Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Wafilipi 4:8​—“Mambo Yoyote Yaliyo ya Kweli, . . . Endeleeni Kuyafikiria Mambo Hayo”

Wafilipi 4:8​—“Mambo Yoyote Yaliyo ya Kweli, . . . Endeleeni Kuyafikiria Mambo Hayo”

 “Mwishowe, akina ndugu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yanayopendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, mambo yoyote ya wema wa adili, na mambo yoyote yanayostahili sifa, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”​—Wafilipi 4:8, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hatimaye, ndugu zangu jazeni fikra zenu kwa mambo mema na yanayostahili kusifiwa; mambo ya kweli, bora, haki, safi, ya kupendeza na ya heshima.”​—Wafilipi 4:8, Habari Njema Kwa Watu Wote.

Maana ya Wafilipi 4:8

 Mungu anapendezwa na mawazo yetu kwa sababu kufikiri kwetu kunaathiri jinsi tunavyotenda. (Zaburi 19:14; Marko 7:20-23) Kwa sababu hiyo, watu wanaotaka kumpendeza Mungu wanakataa kufikiria mambo ambayo yanamchukiza na badala yake wanafikiria kuhusu mambo yanayokubalika machoni pake.

 Mstari huu unataja mambo nane mazuri ambayo Wakristo wanapaswa ‘kuendelea kuyafikiria,’ yaani, kuyazingatia kwa ukawaida.

  •   Mambo “ya kweli.” Maneno hayo yanafafanua mambo mema na yenye kutegemeka, kama vile habari zinazopatikana katika Neno la Mungu, Biblia.​—1 Timotheo 6:20.

  •   Mambo “ya hangaiko zito.” Maneno hayo yanarejezea mambo yaliyo muhimu kikweli. Si mambo madogo-madogo, mambo ya mzaha, na mambo yasiyo na maana au uzito. Badala yake ni mambo yanayomchochea Mkristo kuimarisha azimio lake la kufanya yaliyo sawa.​—Tito 2:6-8.

  •   Mambo “ya uadilifu.” Maneno hayo yanarejelea mipango na matendo ambayo yanapatana na viwango vya Mungu vya yaliyo sawa na ambayo hayategemei viwango vya wanadamu.​—Methali 3:5, 6; 14:12.

  •   Mambo “yaliyo safi kiadili.” Maneno hayo yanatoa wazo la kuwa na nia na mawazo yaliyo safi na matakatifu, si katika mambo yanayohusu ngono peke yake, bali katika mambo yote.​—2 Wakorintho 11:3.

  •   Mambo “yanayopendeka.” Maneno hayo yanarejelea mambo mazuri yanayochochea hisia za upendo badala ya chuki, uchungu, au mizozo.​—1 Petro 4:8.

  •   Mambo “yanayosemwa vema.” Maneno hayo yanarejelea mambo yanayomfanya mtu awe na sifa nzuri ambazo zinakubaliwa na watu wanaomheshimu Mungu.​—Methali 22:1.

  •   Mambo “ya wema wa adili.” Maneno hayo yanafafanua mambo ambayo ni ya maadili mema kulingana viwango vya Mungu. Ni mazuri kabisa.​—2 Petro 1:5, 9.

  •   Mambo “yanayostahili sifa.” Maneno hayo yanarejelea mambo mema yenye sifa machoni pa Mungu. Yanatia ndani matendo ya Yehova yanayostahili sifa, ambayo wanadamu wanapaswa kufikiria.​—Zaburi 78:4.

Muktadha wa Wafilipi 4:8

 Mtume Paulo alikuwa chini ya kifungo cha nyumbani huko Roma, alipoandika barua yake kwa Wafilipi. Hata hivyo, wasomi wa Biblia wanafafanua barua yake kuwa “barua ya shangwe” kwa sababu ina uchangamfu na pia alitumia maneno mengi yenye shauku na yenye upendo mwororo.​—Wafilipi 1:3, 4, 7, 8, 18; 3:1; 4:1, 4, 10.

 Paulo aliwapenda ndugu na dada zake wa kiroho waliokuwa Filipi, na alitaka wao pia wapate shangwe na amani aliyokuwa nayo. (Wafilipi 2:17, 18) Katika sehemu ya mwisho ya barua yake, aliwatia moyo wawe na shangwe, wawe na usawaziko, wamtegemee Mungu kwa kusali daima, na wakaze fikira zao kwenye mambo ambayo yangewasaidia kuwa na amani moyoni na pia amani pamoja na Mungu.​—Wafilipi 4:4-9.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Wafilipi.