Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuishi Milele Duniani

Unaweza Kuishi Milele Duniani

TUMAINI HILO LINAVUTIA KWELIKWELI! Muumba wetu ameahidi kutupatia uzima wa milele, hapa hapa duniani. Hata hivyo, wengi hawaamini ahadi hiyo. Wanasema, ‘Kila mtu atakufa siku moja. Uhai na kifo ni sehemu ya mzunguko wetu wa maisha.’ Wengine wanahisi kwamba inawezekana kuishi milele, lakini si hapa duniani. Wanasema kwamba mtu anaweza kupata uzima wa milele baada ya kufa na kwenda mbinguni. Wewe una maoni gani?

Kabla ya kujibu swali hilo, unaonaje ikiwa utachunguza jinsi Biblia inavyojibu maswali haya matatu: Mwanadamu alikusudiwa kuishi muda mrefu kadiri gani, hasa tukifikiria jinsi alivyoumbwa? Mungu alikuwa na kusudi gani alipoumba dunia na wanadamu? Ilikuwaje wanadamu wakaanza kufa?

MWANADAMU—KIUMBE WA PEKEE

Kati ya viumbe wote ambao Mungu amewaumba duniani, wanadamu ni wa pekee sana. Jinsi gani? Biblia inasema kwamba wanadamu tu ndio walioumbwa kwa “mfano” na “sura” ya Mungu. (Mwanzo 1:26, 27) Hilo linamaanisha nini? Wanadamu wameumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha utu na sifa za Mungu, kama vile upendo na haki.

Kwa kuongezea, wanadamu wana uwezo wa kufikiri na kupambanua mambo, na wanaweza kutofautisha mema na mabaya na kusitawisha uhusiano na Mungu. Hiyo ndiyo sababu tunaweza kutambua jinsi ulimwengu ulivyo wenye kupendeza, na kuvutiwa na maajabu ya uumbaji, sanaa, muziki, na mashairi. Zaidi ya yote, wanadamu wana uwezo wa kumwabudu Muumba wao. Sifa hizo zinafanya wanadamu wawe tofauti kabisa na viumbe wengine wote wanaoishi duniani.

Sasa basi, hebu jiulize: Je, kweli Mungu angetupatia sifa zote hizo nzuri, pamoja na uwezo usio na kikomo wa kuziboresha, ikiwa alikusudia tuishi kwa miaka michache tu? Ukweli ni kwamba Mungu aliwapatia wanadamu sifa na uwezo huo wa pekee ili wafurahie maisha hapa duniani milele.

KUSUDI LA MUNGU

Hata hivyo, baadhi ya watu husema Mungu hakukusudia wanadamu waishi milele duniani. Wanadai kwamba dunia iliumbwa kuwa makao ya muda ya wanadamu, ili kuwapima na kuona wale wanaostahili kwenda kuishi milele mbinguni pamoja na Mungu. Lakini ikiwa jambo hilo lingekuwa kweli, basi lingemaanisha kwamba Mungu ndiye anayesababisha uovu na mambo yote mabaya yaliyojaa duniani. Hiyo ingepingana moja kwa moja na jinsi Mungu alivyo. Biblia inasema hivi kumhusu: “Kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu ambaye kamwe hana ukosefu wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Biblia inataja waziwazi kusudi la Mungu la kuiumba dunia inaposema: “Mbingu ni za Yehova, lakini dunia amewapa wanadamu.” (Zaburi 115:16) Mungu aliiumba dunia ili iwe makao mazuri na ya kudumu ya wanadamu, na alituwekea kila kitu tunachohitaji ili tufurahie maisha milele.—Mwanzo 2:8, 9.

“Mbingu ni za Yehova, lakini dunia amewapa wanadamu.”​—Zaburi 115:16

Biblia pia inataja waziwazi kusudi la Mungu kwa wanadamu. Aliwapatia wazazi wetu wa kwanza jukumu la “[kuijaza] dunia na kuitiisha, na [kutawala] . . . kila kiumbe aliye hai anayetembea duniani.” (Mwanzo 1:28) Lilikuwa pendeleo kubwa sana kwao kuitunza na kuipanua Paradiso ili ienee duniani kote! Kwa kweli, Adamu na Hawa pamoja na wazao ambao wangepata, hawakutarajia thawabu ya kwenda mbinguni, bali walikuwa na tumaini la kuishi milele duniani.

KWA NINI TUNAKUFA?

Hivyo basi, kwa nini tunakufa? Biblia inaonyesha kwamba mmoja wa viumbe wa roho wa Mungu, ambaye baadaye aliasi na akaitwa Shetani Ibilisi, alijaribu kuvuruga mipango ya Mungu huko Edeni. Jinsi gani?

Shetani aliwashawishi wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wajiunge naye na kumwasi Mungu. Shetani alipodai kwamba Mungu alikuwa akiwanyima mambo mazuri, yaani, uhuru wa kujiamulia mema na mabaya, walijiunga naye na wakaamua kumwasi Mungu. Matokeo? Hatimaye walikufa, kama tu ambavyo Mungu alikuwa amewaonya. Walipoteza tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani.—Mwanzo 2:17; 3:1-6; 5:5.

Uasi wa Adamu na Hawa umewaathiri wanadamu wote. Neno la Mungu linasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote.” (Waroma 5:12) Tunakufa kwa sababu tumerithi dhambi na kifo kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, na wala si kwa sababu ya ‘mipango’ ya Mungu ambayo sisi hatuwezi kuielewa.

UNAWEZA KUISHI MILELE DUNIANI

Uasi uliotokea Edeni haukubadili kusudi la Mungu kwa wanadamu na dunia. Mungu alichochewa na upendo wake mkamilifu na sifa ya haki kuandaa njia ya kutukomboa kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo. Mtume Paulo alielezea hivi: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Kwa upendo, Mungu alimtoa “Mwana wake mzaliwa pekee [Yesu Kristo], ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa kujitoa kwa hiari ili kuwa dhabihu ya fidia, Yesu alikomboa kila kitu ambacho Adamu alipoteza. *

Hivi karibuni, ahadi ya Mungu kuhusu dunia paradiso itatimia. Utafurahia maisha mazuri katika dunia hiyo ikiwa utatii himizo hili la Yesu: “Ingieni kupitia lango jembamba, kwa sababu lango ni pana, na barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa, na ni wengi wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na ni wachache wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Wakati wako ujao uko mikononi mwako. Utaamua nini?

^ Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi fidia inavyoweza kukunufaisha, soma somo la 27 la kitabu Furahia Maisha Milele! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, na unachoweza kukipakua bila malipo yoyote kwenye tovuti ya www.mt711.com/sw.