseka

Isaya 42:3

Mathayo 12:​9-​20; Marko 6:​34

Angefunua haki ya Mungu

Isaya 42:​1, 4

Mathayo 12:17-​20

Mshauri wa Ajabu

Isaya 9:​6, 7

Yohana 6:​68

Angetangaza jina la Yehova

Zaburi 22:22

Yohana 17:6

Angesema kwa kutumia mifano

Zaburi 78:2

Mathayo 13:34, 35

Kiongozi

Danieli 9:​25

Mathayo 23:10

Watu wengi hawangemwamini

Isaya 53:1

Yohana 12:37, 38

Angekuwa jiwe la kukwaza

Isaya 8:​14, 15

Mathayo 21:42-​44

Angekataliwa na wanadamu

Zaburi 118:22, 23

Matendo 4:​10, 11

Angechukiwa bila sababu

Zaburi 69:4

Yohana 15:24, 25

Angeingia Yerusalemu kwa ushindi akiwa amepanda punda

Zekaria 9:9

Mathayo 21:​4-9

Angesifiwa na watoto

Zaburi 8:2

Mathayo 21:15, 16

Angekuja katika jina la Yehova

Zaburi 118:26

Yohana 12:12, 13

Angesalitiwa na rafiki anayeaminika

Zaburi 41:9

Yohana 13:18

Angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha e

Zekaria 11:12, 13

Mathayo 26:14-​16; 27:​3-​10

Marafiki wangemwacha

Zekaria 13:7

Mathayo 26:31, 56

Mashahidi wangetoa ushahidi wa uwongo dhidi yake

Zaburi 35:11

Mathayo 26:59-​61

Angekaa kimya mbele ya washtaki wake

Isaya 53:7

Mathayo 27:12-​14

Angetemewa mate

Isaya 50:6

Mathayo 26:67; 27:27, 30

Angepigwa kichwani

Mika 5:1

Marko 15:19

Angepigwa mijeledi

Isaya 50:6

Yohana 19:1

Hakuwazuia waliokuwa wakimpiga

Isaya 50:6

Yohana 18:22, 23

Viongozi wa kidini walipanga njama dhidi yake

Zaburi 2:2

Luka 23:10-​12

Alitundikwa kwenye mti wa mateso kwa kupigiliwa misumari kwenye mikono na miguu

Zaburi 22:16

Mathayo 27:35; Yohana 20:25

Watu walipigia kura (kamari) mavazi yake

Zaburi 22:18

Yohana 19:23, 24

Angehesabiwa na watenda dhambi

Isaya 53:12

Mathayo 27:38

Angetukanwa

Zaburi 22:​7, 8

Mathayo 27:39-​43

Angeteseka kwa ajili ya watenda-dhambi

Isaya 53:​5, 6

1 Petro 2:​23-​25

Angeonekana kuwa amekataliwa na Mungu

Zaburi 22:1

Marko 15:34

Alipewa siki na nyongo anywe

Zaburi 69:21

Mathayo 27:34

Angehisi kiu kabla tu ya kufa

Zaburi 22:15

Yohana 19:28, 29

Angemkabidhi Mungu roho yake

Zaburi 31:5

Luka 23:46

Alidhabihu uhai wake

Isaya 53:12

Marko 15:37

Aliandaa fidia ili kuondoa dhambi

Isaya 53:12

Mathayo 20:28

Mifupa haikuvunjwa

Zaburi 34:20

Yohana 19:31-​33, 36

Angechomwa

Zekaria 12:10

Yohana 19:33-​35, 37

Angezikwa pamoja na matajiri

Isaya 53:9

Mathayo 27:57-​60

Angefufuliwa kutoka kwa wafu

Zaburi 16:10

Matendo 2:​29-​31

Mahali pa msaliti pangechukuliwa na mwingine

Zaburi 109:8

Matendo 1:​15-​20

Angeketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu

Zaburi 110:1

Matendo 2:​34-​36

a McClintock and Strong’s Cyclopedia inasema hivi: “Hakuna shaka kwamba orodha ya makabila na familia za Wayahudi ziliangamia wakati wa uharibifu wa Yerusalemu, si kabla ya hapo.”

b Jina la Kiebrania Imanueli, linalomaanisha “Mungu Yuko Pamoja Nasi, ” linafafanua fungu la Masihi kwa njia nzuri. Kuwapo kwake duniani na kazi zake zinathibitisha kwamba Mungu alikuwa pamoja na waabudu Wake.​—Luka 2:​27-​32; 7:​12-​16.

c Inaonekana kwamba neno “Mnazareti” linatokana na neno la Kiebrania neʹtser, linalomaanisha “chipukizi.”

d Kwa habari zaidi kuhusu mfuatano wa matukio ya Biblia kuhusu mwaka wa 29 W.K. kuwa mwaka ambao Masihi angetokea, ona makala yenye kichwa “Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihi.”

e Unabii huu unapatikana katika kitabu cha Zekaria, hata hivyo, mwandikaji wa Biblia Mathayo alisema kwamba ‘ulisemwa kupitia nabii Yeremia.’ (Mathayo 27:9) Inaonekana kwamba nyakati nyingine kitabu cha Yeremia kiliwekwa kwanza katika sehemu ya Maandiko iliyoitwa “Manabii.” (Luka 24:44) Inaonekana kwamba Mathayo alitaja “Yeremia” kurejelea mkusanyo huo wote wa vitabu, uliotia ndani kitabu cha Zekaria.