Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Nchini Taiwan

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Nchini Taiwan

MIAKA mitano hivi iliyopita, Choong Keon na Julie, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka 35 hivi walikuwa mapainia wa kawaida huko Sydney, Australia. Choong Keon anasema hivi: “Tulifanya kazi ya muda na kuishi raha mustarehe. Hali ya hewa ilikuwa nzuri sana mahali tulipoishi, na tuliishi maisha mazuri. Tulifurahia kuwa karibu na familia na rafiki zetu.” Hata hivyo, Choong Keon na Julie walisumbuliwa na dhamiri. Kwa nini? Walijua kwamba hali zao ziliwaruhusu kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova, lakini walisita kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa.

Kisha, wakiwa kusanyikoni mwaka wa 2009, walisikia hotuba iliyowagusa moyo sana. Hotuba hiyo ilielekezwa hasa kwa wale walioweza kupanua utumishi wao. Msemaji alisema: “Fikiria mfano huu: Dereva anaweza kulielekeza gari lake upande wa kushoto au wa kulia ikiwa tu gari hilo linasonga. Vivyo hivyo, Yesu anaweza kutuongoza kupanua huduma yetu ikiwa tu tunasonga mbele, yaani, ikiwa tunajitahidi kufikia mradi wetu.” * Wenzi hao walihisi kwamba msemaji alikuwa akizungumza nao moja kwa moja. Katika kusanyiko hilohilo, wenzi fulani wa ndoa wamishonari wanaotumika Taiwan walihojiwa. Walisimulia shangwe waliyopata katika huduma na kukazia kwamba bado kulikuwa na uhitaji mkubwa sana. Choong Keon na Julie walihisi tena kwamba maneno hayo yaliwahusu.

Julie anasema hivi: “Baada ya kusanyiko hilo, tulisali kwa Yehova ili atupe ujasiri wa kufanya uamuzi wa kuhamia Taiwan.” Anaongezea hivi: “Lakini tuliogopa. Tulihisi ni kana kwamba tunataka kupiga mbizi katika sehemu yenye kina ya kidimbwi bila kujua kuogelea.” Andiko lililowasaidia “kupiga mbizi” ni Mhubiri 11:4, linalosema hivi: “Anayeuangalia upepo hatapanda mbegu; naye anayetazama mawingu hatavuna.” Choong Keon anasema hivi: “Tuliamua kwamba badala ya kuendelea  ‘kuangalia na kutazama,’ tutaanza ‘kupanda na kuvuna.’” Walisali tena na tena, wakasoma masimulizi ya maisha ya wamishonari, na pia walituma na kupokea barua-pepe nyingi kutoka kwa wale ambao tayari wamehamia Taiwan. Wakauza magari na fanicha zao, kisha wakahamia Taiwan baada ya miezi mitatu.

KUPATA SHANGWE YA KUHUBIRI

Kwa sasa, kuna ndugu na dada zaidi ya 100 kutoka nchi nyingine wanaotumika nchini Taiwan katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Wametoka Australia, Hispania, Japani, Kanada, Korea, Marekani, Ufaransa, na Uingereza, na wana umri wa kati ya miaka 21 na 73. Miongoni mwao kuna dada waseja zaidi ya 50. Ni nini ambacho kimewasaidia ndugu na dada hao wenye bidii kutumika katika nchi ya kigeni? Acheni tuone.

Laura

Laura, dada mseja kutoka Kanada, anatumika akiwa painia magharibi mwa Taiwan. Lakini miaka kumi hivi iliyopita, hakupenda kamwe kuhubiri. Anasema hivi: “Sikufurahia utumishi kwa sababu nilihubiri kijuujuu tu.” Kisha rafiki zake nchini Kanada walimwalika aende nao Mexico ili wakahubiri pamoja kwa mwezi mmoja. “Ilikuwa mara yangu ya kwanza kutumia muda mwingi katika utumishi, na nilifurahia sana!”

Jambo hilo lenye kufurahisha lilimchochea Laura kufikiria kuhamia kutaniko la lugha ya kigeni nchini Kanada. Alijiunga na darasa la kujifunza Kichina, akatumika katika kikundi cha Kichina, kisha akajiwekea mradi wa kuhamia Taiwan. Alihamia huko mnamo Septemba 2008. Laura anasema hivi: “Ilinichukua karibu mwaka mzima kuzoea mazingira yangu mapya, lakini sasa sitamani kurudi Kanada.” Anahisije kuhusu kazi ya kuhubiri? Anasema: “Inaniletea shangwe kwelikweli. Hakuna jambo linaloridhisha zaidi kuliko kuona wanafunzi wa Biblia wakimjua Yehova na kufanya mabadiliko maishani mwao. Nimepata fursa ya kuonja shangwe hiyo nyingi kwa sababu ya kutumika nchini Taiwan.”

