Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Unaweza Kuamini Vitabu vya Injili vya Biblia?

Kwa Nini Unaweza Kuamini Vitabu vya Injili vya Biblia?

“Vimefanikiwa sana. Sinema zinazogharimu mamilioni ya pesa zimetayarishwa . . . na vitabu vinavyonunuliwa kwa wingi vimeandikwa kwa kutegemea vitabu hivyo vya Injili . . . madhehebu ya Kikristo yamekubali vitabu hivyo. Dini nyingi na mawazo mengi ya uwongo yameanzishwa kwa msingi wa vitabu hivyo vya Injili.”—SUPER INTERESSANTE, GAZETI LA BRAZILI.

NI NINI kilichochochea msisimuko huo wote? Gazeti hilo lilikuwa likizungumza kuhusu ongezeko la hivi karibuni la watu wanaopendezwa na kujishughulisha na vitabu vya uwongo vya injili, barua, na maandishi mengine ya uwongo yaliyogunduliwa katikati ya karne ya 20 huko Nag Hammadi na maeneo mengine ya Misri. Kwa ujumla, maandishi hayo na mengine ya aina hiyo yameitwa maandishi ya Kignosti au ya Kiapokrifa. *

Je, Kulikuwa na Mpango wa Siri?

Katika nyakati ambazo kwa ujumla watu hawaamini Biblia na dini kuu za kiothodoksi, inaonekana kwamba maandishi ya Kignosti au ya Kiapokrifa yamewavutia wengi. Maandishi hayo yamebadili sana maoni ya wengi kuhusu mafundisho ya Yesu Kristo na Ukristo wenyewe. Kama gazeti moja lilivyosema: “Injili ya Tomasi na [vitabu vingine vya] kiapokrifa vinagusa mioyo ya watu wengi zaidi leo: watu ambao wana njaa ya kujua mambo ya kiroho lakini hawaamini dini.” Imekadiriwa kwamba katika nchi ya Brazili peke yake “kuna angalau vikundi 30 ambavyo imani yao inategemea vitabu vya Apokrifa.”

Kugunduliwa kwa maandishi hayo kumeeneza maoni ya kwamba katika karne ya nne W.K., Kanisa Katoliki lilifanya mpango wa siri wa kuficha ukweli kumhusu Yesu, na kwamba masimulizi fulani ya maisha yake yaliyokuwa katika maandishi ya Kiapokrifa yalifichwa, na kwamba vile vitabu vinne vya Injili ambavyo viko katika Biblia za leo vilibadilishwa. Elaine Pagels, profesa wa dini, alisema hivi: “Sasa tumeanza kuona kwamba ule ambao tunauita Ukristo na desturi ya Kikristo, kwa kweli ni sehemu ndogo sana iliyochaguliwa kutoka katika vyanzo fulani vichache kati ya vyanzo vingine vingi.”

Kulingana na maoni ya wasomi kama Pagels, Biblia si chanzo pekee cha imani ya Kikristo; kuna vyanzo vingine, kama vile maandishi ya Kiapokrifa. Kwa mfano, kipindi kimoja katika stesheni ya BBC kinachoitwa Mafumbo ya Biblia, kilichozungumza kuhusu “Maria Magdalene wa Kweli,” kilisema kwamba maandishi ya Kiapokrifa yanafundisha kwamba Maria Magdalene alikuwa “mwalimu na kiongozi wa kiroho wa wanafunzi wengine. Yeye si mwanafunzi tu; yeye ni mtume aliyetumwa kwa mitume.” Akitoa maelezo kuhusu daraka hilo la Maria Magdalene, Juan Arias, anaandika hivi katika gazeti O Estado de S. Paulo la Brazili: “Leo tuna kila sababu ya kuamini kwamba kikundi cha kwanza cha Kikristo, kilichoanzishwa na Yesu, kilisimamiwa kabisa na ‘wanawake,’ kwa kuwa makanisa ya kwanza yalikuwa katika nyumba za wanawake, ambamo walitumika wakiwa makasisi na maaskofu.”

