Danieli 2:1-49

  • Mfalme Nebukadneza aota ndoto ya kufadhaisha (1-4)

  • Wenye hekima washindwa kueleza maana ya ndoto (5-13)

  • Danieli amwomba Mungu msaada (14-18)

  • Mungu asifiwa kwa kufunua siri (19-23)

  • Danieli amwambia mfalme ndoto yake (24-35)

  • Maana ya ndoto (36-45)

    • Jiwe la Ufalme laivunja sanamu (44, 45)

  • Danieli aheshimiwa na mfalme (46-49)

2  Katika mwaka wa pili wa utawala wake, Nebukadneza aliota ndoto kadhaa, akahangaika* sana+ hivi kwamba akashindwa kulala.⁠  Basi mfalme akaagiza makuhani wachawi, watu wanaofanya mazingaombwe, walozi, na Wakaldayo* waitwe ili wamwambie mfalme ndoto zake. Kwa hiyo wakaja na kusimama mbele ya mfalme.+  Kisha mfalme akawaambia: “Nimeota ndoto, nami ninahangaika* kwa sababu ninataka kujua nilichoota.”  Wakaldayo wakamjibu mfalme kwa lugha ya Kiaramu:*+ “Ee mfalme, na uishi milele. Tusimulie ndoto yako sisi watumishi wako, nasi tutakuambia maana yake.”  Mfalme akawajibu Wakaldayo: “Nimeamua hivi: Msiponiambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, mtakatwa vipandevipande, na nyumba zenu zitageuzwa kuwa vyoo vya umma.*  Lakini mkiniambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, nitawapa zawadi na tuzo na heshima kubwa.+ Basi niambieni ndoto hiyo na maana yake.”  Wakamjibu kwa mara ya pili: “Ee mfalme, tuambie ndoto yako, sisi watumishi wako, nasi tutakueleza maana yake.”  Mfalme akawajibu: “Najua vema kwamba mnajaribu kujipatia muda, kwa kuwa mnajua uamuzi wangu.  Msiponiambia ndoto yangu, adhabu yenu nyote ni moja tu. Lakini mmekubaliana kunidanganya na kunihadaa, mkitumaini kwamba hali itabadilika. Basi niambieni ndoto hiyo, nami nitajua kwamba mnaweza kueleza maana yake.” 10  Wakaldayo wakamjibu mfalme: “Hakuna mtu yeyote duniani* anayeweza kufanya jambo ambalo wewe mfalme unaagiza, kwa sababu hakuna mfalme yeyote mkuu wala gavana aliyewahi kumwomba kuhani yeyote mchawi, au mtu yeyote anayefanya mazingaombwe, au Mkaldayo afanye jambo kama hili. 11  Jambo ambalo wewe mfalme unaomba ni gumu, na hakuna yeyote anayeweza kukwambia jambo hilo isipokuwa miungu, ambao hawaishi miongoni mwa wanadamu.”* 12  Ndipo mfalme akashikwa na ghadhabu kali, akaagiza wanaume wote wenye hekima wa Babiloni waangamizwe.+ 13  Agizo hilo lilipotolewa na wakati ulipokaribia wa kuwaua wanaume hao wenye hekima, walimtafuta pia Danieli na wenzake ili wawaue. 14  Wakati huo, kwa busara na tahadhari Danieli alizungumza na Arioko mkuu wa walinzi wa mfalme, alipokuwa akienda kuwaua wanaume wenye hekima wa Babiloni. 15  Akamuuliza Arioko ofisa wa mfalme: “Kwa nini mfalme ametoa agizo kali hivyo?” Ndipo Arioko akamweleza Danieli jambo hilo.+ 16  Basi Danieli akaenda na kumwomba mfalme ampe muda ili amweleze maana ya ndoto yake. 17  Kisha Danieli akarudi nyumbani kwake na kuwajulisha wenzake, Hanania, Mishaeli, na Azaria kuhusu jambo hilo. 18  Akawaambia wasali ili Mungu wa mbinguni awaonyeshe rehema na kuwajulisha siri hiyo, ili yeye Danieli, na wenzake wasiangamizwe pamoja na wale wanaume wengine wenye hekima wa Babiloni. 