Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utachagua Kuamini Nini?

Utachagua Kuamini Nini?

“Ulimwengu unaweza kujiumba wenyewe, na utajiumba.”​—Stephen Hawking na Leonard Mlodinow, wataalamu wa fizikia, 2010.

“Mungu aliumba mbingu na dunia.”​—Biblia, Mwanzo 1:1.

Je, ulimwengu na viumbe vilivyomo viliumbwa na Mungu au vilijitokeza vyenyewe tu bila utaratibu wowote? Maneno ya wataalamu wawili wa fizikia walionukuliwa mwanzoni mwa makala hii na maneno ya kwanza katika Biblia, yanatoa majibu yanayotofautiana kabisa. Kila upande una watu wanaoamini kabisa maoni yao. Hata hivyo, watu wengi hawana uhakika. Kumekuwa na mabishano mengi kuhusu mada hiyo ambayo yameandikwa kwenye vitabu maarufu au kuonyeshwa kwenye vipindi mbalimbali vya televisheni.

Huenda walimu wako walikufundisha kwa usadikisho kabisa kwamba ulimwengu na viumbe vilivyomo vilijitokeza vyenyewe tu, na kwamba hakuna Muumba. Lakini, je, walimu wako walikupatia uthibitisho kwamba hakuna Muumba? Kwa upande mwingine, huenda umewasikia walimu wa dini wakihubiri kwamba kuna Muumba. Lakini je, walikuthibitishia kwamba kweli kuna Muumba? Au walikwambia uamini jambo hilo kwa sababu tu ni “imani” au fundisho la kidini?

Huenda umefikiria swali hili na unahisi kwamba hakuna mtu yeyote anayeweza kujua kwa uhakika ikiwa kuna Muumba au la. Na huenda unajiuliza swali lingine: Je, kuna umuhimu wowote wa kujua jibu la swali hilo?

Kwanza, gazeti hili la Amkeni! litaeleza baadhi ya mambo ya hakika ambayo yamewachochea watu wengi kuamini kwamba kuna Muumba. Kisha, litaeleza kwa nini kujua chanzo cha uhai duniani ni jambo muhimu sana.