 KUKABILIANA NA CHANGAMOTO YA KUJIFUNZA LUGHA MPYA

Brian na Michelle

Brian na Michelle, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka 35 hivi kutoka Marekani walihamia Taiwan miaka minane hivi iliyopita. Mwanzoni, walihisi kwamba hawatimizi mengi katika huduma. Lakini mmishonari mwenye uzoefu aliwaambia hivi: “Hata ukifaulu kumpa mtu trakti tu, unapaswa kukumbuka kwamba huenda ndiyo mara ya kwanza kwa mtu huyo kusikia ujumbe kumhusu Yehova. Kwa hiyo, tayari unatimiza jambo muhimu katika huduma!” Maneno hayo yenye kutia moyo yaliwasaidia sana Brian na Michelle kutokata tamaa. Ndugu mwingine aliwaambia hivi: “Ili msivunjike moyo, pimeni maendeleo yenu ya kujifunza Kichina baada ya kila kusanyiko, msifanye hivyo siku baada ya siku.” Na kwa kweli walifanya maendeleo, na sasa ni mapainia wenye matokeo.

Ni nini kinachoweza kukuchochea kukabili changamoto ya kujifunza lugha ya kigeni? Jitahidi kutembelea nchi unayotaka kuhamia. Hudhuria mikutano huko, shirikiana na ndugu na dada wenyeji, na kuhubiri pamoja nao. Brian anasema hivi: “Ukiona wengi wakiitikia vizuri ujumbe wa Ufalme na kuona upendo mchangamfu wa ndugu na dada, utachochewa kukabiliana na changamoto za kutumika katika nchi nyingine.”

NAMNA GANI KAZI YA KIMWILI?

Kristin na Michelle

Mapainia wengi waliohamia Taiwan kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi hujitegemeza kifedha kwa kufundisha Kiingereza. Kristin na Michelle huuza samaki. Kristin anasema hivi: “Sikuwa nimewahi kufanya kazi kama hiyo, lakini inanisaidia kuishi katika nchi hii.” Baada ya muda, Kristin alipata wateja walionunua samaki kwa ukawaida. Kazi hiyo ya muda inamtegemeza kifedha pamoja na mke wake, na inawawezesha kuwa na wakati wa kutosha wa kufanya kazi yao muhimu zaidi ya kuvua watu, yaani, kazi ya upainia.

“FURAHIA SAFARI”

William na Jennifer, wenzi wa ndoa kutoka Marekani waliwasili Taiwan miaka saba hivi iliyopita. William anasema hivi: “Kujifunza lugha, kufanya upainia, kulitunza kutaniko, na kujitegemeza kifedha ni mambo yanayochosha pindi nyingine.” Ni nini ambacho kimewasaidia kufanikiwa na kudumisha furaha yao? Wanajitahidi kujiwekea miradi wanayoweza kutimiza. Kwa mfano, hawakutarajia kujifunza Kichina haraka, na hivyo hawakuvunjika moyo sana walipoona wanafanya maendeleo polepole.

William na Jennifer

William anakumbuka mwangalizi fulani anayesafiri alimwambia hivi siku moja: “Furahia safari, si mwisho wa safari tu.” Yaani, baada ya kuweka mradi wa kiroho, tunapaswa kufurahia hatua tunazopiga ili tutimize mradi wetu. William anasema kwamba kutumia shauri hilo kulimsaidia yeye na mke wake kufanya mabadiliko kulingana na hali, kusikiliza ushauri wa ndugu wenyeji wanaoongoza, na kubadili njia yao ya kufanya mambo ili wafanikiwe kutimiza huduma yao katika nchi ya kigeni. Anaongezea hivi: “Hilo pia lilitusaidia kukumbuka kutenga wakati wa kufurahia mandhari maridadi ya kisiwa hicho.”