Watu wengi wanaona kwamba maandishi ya Kiapokrifa yana uzito zaidi kuliko Biblia. Hata hivyo, maoni hayo yanatokeza maswali fulani ya maana: Je, maandishi ya Kiapokrifa ni msingi unaofaa wa imani ya Kikristo? Maoni hayo yanapopinga mafundisho yaliyo wazi ya Biblia, tunapaswa kuamini nini, Biblia au vitabu vya Apokrifa? Je, kweli kulikuwa na mpango wa siri katika karne ya nne wa kuficha vitabu hivyo na kubadili vile vitabu vinne vya Injili ili kuondoa habari ya maana kumhusu Yesu, Maria Magdalene, na wengine? Ili tupate majibu kwa maswali hayo, acheni tuchunguze Injili moja kati ya zile Injili nne za Biblia, Injili ya Yohana.

Uthibitisho Kutoka Katika Injili ya Yohana

Kipande cha maana sana cha kitabu cha Injili ya Yohana kilipatikana huko Misri mwanzoni mwa karne ya 20 na sasa kinaitwa Papyrus Rylands 457 (P52). Kipande hicho kina kitabu cha Yohana 18:31-33, 37, 38 ambacho kinapatikana katika Biblia za leo na kimewekwa katika Maktaba ya John Rylands, huko Manchester, Uingereza. Hicho ndicho kipande cha zamani zaidi kilichopo cha hati ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Wasomi wengi wanaamini kwamba kiliandikwa karibu mwaka wa 125 W.K., robo karne hivi baada ya kifo cha Yohana. Jambo la kushangaza ni kwamba maandishi ya kipande hicho yanalingana sana na maandishi ya hati za baadaye. Uhakika wa kwamba nakala ya zamani sana ya Injili ya Yohana ilikuwa tayari imefika nchini Misri, ambako kipande hicho kilipatikana, unaunga mkono maoni ya kwamba habari njema kulingana na Yohana kwa kweli iliandikwa na Yohana mwenyewe katika karne ya kwanza W.K., kama Biblia inavyoonyesha. Kwa hiyo, kitabu cha Yohana kiliandikwa na mtu aliyejionea matukio hayo.

Kwa upande mwingine, maandishi yote ya Kiapokrifa yaliandikwa katika karne ya pili na kuendelea, miaka 100 au zaidi baada ya mambo yaliyomo kutukia. Wataalamu fulani wanadai kwamba maandishi ya Kiapokrifa yanategemea maandishi au mapokeo ya zamani, lakini hakuna uthibitisho wa jambo hilo. Kwa hiyo, swali hili linafaa, Ungeamini nini, ushahidi wa watu waliojionea matukio hayo au wa watu walioishi miaka 100 baadaye? Jibu ni wazi. *

Hati ya Papyrus Rylands 457 (P52), kipande cha Injili ya Yohana cha karne ya pili W.K., kiliandikwa miaka michache tu baada ya maandishi ya awali ya Injili hiyo

Namna gani dai la kwamba vitabu vya Injili vya Biblia vilibadilishwa ili kuficha masimulizi fulani ya maisha ya Yesu? Kwa mfano, je, kuna uthibitisho wowote kwamba Injili ya Yohana ilibadilishwa katika karne ya nne ili kupotosha ukweli? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kukumbuka kwamba chanzo kimoja kikuu cha Biblia ya leo ni hati ya karne ya nne inayoitwa Vatican 1209. Ikiwa Biblia yetu ina mabadiliko yaliyofanywa katika karne ya nne, basi mabadiliko hayo yangekuwa katika hati hiyo. Jambo la kufurahisha ni kwamba hati nyingine ambayo ina sehemu kubwa ya kitabu cha Luka na Yohana, inayoitwa Bodmer 14, 15 (P75), iliandikwa kati ya mwaka wa 175 W.K. na 225 W.K. Wataalamu wanasema kwamba maandishi yake yanalingana sana na yale ya Vatican 1209. Yaani, hakuna mabadiliko makubwa yaliyofanywa katika vitabu vya Injili vya Biblia, na hati ya Vatican 1209 inathibitisha hilo.

Hakuna uthibitisho wowote, katika maandishi au wa aina nyingine, ambao unaonyesha kwamba maandishi ya kitabu cha Yohana au vile vitabu vingine vya Injili yalibadilishwa katika karne ya nne. Baada ya kuchunguza vipande mbalimbali vya hati vilivyogunduliwa huko Oxyrhynchus, Misri, Dakt. Peter M. Head, wa Chuo Kikuu cha Cambridge, anaandika hivi: “Kwa ujumla, hati hizo zinathibitisha kwamba hati maarufu [zilizoandikwa kwa herufi kubwa katika karne ya nne na kuendelea] ambazo ni msingi wa tafsiri muhimu za kisasa ni sahihi. Hakuna kitu chochote katika hati hizo kinachohitaji uelewaji mpya kabisa wa maandishi ya awali ya Agano Jipya.”

