Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri?

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri?

Vijana Huuliza

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri?

“Nimepata nafasi nzuri sana za kuzungumza kuhusu imani yangu shuleni. Lakini sikuzitumia.”—Kaleb. *

“Mwalimu wetu aliuliza wanafunzi maoni yao kuhusu mageuzi. Nilijua kwamba hii ilikuwa nafasi nzuri ya kuwahubiria. Lakini niliogopa sana hivi kwamba sikusema chochote. Baadaye, nilihisi vibaya sana.”—Jasmine.

IKIWA wewe ni kijana Mkristo, huenda umehisi kama Kaleb na Jasmine. Kama wao, huenda wewe pia unapenda kweli za Biblia ambazo umejifunza na unataka kuwaambia wengine kuzihusu. Hata hivyo, huenda ukaogopa kuzungumza na wengine kuhusu imani yako. Lakini unaweza kupata ujasiri. Jinsi gani? Kila mwaka chukua hatua zifuatazo ili ujitayarishe:

1. Tambua unachoogopa. Unapofikiria kuwahubiria wengine, ni rahisi kuwazia tu mambo mabaya yanayoweza kutokea! Hata hivyo, nyakati nyingine unaweza kupunguza woga wako kwa kuandika jinsi unavyohisi.

Kamilisha sentensi ifuatayo.

▪ Nikihubiri shuleni, huenda jambo hili litatokea:

․․․․․

Huenda ukafarijika kujua kwamba vijana wengine Wakristo wanahisi kama wewe. Kwa mfano, Christopher mwenye umri wa miaka 14 anasema hivi, “Ninaogopa watoto watanidhihaki na kusema mimi ni mtu wa ajabu.” Na Kaleb aliyetajwa mwanzoni, anasema, “Nilikuwa na wasiwasi kwamba mtu fulani angeniuliza swali ambalo singeweza kujibu.”

2. Kabiliana na kipingamizi. Huenda una sababu nzuri ya kuogopa. “Watoto fulani walijifanya wanapendezwa na imani yangu,” anasema Ashley. “Lakini baadaye walipotosha maneno yangu na kunidhihaki mbele ya wengine.” Nicole, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi kuhusu hali iliyompata: “Mvulana mmoja alilinganisha mstari fulani katika Biblia yake na mstari huohuo katika Biblia yangu, na maneno yalikuwa tofauti. Alisema kwamba Biblia yangu ilikuwa imebadilishwa. Nilishtuka! Sikujua la kusema.” *

Huenda hali kama hizo zikakuogopesha sana! Lakini badala ya kuhepa, chukua hali hizo kuwa sehemu ya kawaida ya maisha ya Mkristo. (2 Timotheo 3:12) “Yesu alisema kwamba wafuasi wake watateswa,” anasema Matthew mwenye umri wa miaka 13, “hivyo hatuwezi kumtarajia kila mtu atupende au apende imani yetu.”—Yohana 15:20.

3. Fikiria faida. Je, kunaweza kuwa na matokeo yoyote mazuri kutokana na hali inayoonekana kuwa mbaya? Amber, mwenye umri wa miaka 21, ana maoni hayo. “Si rahisi kuwahubiria watu wasioheshimu Biblia,” anasema, “lakini kufanya hivyo kunakusaidia kuelewa na kuchunguza mambo unayoamini.”—Waroma 12:2.

Tazama tena kile ulichoandika katika Hatua ya 1. Fikiria angalau faida mbili unazoweza kupata kutokana na hali hiyo, na uziandike hapa chini.

1 ․․․․․

2 ․․․․․

Pendekezo: Kuwahubiria wengine kunaweza kukupunguziaje shinikizo kutoka kwa marafiki? Kuwahubiria kutakusaidiaje ujiamini zaidi? Kutaboreshaje hisia zako kumwelekea Yehova Mungu? Yehova atahisije kukuhusu?—Methali 23:15.

4. Jitayarishe. “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu,” linasema andiko la Methali 15:28. Zaidi ya kutafakari mambo utakayosema, jaribu kufikiria maswali ambayo huenda watu wakauliza. Fanya utafiti kuhusu habari hizo, na utayarishe jibu unaloweza kutoa kwa urahisi.—Ona chati  “Panga Utakavyojibu,” kwenye ukurasa wa 25.

