Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAHOJIANO | YAN-DER HSUUW

Mtaalamu wa Biolojia ya Viini-Tete Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Mtaalamu wa Biolojia ya Viini-Tete Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

PROFESA Yan-Der Hsuuw ni kiongozi wa utafiti wa viini-tete katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Taifa cha Pingtung, nchini Taiwan. Awali aliamini katika mageuzi, lakini akabadili maoni yake baada ya kuwa mtafiti wa masuala ya kisayansi. Alimweleza mwandishi wa Amkeni! sababu zilizomfanya abadili imani yake.

Tueleze kidogo kuhusu malezi yako.

Nilizaliwa mwaka wa 1966 na kulelewa nchini Taiwan. Dini ya wazazi wangu ilitegemea mafundisho ya Watao na Wabudha. Ingawa tuliabudu mababu na kutoa sala kwa sanamu, hatukuwahi kufikiria ikiwa kuna Muumba.

Kwa nini ulijifunza biolojia?

Nilipokuwa mtoto, nilipenda sana kutunza wanyama-vipenzi, na nilitaka kujifunza jinsi ya kukomesha kuteseka kwa wanyama na wanadamu. Hivyo kwa kipindi fulani nilisomea tiba ya wanyama, na baadaye nikajifunza biolojia ya viini-tete. Nilitumaini kwamba elimu hiyo ingenisaidia kujua chanzo uhai.

Kwa nini wakati huo uliamini mageuzi?

Maprofesa wa chuo kikuu walifundisha nadharia ya mageuzi, wakidai kuna uthibitisho unaotegemeza fundisho hilo. Mimi niliwaamini.

Kwa nini ulianza kusoma Biblia?

Kwa sababu mbili. Kwanza, niliamini kwamba kwa kuwa kuna miungu mingi, lazima mmoja awe mkuu kuliko wote. Nilijiuliza ni Mungu yupi huyo. Pili, nilijua kuwa Biblia ni kitabu kinachoheshimiwa sana. Hivyo nikaanza masomo ya Biblia.

Nilipoanza masomo kwenye Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Leuven nchini Ubelgiji mwaka wa 1992, nilitembelea kanisa moja la Kikatoliki na kumwomba kasisi anisaidie kuelewa Biblia, lakini alikataa ombi langu.

Kwa hiyo, uhitaji wako wa chakula cha kiroho ulitimizwaje?

Miaka miwili baadaye, nilipokuwa nikifanya utafiti wa kisayansi nchini Ubelgiji, nilikutana na Ruth, mwenyeji wa Poland, ambaye ni Shahidi wa Yehova. Alikuwa amejifunza Kichina ili kuwasaidia wanafunzi wa chuo kikuu waliotaka kujifunza kumhusu Mungu. Kwa kuwa nilikuwa nimesali nipate msaada wa kujifunza Biblia, nilifurahi kukutana naye.

Ruth alinionyesha kwamba Biblia inapatana na sayansi, ingawa si kitabu cha kisayansi. Kwa mfano, Daudi, mwandikaji wa Biblia alisali hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa, kuhusiana na siku ambazo zilifanyizwa na hakukuwako hata moja kati ya hizo.” (Zaburi 139:16) Ingawa Daudi alitumia lugha ya kishairi, alikuwa sahihi. Kabla ya sehemu za mwili kufanyizwa, tayari kuna maagizo ya jinsi mwili utakavyokua. Usahihi wa Biblia ulinithibitishia kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu. Pia, nikaanza kuamini kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli, Yehova. 1

Ni nini kilichokusadikisha kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai?

Lengo moja la utafiti wa kisayansi ni kutafuta ukweli, si kutegemeza mambo ya kuwaziwa. Utafiti wangu wa viini-tete ulibadili maoni yangu, nikafikia mkataa kwamba uhai una chanzo, haukujitokeza. Kwa mfano, mainjinia huunda mifumo ya viwandani ambayo inaunganisha sehemu sahihi za kitu fulani kwa mpangilio na njia inayofaa. Ukuzi wa viini-tete unaweza kufananishwa na mfano huo lakini ni tata zaidi.

Je, ukuzi huo huanza na chembe moja tu iliyotungishwa?

Ndiyo. Kisha chembe hiyo isiyoonekana kwa macho huanza kugawanyika. Kwa kipindi fulani, idadi ya chembe huongezeka mara mbili ndani ya kila saa 12 hadi 24. Mwanzoni mwa hatua hiyo, chembe zinazoitwa chembe za msingi zinafanyizwa. 2 Chembe hizo za msingi zinaweza kutokeza karibu aina zote 200 hivi za chembe zinazohitajiwa ili mtoto azaliwe akiwa kamili. Aina hizo 200 hivi zinatia ndani chembe za damu, za mifupa, za neva, na kadhalika.

Utafiti wangu wa viini-tete umenithibitishia kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai

Chembe zinazofaa lazima zitokezwe kwa mpangilio na mahali sahihi. Kwanza chembe hizo huungana kufanyiza tishu, kisha tishu zinaungana na kuwa viungo. Ni injinia gani anayeweza kuandika maagizo ya mfumo kama huo? Isitoshe, maagizo ya ukuzi wa viini-tete yameandikwa kwa njia ya pekee katika DNA. Ninapofikiria utaratibu huo mzuri ninasadiki kwamba uhai ulibuniwa na Mungu.

Kwa nini uliamua kuwa Shahidi wa Yehova?

Nilivutiwa na upendo wao. Yesu Kristo alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo huo hauna ubaguzi. Hauathiriwi na taifa, tamaduni, au rangi ya mtu. Nilijionea mwenyewe upendo wa aina hiyo nilipoanza kushirikiana na Mashahidi.

^ 2. Kwa sababu ya dhamiri yake, Profesa Yan-Der Hsuuw hatumii chembe za msingi za viini-tete vya wanadamu katika utafiti wake.