Tunaweza Kukata Kauli Gani?

Vitabu vinne vinavyokubaliwa vya Injili, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, vilikubaliwa na Wakristo ulimwenguni pote zamani kuanzia angalau katikati ya karne ya pili. Kitabu cha Tatiani cha Diatessaron (neno la Kigiriki linalomaanisha “kupitia [vile] vitabu vinne”), kilichoandikwa kati ya mwaka wa 160 na 175 W.K., kilitegemea tu vile vitabu vinne vya Injili vilivyokubaliwa na hakikutegemea kamwe zile “injili” za Kignosti. (Ona sanduku  “Vitabu vya Injili Vilitetewa Zamani.”) Pia, maelezo ya Irenaeus katika karne ya pili W.K. yanafurahisha. Alikazia kwamba ni lazima kuwe na Injili nne, kama vile ulimwengu ulivyo na sehemu nne na pande nne ambako upepo unavuma. Ingawa ulinganisho wake unaweza kutiliwa shaka, jambo hilo linaunga mkono wazo la kwamba wakati huo kulikuwa na Injili nne tu zilizokubaliwa.

Mambo hayo yote ya kweli yanaonyesha nini? Yanaonyesha kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambayo tunayo leo, kutia ndani vile vitabu vinne vya Injili, hayakubadilika sana kuanzia karne ya pili na kuendelea. Hakuna sababu nzuri ya kuamini kwamba katika karne ya nne kulikuwa na mpango wa siri wa kubadili au kuficha sehemu yoyote ya Maandiko ambayo yameongozwa na roho ya Mungu. Kinyume chake, msomi wa Biblia Bruce Metzger aliandika hivi: “Kufikia mwishoni mwa karne ya pili, . . . makutaniko mbalimbali ya waamini yaliyoenea kotekote huko Mediterania na pia kuanzia Uingereza mpaka Mesopotamia yalikubali kabisa sehemu kubwa ya Agano Jipya.”

Mtume Paulo na mtume Petro walitetea kweli ya Neno la Mungu. Wote wawili waliwaonya vikali Wakristo wenzao wasikubali au kuamini jambo lingine lolote isipokuwa mambo waliyofundishwa. Kwa mfano, Paulo alimwandikia hivi Timotheo: “Ee Timotheo, linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu na kutoka kwenye maneno yanayopingana ya ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’ Kwa maana kwa kujisifia ujuzi wa namna hiyo wengine wamegeuka kutoka kwenye imani.” Petro alitoa ushahidi ufuatao: “Sivyo, haikuwa kwa kufuata hadithi za uwongo zilizotungwa kwa ufundi kwamba tuliwafahamisha ninyi juu ya nguvu na kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo, lakini ilikuwa kwa sisi kuwa mashahidi wa kujionea fahari yake.”—1 Timotheo 6:20, 21; 2 Petro 1:16.

Karne nyingi zilizopita, nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu kusema hivi: “Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.” (Isaya 40:8) Tunaweza pia kuwa na hakika kwamba Yule aliyeongoza kuandikwa kwa Maandiko Matakatifu aliyalinda pia katika miaka yote hiyo ili “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.

^ fu. 3 Neno “Kignosti” linatokana na neno la Kigiriki ambalo linaweza kumaanisha “ujuzi wa kisiri” na neno “Apokrifa” linaloweza kumaanisha “habari iliyofichwa kwa uangalifu.” Maneno hayo yanatumiwa kuhusu maandishi ya uwongo au yasiyokubaliwa ambayo yanajaribu kuiga vitabu vya Injili, Matendo, barua, na mafunuo katika vitabu vinavyokubaliwa vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

^ fu. 11 Tatizo lingine kuhusu maandishi ya Kiapokrifa ni kwamba nakala zilizobaki ni chache sana. Injili ya Maria Magdalene iliyotajwa mwanzoni mwa habari hii inapatikana katika vipande viwili tu vidogo na kipande kikubwa zaidi hakina nusu ya maandishi yaliyoandikwa kwanza. Kwa kuongezea, kuna tofauti kubwa katika hati zilizopo.