5. Jinsi ya kuanza. Unapokuwa tayari kuwahubiria wengine, utaanzaje? Kuna njia mbalimbali. Kuwahubiria wengine ni kama kuogelea: Watu fulani huingia ndani ya maji polepole; wengine hujitosa moja kwa moja majini. Vivyo hivyo, unaweza kuanza kwa kuzungumzia mambo yasiyohusu dini na kuona ikiwa mtu huyo anapendezwa. Lakini ikiwa una wasiwasi kwamba utakosea, huenda ikawa bora zaidi ‘kujitosa moja kwa moja.’ (Luka 12:11, 12) “Wazo tu la kuwahubiria wengine hunitia wasiwasi zaidi kuliko kuwahubiria,” anasema Andrew mwenye umri wa miaka 17. “Mara tu nilipoanzisha mazungumzo, ilikuwa rahisi kuliko nilivyofikiria!” *

6. Uwe mwenye busara. Kama vile huwezi kupiga mbizi ndani ya maji yasiyo na kina, jihadhari usijihusishe na mabishano yasiyo na maana. Kumbuka, kuna wakati wa kusema na wakati wa kukaa kimya. (Mhubiri 3:1, 7) Nyakati nyingine, hata Yesu alikataa kujibu maswali. (Mathayo 26:62, 63) Na kumbuka kanuni hii: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Methali 22:3, Union Version.

Hivyo, ukiona kwamba mtabishana, ‘usiendelee mbele.’ Badala yake, mpe jibu fupi kwa busara. Kwa mfano, mwanafunzi mwenzako akikuuliza kwa dhihaka, ‘Kwa nini huvuti sigara?’ unaweza kusema, ‘Kwa sababu sipendi kuuchafua mwili wangu!’ Ikitegemea jibu lake, utaamua ikiwa utamweleza zaidi kuhusu mambo unayoamini.

Hatua zilizotajwa zinaweza kukusaidia ‘sikuzote kuwa tayari kuitetea’ imani yako. (1 Petro 3:15) Bila shaka, kuwa tayari hakumaanishi kwamba hutaogopa. Lakini Alana, mwenye umri wa miaka 18, anasema: “Unapowahubiria wengine hata ingawa unaogopa, unahisi ni kama umetimiza jambo fulani—umekabiliana na woga wako ingawa ulijua kwamba huenda hutapata matokeo mazuri. Unapokuwa na matokeo mazuri, unahisi vizuri hata zaidi! Utafurahi kwa sababu ulikuwa na ujasiri na ukahubiri.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 11 Tafsiri za Biblia hutumia maneno tofauti. Hata hivyo, tafsiri fulani zinashikamana sana na lugha za awali ambazo zilitumiwa kuandika Biblia.

^ fu. 19 Ona sanduku  “Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo,” kwenye ukurasa wa 26.

[MAMBO YA KUFIKIRIA

Je, inawezekana kwamba mwanafunzi fulani katika shule yenu ana mawazo kama haya?

‘Ninajua wewe ni Shahidi wa Yehova. Huenda ukafikiri nitakudhihaki, lakini ninakuheshimu sana. Inakuwaje kwamba wewe ni mtulivu hivyo ingawa kuna matatizo mengi sana ulimwenguni? Mimi ninaogopa. Je, kutakuwa na vita vingine hivi karibuni? Je, wazazi wangu watatalikiana? Je, nitamaliza masomo shuleni leo bila kupigwa risasi au kudungwa kisu? Nina maswali mengi sana, lakini inaonekana wewe una kusudi maishani na unajua unachotaka kufanya. Dini yako ndiyo inayofanya uwe hivyo, sivyo? Ningependa kuzungumza nawe kuhusu mambo hayo, lakini ninaogopa kuanzisha mazungumzo. Tafadhali unaweza kuzungumza nami?’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Watoto fulani walinicheka nilipowahubiria. Lakini kwa kawaida wao huachana nami wanapotambua kwamba sijali hata wanaponidhihaki.”—Francesca, Luxembourg.

“Ukikosa kuwahubiria wengine, unaweza kusahau kwamba wewe ni Mkristo na uanze kufanya mambo kama watu wengine. Hupaswi kuwafuata watu; unapaswa kudumisha msimamo wako.”—Samantha, Marekani.

