Barua ya Kwanza kwa Wathesalonike 2:1-20

  • Huduma ya Paulo huko Thesalonike (1-12)

  • Wathesalonike walilikubali neno la Mungu (13-16)

  • Paulo atamani kuwaona Wathesalonike (17-20)

2  Kwa kweli, ninyi wenyewe akina ndugu mnajua kwamba ziara yetu kwenu ilikuwa na mafanikio.+  Kwa maana ingawa kwanza tulikuwa tumeteseka na kudharauliwa huko Filipi,+ kama mnavyojua, tulijipa ujasiri* kupitia Mungu wetu ili tuwatangazie ninyi habari njema ya Mungu+ licha ya upinzani.*  Kwa maana mambo tunayowahimiza hayatokani na kosa, uchafu, wala udanganyifu,  lakini kwa kuwa tumekubaliwa na Mungu kukabidhiwa habari njema, hatusemi ili tuwapendeze wanadamu, bali tumpendeze Mungu ambaye huchunguza mioyo yetu.+  Kwa kweli, mnajua hatukutumia kamwe maneno ya kuwasifusifu au kuwa wanafiki tukiwa na makusudi yenye pupa;+ Mungu ni shahidi!  Wala hatujatafuta utukufu kutoka kwa wanadamu, iwe ni kutoka kwenu au kwa watu wengine, ingawa tukiwa mitume wa Kristo tungeweza kuwa mzigo wenye gharama kwenu.+  Badala yake, tuliwatendea kwa upole, kama vile mama anayenyonyesha anavyowatunza* watoto wake kwa wororo.  Basi, kwa maana tulikuwa na upendo mwororo kwenu, tulijitahidi* kuwapa habari njema ya Mungu na hata uhai wetu* wenyewe,+ kwa sababu tuliwapenda sana.+  Hakika akina ndugu, mnakumbuka kazi yetu ngumu na yenye kutaabisha. Tulifanya kazi usiku na mchana, ili tusimpe yeyote kati yenu mzigo wenye gharama,+ tulipowahubiria habari njema ya Mungu. 10  Ninyi ni mashahidi, na Mungu vilevile, wa jinsi tulivyokuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika kwenu. 11  Mnajua jinsi tulivyoendelea kumhimiza, kumfariji, na kumshauri kila mmoja wenu,+ kama baba+ anavyowatendea watoto wake, 12  ili mwendelee kutembea kwa kumstahili Mungu+ anayewaita kwenye Ufalme+ na utukufu wake.+ 13  Kwa kweli, hii ndiyo sababu tunamshukuru Mungu bila kuacha,+ kwa kuwa mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali si kama neno la wanadamu, bali kama lilivyo kwa kweli, neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini. 14  Kwa maana, akina ndugu mliiga makutaniko ya Mungu yaliyo katika muungano na Kristo Yesu huko Yudea, kwa sababu mliteswa na wananchi wenzenu,+ kama vile wao pia wanavyoteswa na Wayahudi, 15  ambao hata walimuua Bwana Yesu+ na manabii na wakatutesa.+ Zaidi ya hayo, hawafanyi mambo yanayompendeza Mungu, na wanapinga mambo yanayowafaa wanadamu wote, 16  wakijaribu kutuzuia kuzungumza na watu wa mataifa ili waokolewe.+ Kwa hiyo, sikuzote wanajaza kipimo cha dhambi zao. Lakini hatimaye hasira yake imekuja juu yao.+ 17  Hata hivyo, akina ndugu, tulipotenganishwa nanyi* kwa muda mfupi (katika mwili, bali si moyoni), kwa kuwa tulitamani sana, tulijitahidi kabisa kuwaona tena uso kwa uso.* 18  Kwa sababu hiyo, tulitaka kuja kwenu, ndiyo, mimi Paulo, nilijaribu si mara moja tu bali mara mbili; lakini Shetani aliifunga njia yetu. 19  Ni nini tumaini letu au shangwe au taji la furaha mbele ya Bwana wetu Yesu wakati wa kuwapo kwake? Je, kwa kweli si ninyi?+ 20  Kwa kweli ninyi ndio utukufu na shangwe yetu.

Maelezo ya Chini

Au “uhodari.”
Au labda, “licha ya kupambana sana.”
Au “anavyowalea kwa upendo.”
Tnn., “tulipendezwa vema.”
Au “nafsi zetu.”
Au “tulipoachwa mayatima.”
Tnn., “kuona nyuso zenu.”