Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini maana ya kuunganisha vijiti viwili vinavyotajwa katika Ezekieli sura ya 37?

Pia, ujumbe huo ulitabiri kuunganishwa kwa watu wa Mungu kulikoanza katika kipindi cha siku za mwisho.

Yehova alimwambia nabii wake Ezekieli aandike juu ya vijiti viwili. Alipaswa kuandika hivi juu ya kijiti kimoja: “Kwa Yuda na kwa wenzake, wana wa Israeli,” na juu ya kile kingine, “Kwa Yosefu, kijiti cha Efraimu, na wenzake, nyumba yote ya Israeli.” Vijiti hivyo viwili vilipaswa “viwe kijiti kimoja” mkononi mwa Ezekieli.—Eze. 37:15-17.

“Efraimu” liliwakilisha nini? Efraimu lilikuwa kabila ambalo Yeroboamu, mfalme wa kwanza wa ufalme wa kaskazini lenye makabila kumi alitoka, na ndilo lililokuwa kabila lenye watu wengi zaidi. (Kum. 33:13, 17; 1 Fal. 11:26) Kabila hilo lilitokana na mwana wa Yosefu aliyeitwa Efraimu. (Hes. 1:32, 33) Yosefu alikuwa amepokea baraka ya pekee kutoka kwa Yakobo, baba yake. Hivyo, ilifaa kukiita kijiti kilichowakilisha ufalme wa makabila kumi, “kijiti cha Efraimu.” Kufikia wakati ambapo Ezekieli aliandika unabii kuhusu vijiti hivyo viwili, muda mrefu ulikuwa umepita tangu watu katika ufalme wa kaskazini wa Israeli wapelekwe uhamishoni huko Ashuru mwaka wa 740 K.W.K. (2 Fal. 17:6) Hivyo, kufikia wakati huo, Waisraeli wengi walikuwa wametawanyika kotekote katika Milki ya Babiloni, iliyokuwa imechukua nafasi ya Milki ya Ashuru.

Katika mwaka wa 607 K.W.K., huenda baadhi ya watu waliobaki kutoka katika ufalme wa kaskazini pamoja na wakazi wa ufalme wa kusini wenye makabila mawili, walipelekwa uhamishoni Babiloni. Wafalme wa ukoo wa Yuda walitawala makabila hayo mawili, nao walihusianishwa na makuhani waliotumikia katika hekalu lililokuwa Yerusalemu. (2 Nya. 11:13, 14; 34:30) Hivyo, ilifaa kwamba kijiti cha “Yuda” kiwakilishe ufalme huo wa makabila mawili.

Vijiti hivyo viwili viliunganishwa lini? Vijiti hivyo viliunganishwa wakati ambapo Waisraeli walirudi kujenga upya hekalu la Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. Watu kutoka katika ufalme wa makabila mawili na ufalme wa makabila kumi walirudi wakiwa pamoja kutoka uhamishoni. Hakukuwa na mgawanyiko tena kati ya wana wa Israeli. (Eze. 37:21, 22) Kwa mara nyingine, Waisraeli walimtumikia Yehova kwa umoja. Pia, kuunganishwa huko kulikuwa kumetabiriwa na nabii Isaya na Yeremia.—Isa. 11:12, 13; Yer. 31:1, 6, 31.

Ni ukweli gani muhimu kuhusu ibada safi unaoonyeshwa na unabii huo? Ni ukweli huu: Yehova atawafanya waabudu wake wawe kitu “kimoja.” (Eze. 37:18, 19) Je, ahadi hiyo inayohusu umoja imetimia katika siku zetu? Ndiyo. Mwanzoni, unabii huo ulianza kutimia mwaka wa 1919, watu wa Mungu walipopangwa upya hatua kwa hatua na kuunganishwa tena. Jitihada za Shetani za kusababisha mgawanyiko wa kudumu kati yao zilishindwa.

Wakati huo, watu wengi kati ya wale waliokuwa wameunganishwa walikuwa na tumaini la kuwa wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufu. 20:6) Waliwakilisha kijiti cha Yuda kwa njia ya mfano. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, watu wengi wenye tumaini la kuishi duniani walianza kujiunga na Wayahudi hao wa kiroho. (Zek. 8:23) Walikuwa kama kijiti cha Yosefu, na hawakuwa na tumaini la kutawala pamoja na Kristo.

Leo, vikundi vyote viwili vya watu wa Yehova vinatumikia kwa umoja chini ya Mfalme mmoja, Yesu Kristo, anayetajwa katika unabii kuwa “mtumishi wangu Daudi.” (Eze. 37:24, 25) Yesu alisali kwamba wafuasi wake wangekuwa ‘kitu kimoja, kama vile ambavyo Baba yumo katika muungano pamoja naye, na Yesu yuko katika muungano pamoja na Baba.’ * (Yoh. 17:20, 21) Pia, Yesu alitabiri kwamba kundi dogo la wafuasi wake watiwa mafuta lingekuwa “kundi moja” na “kondoo wengine.” Wote wangekuwa chini ya “mchungaji mmoja.” (Yoh. 10:16) Maneno hayo ya Yesu yanafafanua vizuri sana umoja wa kiroho wa watu wa Yehova leo, licha ya tumaini walilo nalo la wakati ujao!

^ fu. 6 Inapendeza kuona jinsi ambavyo Yesu aliorodhesha mambo alipotumia mifano ambayo ilikuwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake. Kwanza, alizungumzia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” kikundi kidogo cha ndugu watiwa mafuta ambao wangeongoza. (Mt. 24:45-47) Kisha, alitoa mifano ambayo iliwahusu hasa wale wote wenye tumaini la kwenda mbinguni. (Mt. 25:1-30) Mwishowe, alizungumzia wale wenye tumaini la kuishi duniani ambao wangewategemeza ndugu za Kristo. (Mt. 25:31-46) Vivyo hivyo, utimizo wa kisasa wa unabii wa Ezekieli unawahusu wale walio na tumaini la kwenda mbinguni. Ingawa kwa kawaida ufalme wa makabila kumi haufananishi wale walio na tumaini la kuishi duniani, kuunganishwa kunakozungumziwa katika unabii huo kunatukumbusha umoja uliopo kati ya wale walio na tumaini la kuishi duniani na wale walio na tumaini la kwenda mbinguni.