“Nilipokuwa mdogo, sikutaka kuwa tofauti na watoto wengine. Lakini nilianza kutambua jinsi imani yangu inavyonifanya niwe na maisha bora zaidi. Hilo lilinisaidia niwe na uhakika hata zaidi na kunifanya nijivunie mambo ninayoamini.”—Jason, New Zealand.

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

 JINSI YA KUANZISHA MAZUNGUMZO

“Unapanga kufanya nini wakati wa likizo?” [Baada ya kusikiliza jibu, taja mipango yako ya kiroho, kama vile kuhudhuria kusanyiko au kutumia wakati mwingi zaidi kuhubiri.]

▪ Taja habari ya karibuni, kisha umwulize: “Je, ulisikia habari hiyo? Una maoni gani kuihusu?”

“Je, unafikiri hali ya kiuchumi ulimwenguni [au tatizo lingine] itakuwa bora? [Mruhusu ajibu.] kwa nini unasema hivyo?”

“Wewe ni wa dini gani?”

“Unafikiri maisha yako yatakuwaje miaka mitano ijayo?” [Baada ya kusikiliza jibu, mweleze miradi yako ya kiroho.]

[Chati katika ukurasa wa 25]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Panga Utakavyojibu

Kata hapa!

Pendekezo: Zungumzia chati hii pamoja na wazazi na marafiki wako. Kamilisha chati hii. Kisha fikiria maswali mengine ambayo wanafunzi wenzako wanaweza kuuliza.

Maadili

Swali

Maoni yako ni ni kuhusu ushoga?

Jibu

Siwachukii mashoga ila sikubaliani na mwenendo wao.

Swali lingine

Je, hayo si ni maoni yenye ubaguzi?

Utafiti

1 Wakorintho 6:9, 10; Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, sura ya 28. *

Jibu

Hapana, kwa sababu sikubaliani na aina zote za ukosefu wa maadili si ushoga peke yake.

Mpenzi

Swali

Kwa nini huna mpenzi?

Jibu

Nimeamua kutokuwa na mpenzi hadi nitakapokuwa mtu mzima.

Swali lingine

Je dini yako inakukataza?

Utafiti

Wimbo wa Sulemani 8:4; Vijana Huuliza, Buku la 2, Sura ya 1.

Jibu

Ndiyo. Sisi huwa na wapenzi tunapokuwa tayari kuoa au kuolewa, na siko tayari kufanya hivyo bado!

Kutokuwamo

Swali

Kwa nini husalimu bendera?

Jibu

Ninaheshimu nchi ninamoishi, lakini siiabudu.

Swali lingine

Kwa hiyo huwezi kupigania nchi yako?

Utafiti

Isaya 2:4; Yohana 13:35; Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 148-151. *

Jibu

Hapana, na mamilioni ya Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingine hawawezi kupigana dhidi ya nchi hii.

Damu

Swali

Kwa nini hukubali kutiwa damu mishipani?

Jibu

Ninakubali matibabu salama kupitia mishipa​—ambayo hayana hatari ya kuambukiza UKIMWI. Lakini Biblia inasema tujiepushe na damu, kwa hiyo sikubali kutiwa damu mishipani.

Swali lingine

Lakini namna gani ikiwa unachungulia kaburi? Si Mungu atakusamehe?

Utafiti

Matendo 5:28, 29; Waebrania 11:6; Kitabu Bibia inafundisha, ukurasa wa 129-131.

Jibu

Maamuzi

Swali

Fulani ni mshiriki wa kanisa lenu, na alifanya hivi na vile. Kwa nini wewe huwezi kufanya hivyo?

Jibu

Tunafundishwa sheria za Mungu, na hatulazimishwi kuzifuata! Kila mtu lazima afanye maamuzi yake mwenyewe.

Swali lingine

Si hilo linaonyesha kwamba dini yenu ina viwango mbalimbali

Utafiti

Jibu

Uumbaji

Swali

Kwa nini huamini mageuzi?

Jibu

Kwa nini niamini mageuzi? Hata wanasayansi wenyewe hawakubaliani kuhusu mageuzi, na eti hao ndio wataalamu!

Swali lingine

Utafiti

Jibu

[Maelezo ya chini]

^ fu. 55 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 77 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kuwahubiria wengine ni kama kuogelea. Unaweza kuanza polepole au unaweza kujitosa moja kwa moja!