19  Kisha Danieli akafunuliwa siri hiyo katika maono wakati wa usiku.+ Basi Danieli akamsifu Mungu wa mbinguni. 20  Danieli akasema: “Jina la Mungu na lisifiwe kwa umilele wote,*Kwa maana hekima na uwezo ni wake peke yake.+ 21  Yeye hubadili nyakati na majira,+Huwaondoa wafalme na kuwaweka wafalme,+Huwapa hekima walio na hekima na kuwapa ujuzi wale walio na utambuzi.+ 22  Yeye hufunua mambo yenye kina na mambo yaliyofichika,+ Anajua yaliyo gizani,+Na nuru hukaa pamoja naye.+ 23  Ee Mungu wa mababu zangu, ninakushukuru na kukusifu, Kwa sababu umenipa hekima na nguvu. Na sasa umenijulisha tulichokuomba;Umetujulisha jambo linalomhangaisha mfalme.”+ 24  Kisha Danieli akaenda kwa Arioko, ambaye alikuwa ameteuliwa na mfalme kuwaangamiza wanaume wenye hekima wa Babiloni,+ akamwambia: “Usimwangamize mwanamume yeyote mwenye hekima wa Babiloni. Nipeleke mbele ya mfalme, nami nitamweleza mfalme maana ya ndoto yake.” 25  Mara moja Arioko akampeleka Danieli mbele ya mfalme na kumwambia: “Nimempata mwanamume fulani miongoni mwa watu waliohamishwa kutoka Yuda+ anayeweza kukueleza maana ya ndoto yako.” 26  Mfalme akamuuliza Danieli, aliyeitwa Belteshaza:+ “Je, kweli unaweza kuniambia ndoto niliyoota, na maana yake?”+ 27  Danieli akamjibu mfalme: “Hakuna mwanamume yeyote mwenye hekima, wala mtu anayefanya mazingaombwe, wala kuhani yeyote mchawi, wala mnajimu yeyote anayeweza kukufunulia wewe mfalme siri unayoomba ifunuliwe.+ 28  Lakini kuna Mungu mbinguni ambaye ni Mfunuaji wa siri,+ naye amekujulisha wewe Mfalme Nebukadneza mambo yatakayotukia katika kipindi cha mwisho cha zile siku. Hii ndiyo ndoto yako, na haya ndiyo maono yaliyokujia kichwani ulipokuwa umelala kitandani: 29  “Ee mfalme, ulipokuwa kitandani uliona katika mawazo yako mambo yatakayotukia wakati ujao, na Mfunuaji wa siri amekujulisha mambo yatakayotukia. 30  Lakini siri hii imefunuliwa kwangu si kwa sababu nina hekima nyingi zaidi kuliko mtu yeyote anayeishi, bali ilifunuliwa kwangu ili nikueleze wewe mfalme maana ya ndoto yako ili ujue mawazo yaliyo moyoni mwako.+ 31  “Wewe, Ee mfalme, ulitazama na kuona sanamu kubwa sana. Sanamu hiyo, iliyokuwa kubwa sana na iliyong’aa kupita kiasi, ilisimama mbele yako, nayo ilikuwa yenye kutisha. 32  Kichwa cha sanamu hiyo kilikuwa cha dhahabu bora,+ kifua chake na mikono yake ilikuwa ya fedha,+ tumbo na mapaja yake yalikuwa ya shaba,+ 33  miguu yake ilikuwa ya chuma,+ na kwa sehemu, nyayo zake zilikuwa za chuma na kwa sehemu zilikuwa za udongo wa mfinyanzi.*+ 34  Uliendelea kutazama hadi jiwe likakatwa, si kwa mikono, nalo likaipiga sanamu hiyo kwenye nyayo zake za chuma na za udongo wa mfinyanzi na kuzipondaponda.+ 35  Wakati huo kile chuma, ule udongo wa mfinyanzi, ile shaba, ile fedha, na ile dhahabu, vyote pamoja, vikapondwapondwa na kuwa kama makapi kutoka kwenye uwanja wa kupuria wakati wa kiangazi, kisha upepo ukavipeperusha mbali hivi kwamba hakuna chembe yoyote ya vitu hivyo ingeweza kupatikana. Lakini lile jiwe lililoipiga ile sanamu likawa mlima mkubwa, nalo likaijaza dunia yote. 36  “Hiyo ndiyo ndoto yako, na sasa tutakueleza maana yake. 37  Wewe, Ee mfalme—mfalme wa wafalme ambaye Mungu wa mbinguni amekupa ufalme,+ uwezo, nguvu, na utukufu, 38  na kuwaweka mikononi mwako wanadamu mahali popote ambapo huenda wanaishi, na pia wanyama wa mwituni na ndege wa angani, na kukufanya kuwa mtawala juu ya hao wote+—wewe mwenyewe ndiye kichwa cha dhahabu.+ 39  “Lakini baada yako ufalme mwingine utainuka,+ ulio dhaifu kwako; kisha ufalme mwingine, wa tatu, wa shaba, ambao utaitawala dunia yote.+ 40  “Ufalme wa nne utakuwa wenye nguvu kama chuma.+ Kwa maana kama vile chuma kinavyopondaponda na kusagasaga vitu vingine vyote, naam, kama chuma kinachovunjavunja, ufalme huo utapondaponda na kuzivunjavunja falme hizo zote.+ 41  “Na kama tu ulivyoona kwamba nyayo na vidole vya miguu kwa sehemu vilikuwa vya udongo wa mfinyanzi na kwa sehemu vilikuwa vya chuma, ufalme huo utagawanyika, lakini ugumu fulani wa chuma utakuwa ndani yake, kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi. 42  Na kama vile vidole vyake vya miguu vilikuwa kwa sehemu vya chuma na kwa sehemu vya udongo wa mfinyanzi, ndivyo ufalme huo utakavyokuwa na nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu. 43  Kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi, sehemu hizo zitachanganyika na wanadamu;* lakini hazitashikamana na wanadamu, kama tu chuma kisivyochanganyika na udongo wa mfinyanzi. 44  “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme+ ambao hautaangamizwa kamwe.+ Na ufalme huo hautakabidhiwa watu wengine wowote.+ Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote,+ nao pekee utasimama milele,+ 45  kama tu ulivyoona kwamba jiwe ambalo halikukatwa kwa mikono lilitoka kwenye mlima, na kwamba lilipondaponda kile chuma, ile shaba, ule udongo wa mfinyanzi, ile fedha, na ile dhahabu.+ Mungu Mtukufu amemjulisha mfalme mambo yatakayotukia wakati ujao.+ Ndoto hiyo ni ya kweli, na maana yake inategemeka.” 46  Ndipo Mfalme Nebukadneza akaanguka chini kifudifudi mbele ya Danieli na kumpa heshima kubwa. Naye akaagiza apewe zawadi na kufukiziwa uvumba. 47  Mfalme akamwambia Danieli: “Kwa kweli Mungu wako ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme na Mfunuaji wa siri, kwa sababu uliweza kufunua siri hii.”+ 48  Kisha mfalme akampandisha cheo Danieli na kumpa zawadi nyingi bora, naye akamfanya kuwa mtawala wa mkoa wote wa* Babiloni+ na msimamizi mkuu wa wanaume wote wenye hekima wa Babiloni. 49  Na kwa ombi la Danieli, mfalme akawaweka Shadraki, Meshaki, na Abednego+ kuwa wakuu wa usimamizi wa mkoa wa* Babiloni, lakini Danieli alifanya kazi katika makao ya mfalme.

Maelezo ya Chini

Tnn., “roho yake ikahangaika.”
Yaani, kikundi kilichokuwa stadi katika ubashiri na unajimu.
Tnn., “roho yangu inahangaika.”
Sehemu ya Da 2:4b hadi 7:28 iliandikwa kwa Kiaramu.
Au labda, “maeneo ya takataka; marundo ya mavi.”
Au “katika nchi kavu.”
Tnn., “wenye mwili wa nyama.”
Au “milele hata milele.”
Au “udongo wa mfinyanzi (uliofinyangwa) uliochomwa.”
Au “uzao wa wanadamu,” yaani, watu wa kawaida.
Au “wilaya yote ya utawala ya.”
Au “wilaya ya utawala ya.”