Sawa na William na Jennifer, Megan, dada mseja painia kutoka Marekani ‘anafurahia safari yake’ anapojitahidi kufikia mradi wake wa kuongea Kichina kwa ufasaha zaidi. Kila mwisho-juma, anajiunga na kikundi kinachohubiri eneo zuri ajabu katika bandari kubwa zaidi nchini Taiwan, bandari ya Kaohsiung. Megan amehubiri habari njema kutoka meli moja hadi nyingine na kuwahubiria wavuvi kutoka Bangladesh, India, Indonesia, Thailand, Ufilipino, na Vanuatu. Anasema hivi: “Kwa kuwa wavuvi huwa bandarini kwa muda mfupi tu, tunaanzisha funzo la Biblia papo hapo. Ili niwafikie wote, mara nyingi ninajifunza na watu wanne au watano  wakati uleule.” Na amefanya maendeleo gani katika kujifunza Kichina? Anasema hivi: “Laiti ningeweza kujifunza haraka, lakini ninakumbuka maneno haya niliyoambiwa na ndugu fulani, ‘Jitahidi kadiri unavyoweza, na Yehova atakusaidia katika mambo mengine yote.’”

Megan

MAISHA SALAMA, RAHISI, NA YENYE KUSISIMUA

Kabla Cathy hajahamia nchi nyingine kutoka Uingereza, alifanya utafiti ili kujua eneo ambalo lingekuwa salama kwa dada mseja. Alimjulisha Yehova hangaiko lake kupitia sala na kisha akaandikia ofisi kadhaa za tawi barua ili kujua hatari ambazo dada waseja wanaweza kukabili katika nchi hizo. Baadaye, alichanganua kwa makini majibu ya barua zake na kuamua kwamba Taiwan ingemfaa.

Katika mwaka wa 2004, akiwa na umri wa miaka 31, Cathy alihamia Taiwan, ambako anaishi maisha rahisi kabisa. Anasema hivi: “Niliwauliza ndugu na dada mahali bora pa kununua matunda na mboga kwa bei nafuu. Ushauri wao mzuri ulinisaidia kutumia akiba yangu ya pesa kwa muda mrefu zaidi.” Ni nini kinachomsaidia kuendelea kuishi maisha rahisi? Cathy anasema hivi: “Mara nyingi mimi husali kwa Yehova ili anisaidie kuridhika na chakula na mavazi ya kawaida tu. Ninahisi kwamba Yehova anajibu sala zangu kwa kunisaidia kutambua mahitaji yangu ya lazima na kutotamani vitu ambavyo si vya lazima.” Anaongezea hivi: “Ninafurahia kuishi maisha rahisi kwa sababu yananisaidia kukazia fikira mambo ya kiroho.”

Cathy

Ingawa maisha ya Cathy ni rahisi, yanasisimua. Anaeleza ni kwa nini yanasisimua: “Ninahubiri katika eneo ambalo watu wengi wanasikiliza habari njema. Hilo huniletea shangwe kwelikweli!” Alipofika Taiwan, kulikuwa na makutaniko mawili ya Kichina katika jiji alikotumika akiwa painia, lakini sasa kuna makutaniko saba. Cathy anasema hivi: “Kujionea ongezeko hilo kubwa ajabu na kushiriki katika mavuno hayo hunifanya nisisimke sana kila siku!”

“HATA MIMI NILIHITAJIKA!”

Choong Keon na Julie waliotajwa mwanzoni wanaendeleaje? Mwanzoni, Choong Keon alihisi kwamba hakulisaidia sana kutaniko kwa sababu hakujua vizuri Kichina. Lakini ndugu wenyeji hawakuhisi hivyo. Choong Keon anasema hivi: “Kutaniko letu lilipogawanywa na kuwa makutaniko mawili, nilipewa mapendeleo mengi zaidi nikiwa mtumishi wa huduma. Wakati huo, nilihisi kwa kweli kwamba nilikuwa nikitumika kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi.” Anasema hivi huku akitabasamu: “Nilifurahi sana kwamba hata mimi nilihitajika!” Sasa anatumika akiwa mzee wa kutaniko. Julie anaongezea hivi: “Tunahisi tunatimiza jambo muhimu, tumeridhika na kupata furaha kuliko wakati mwingine wowote. Tulikuja hapa kusaidia, lakini tunahisi kwamba mambo hayo yenye kusisimua yametusaidia sisi. Tunamshukuru Yehova kwa kuturuhusu tutumike hapa!”

Nchi nyingi bado zinahitaji wafanyakazi zaidi katika mavuno ya kiroho. Je, unamalizia masomo yako shuleni na unafikiria jinsi utakavyotumia maisha yako? Je, wewe ni mseja na unatamani kutumiwa zaidi na tengenezo la Yehova? Je, ungependa kuipatia familia yako urithi wa kiroho wenye thamani? Je, umestaafu, na una uzoefu mwingi wenye thamani unaoweza kushiriki na wengine? Uwe na hakika kwamba unaweza kupata baraka tele ukiamua kupanua huduma yako kwa kutumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme.