Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya Kwanza

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya Kwanza

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?​—Sehemu ya Kwanza

Kwa Nini Ni Muhimu Tujue Jambo Hilo?; Uthibitisho Unaonyesha Nini?

Hii ni makala ya kwanza kati ya makala mbili katika matoleo mawili yanayofuatana ya Mnara wa Mlinzi ambayo yanazungumzia maswali ya wasomi kuhusu mwaka wa kuharibiwa kwa jiji la kale la Yerusalemu. Sehemu hizi mbili zinazofuatana zinazungumzia majibu ya maswali ambayo yamewatatanisha wasomaji fulani. Majibu hayo yaliyofanyiwa utafiti kikamili yanategemea Biblia.

“Wanahistoria na waakiolojia wengi wanasema kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 586 au 587 K.W.K. * Basi, kwa nini Mashahidi wa Yehova wanasema kwamba jiji hilo liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K.? Mnategemea nini ili kupata mwaka huo?”

NDIVYO alivyouliza mmoja wa wasomaji wetu. Lakini kwa nini tupendezwe kujua mwaka hususa ambao Mfalme wa Babiloni, Nebukadneza wa Pili, aliharibu jiji la Yerusalemu? Kwanza, ni kwa sababu tukio hilo lilikuwa mwanzo wa kipindi muhimu cha mabadiliko katika historia ya watu wa Mungu. Mwanahistoria mmoja alisema kuwa tukio hilo lilisababisha “msiba mkubwa, ndiyo, msiba usio na kifani.” Hekalu lililokuwa kitovu cha ibada ya Mungu Mweza-Yote kwa zaidi ya miaka 400 liliharibiwa mwaka huo. Mtunga-zaburi fulani wa Biblia aliomboleza hivi: ‘Ee Mungu, wamelitia unajisi hekalu lako takatifu, na kufanya mji wa Yerusalemu kuwa magofu.’—Zaburi 79:1, Biblia Habari Njema. *

Sababu ya pili ni kwamba kujua mwaka hususa ambapo ‘msiba huo usio na kifani’ ulianza na kuelewa jinsi kurudishwa kwa ibada safi jijini Yerusalemu kulivyotimiza kikamili unabii wa Biblia, kutafanya uwe na uhakika kwamba Neno la Mungu linategemeka. Kwa hiyo, kwa nini Mashahidi wa Yehova wanashikilia mwaka ambao unatofautiana kwa miaka 20 na mwaka ambao unakubaliwa na wengi? Kwa ufupi, ni kwa sababu ya uthibitisho ulio katika Biblia.

“Miaka Sabini” kwa Ajili ya Nani?

Miaka mingi kabla ya uharibifu huo, nabii Myahudi Yeremia alitoa dokezo muhimu kuhusu mfuatano wa matukio unaotajwa katika Biblia. Aliwaonya “wakazi wa Yerusalemu,” akisema: “Nchi hii yote itakuwa magofu matupu na ukiwa, na mataifa ya jirani yatamtumikia mfalme wa Babuloni kwa muda wa miaka sabini.” (Yeremia 25:1, 2, 11, BHN) Baadaye, nabii huyo aliongeza: “Yehova amesema hivi, ‘Kupatana na kutimia kwa miaka 70 katika Babiloni nitawakazia ninyi fikira, nami nitawatimizia neno langu jema kwa kuwarudisha tena mahali hapa.’” (Yeremia 29:10) Hiyo “miaka sabini” inamaanisha nini? Na kipindi hicho cha wakati kinatusaidia jinsi gani kujua mwaka wa kuharibiwa kwa Yerusalemu?

Badala ya kusema miaka 70 “katika Babiloni” tafsiri nyingi zinasema “kwa ajili ya Babiloni.” (New International Version) Kwa hiyo, wanahistoria fulani wanadai kwamba kipindi hicho cha miaka 70 kinahusu Milki ya Babiloni. Kulingana na mfuatano wa matukio katika vitabu vya kihistoria, Wababiloni walitawala nchi ya kale ya Yuda na Yerusalemu kwa miaka 70 hivi, kuanzia karibu 609 K.W.K. mpaka 539 K.W.K., wakati jiji kuu la Babiloni lilipotekwa.

Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba ile miaka 70 ilipaswa kuwa kipindi cha adhabu kali kutoka kwa Mungu, adhabu ambayo hasa ilielekezwa kwa watu wa Yuda na Yerusalemu, ambao walikuwa wamefanya agano la kumtii. (Kutoka 19:3-6) Walipokataa kuacha njia zao mbaya, Mungu alisema hivi: “Nami nitatuma Nebukadreza, mfalme wa Babeli, . . . juu ya nchi hii, na juu ya wakaao ndani yake, na juu ya mataifa haya yote yaliyopo pande zote.” (Yeremia 25:4, 5, 8, 9, Union Version) Ingawa mataifa yaliyokuwa karibu yangeshambuliwa na Babiloni, uharibifu wa Yerusalemu na ule uhamisho wa miaka 70 ambao ungefuata uliitwa na Yeremia ‘adhabu ya watu wangu,’ kwa kuwa Yerusalemu lilifanya “dhambi mbaya.”—Maombolezo 1:8; 3:42; 4:6, BHN.

Kwa hiyo, kulingana na Biblia, ile miaka 70 ilikuwa kipindi cha adhabu kali kwa Yuda, na Mungu aliwatumia Wababiloni kuwaadhibu vikali. Hata hivyo, Mungu aliwaambia Wayahudi: ‘Baada ya miaka sabini, nitawarudisha mahali hapa,’ yaani, katika nchi ya Yuda na Yerusalemu.—Yeremia 29:10, BHN.

Ile “Miaka Sabini” Ilianza Wakati Gani?

Ezra, mwanahistoria aliyeongozwa na roho ya Mungu, ambaye aliishi baada ya ile miaka 70 ya unabii wa Yeremia kutimizwa aliandika hivi kumhusu Mfalme Nebukadneza: “Wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikia yeye na wanawe hata kulipoingia milki ya Uajemi; ili kulitimiza neno la BWANA kwa kinywa cha Yeremia, hata nchi itakapofurahia sabato zake; kwa maana siku zote ilipokaa ukiwa ilishika sabato, kutimiza miaka sabini.”—2 Nyakati 36:20, 21, UV.

Hivyo, ile miaka 70 ingekuwa kipindi ambacho Yerusalemu na nchi ya Yuda ingefurahia “sabato zake.” Hilo lilimaanisha kwamba nchi hiyo haingelimwa, haingepandwa mbegu, wala matawi katika mashamba yake ya mizabibu kupunguzwa. (Mambo ya Walawi 25:1-5) Kwa sababu ya kutotii kwa watu wa Mungu, ambao huenda dhambi zao zilitia ndani kukosa kushika miaka yote ya Sabato, adhabu ilikuwa kwamba nchi yao ikae ukiwa na bila kulimwa kwa miaka 70.—Mambo ya Walawi 26:27, 32-35, 42, 43.

Nchi ya Yuda iliachwa ukiwa na bila kulimwa wakati gani? Wababiloni wakiongozwa na Nebukadneza walishambulia jiji la Yerusalemu mara ya kwanza, kisha baada ya miaka kumi hivi, wakalishambulia tena. Ile miaka 70 ilianza wakati gani? Bila shaka, haikuanza wakati Nebukadneza alipozingira Yerusalemu mara ya kwanza. Kwa nini? Ingawa wakati huo Nebukadneza alichukua mateka wengi kutoka Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni, bado aliacha watu wengine katika nchi. Pia, hakuliharibu Yerusalemu wakati huo. Kwa miaka iliyofuata baada ya uhamisho huo wa kwanza, wale waliobaki Yuda, yaani, “watu wa tabaka ya chini,” waliendelea kulima nchi yao. (2 Wafalme 24:8-17) Lakini mambo yakabadilika haraka.

Maasi ya Wayahudi yalifanya Wababiloni warudi Yerusalemu. (2 Wafalme 24:20; 25:8-10) Waliharibu jiji, kutia ndani hekalu lake takatifu, na wakawapeleka wakaaji wengi wa jiji hilo utekwani huko Babiloni. Katika kipindi cha miezi miwili, “Waisraeli wote [waliokuwa wamebaki katika nchi hiyo], wadogo na wakubwa pamoja na maofisa wa majeshi, waliondoka, wakaenda Misri, kwa sababu waliogopa Wakaldayo.” (2 Wafalme 25:25, 26, BHN) Hivyo, mwaka huo, katika mwezi wa saba wa Wayahudi, Tishri (Septemba/Oktoba), ndipo ingeweza kusemwa kwamba nchi hiyo, ambayo ilikuwa imeachwa ukiwa na bila kulimwa, ilianza kushika Sabato. Kupitia Yeremia, Mungu aliwaambia hivi Wayahudi waliokimbilia Misri: “Mmeona mabaya yote niliyoleta juu ya Yerusalemu, na juu ya miji yote ya Yuda; na, tazama, ni ukiwa leo, wala hapana mtu akaaye ndani yake.” (Yeremia 44:1, 2, UV) Basi, inaonekana kwamba tukio hilo ndilo lililokuwa mwanzo wa ile miaka 70. Tukio hilo lilitokea mwaka gani? Ili tupate jibu, tunahitaji kujua kipindi hicho kiliisha wakati gani.

Ile “Miaka Sabini” Iliisha Wakati Gani?

Nabii Danieli, ambaye aliishi mpaka ‘ufalme wa Uajemi ulipoanza kutawala,’ alikuwa huko Babiloni na alifanya hesabu kuhusu wakati ambapo ile miaka 70 ingekwisha. Aliandika hivi: “Mimi, Danieli, kwa kuvisoma vitabu, nilifahamu hesabu ya miaka, ambayo neno la BWANA lilimjia Yeremia nabii, ya kuutimiza ukiwa wa Yerusalemu, yaani, miaka sabini.”—Danieli 9:1, 2, UV.

Ezra alitafakari kuhusu unabii mbalimbali wa Yeremia na akahusianisha mwisho wa ‘ile miaka sabini’ na wakati ambapo ‘BWANA alichochea moyo wa Koreshi mfalme wa Uajemi atoe mwito.’ (2 Nyakati 36:21, 22, NIV) Wayahudi waliachiliwa huru mwaka gani? Agizo la kuwaachilia huru kutoka uhamishoni lilitolewa katika “mwaka wa kwanza wa Koreshi mfalme wa Uajemi.” (Ona sanduku  “Mwaka Muhimu Katika Historia.”) Hivyo, mwezi wa Oktoba mwaka wa 537 K.W.K., tayari Wayahudi walikuwa wamerudi Yerusalemu ili kurudisha ibada ya kweli.—Ezra 1:1-5; 2:1; 3:1-5.

Hivyo, kulingana na mfuatano wa matukio katika Biblia, ile miaka 70 ilikwisha mwaka wa 537 K.W.K. Tukihesabu miaka 70 kurudi nyuma, kipindi hicho kilianza mwaka wa 607 K.W.K.

Lakini ikiwa uthibitisho kutoka katika Maandiko unaonyesha waziwazi kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., kwa nini wanahistoria wengi wanashikilia mwaka wa 587 K.W.K.? Wanategemea vyanzo viwili vya habari—maandishi ya wanahistoria wa kale na orodha ya Ptolemy. Je, vyanzo hivyo vinategemeka zaidi kuliko Maandiko? Acheni tuone.

Je, Maandishi ya Wanahistoria wa Kale Ni Sahihi?

Wanahistoria walioishi karibu na wakati ambapo jiji la Yerusalemu liliharibiwa wanatoa habari zinazotofautiana kuhusu wafalme wa Milki Mpya ya Babiloni. * (Ona sanduku  “Wafalme wa Milki Mpya ya Babiloni.”) Mfuatano wao wa matukio haupatani na ule wa Biblia. Hata hivyo, maandishi yao yanategemeka kadiri gani?

Mbabiloni anayeitwa Berossus, ambaye alikuwa “kuhani wa Beli,” ni mmoja kati ya wanahistoria walioishi karibu na kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni. Kitabu chake kinachoitwa Babyloniaca, ambacho aliandika yapata mwaka wa 281 K.W.K., kilipotea, na ni visehemu tu vya kitabu hicho ambavyo vimehifadhiwa katika maandishi ya wanahistoria wengine. Berossus alidai kwamba alitumia “vitabu ambavyo vilikuwa vimehifadhiwa kwa uangalifu sana huko Babiloni.”1 Je, maandishi yake yalikuwa sahihi? Fikiria mfano mmoja.

Berossus aliandika kwamba Mfalme Senakeribu wa Ashuru alitawala baada ya “ndugu [yake]”; na baada yake mwana wake [Esarhadoni akatawala kwa] miaka 8; kisha, Sammuges [Shamash-shuma-ukin] akatawala kwa miaka 21.” (Kitabu cha Tatu, 2.1, 4) Hata hivyo, hati za historia ya Babiloni zilizoandikwa muda mrefu kabla ya kipindi cha Berossus zinasema kwamba Senakeribu alitawala baada ya baba yake, Sargoni wa Pili, na si baada ya ndugu yake; Esarhadoni alitawala miaka 12, si miaka minane; naye Shamash-shuma-ukin akatawala miaka 20, si miaka 21. Ingawa msomi R. J. van der Spek, anakubali kwamba Berossus alichunguza maandishi ya mfuatano wa matukio ya Wababiloni, anaandika hivi: “Hilo halikumzuia kuongeza mambo yake na ufafanuzi wake.”2

Wasomi wengine wana maoni gani kumhusu Berossus? “Zamani Berossus alionwa kuwa mwanahistoria,” anasema S. M. Burstein, ambaye alifanya uchunguzi wa kina kuhusu maandishi ya Berossus. Hata hivyo, alimalizia kwa kusema hivi: “Kwa kuchunguza maandishi yake, tunaona kwamba yamepungukiwa kihistoria. Hata sasa, visehemu vya Babyloniaca vina makosa mengi kuhusu mambo rahisi ya hakika . . . Mwanahistoria hapaswi kufanya makosa kama hayo, lakini kusudi la Berossus’ halikuwa kuandika habari za kihistoria.”3

Kutokana na hayo, una maoni gani? Je, hesabu za Berossus zinapaswa kuonwa kuwa sahihi na zenye kutegemeka? Namna gani wanahistoria wengine wa kale, ambao mara nyingi, waliandika mfuatano wa matukio ya kihistoria wakitegemea maandishi ya Berossus? Je, kweli maelezo yao yanaweza kutegemeka?

Orodha ya Ptolemy

Orodha ya Majina ya Wafalme iliyoandikwa na mtaalamu wa nyota wa karne ya pili W.K. Claudius Ptolemy, inatumiwa pia kuunga mkono mwaka wa 587 K.W.K. Orodha ya wafalme ya Ptolemy inaonwa kuwa msingi wa mfuatano wa matukio ya historia ya kale, kutia ndani kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni.

Ptolemy aliandika orodha yake miaka 600 hivi baada ya kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni kuisha. Basi, aliamua jinsi gani mwaka ambao mfalme wa kwanza kwenye orodha yake alianza kutawala? Ptolemy alieleza kwamba kwa kutumia hesabu za wataalamu wa nyota, ambazo kwa kadiri fulani zilitegemea kupatwa kwa mwezi, “tumehesabu kurudi nyuma mpaka mwanzo wa utawala wa Nabonassar,” mfalme wa kwanza kwenye orodha yake.4 Hivyo, Christopher Walker wa Jumba la Makumbusho la Uingereza anasema kwamba orodha ya Ptolemy ilikuwa “mbinu iliyokusudiwa kuwapa wataalamu wa nyota mfuatano mzuri wa matukio,” bali “si kuwapa wanahistoria rekodi sahihi kuhusu kuinuka na kufa kwa wafalme.”5

“Kwa muda mrefu, wataalamu wa nyota wameona Orodha hiyo kuwa yenye kutegemeka,” anaandika Leo Depuydt, mmoja kati ya wasomi wanaomtetea sana Ptolemy, “lakini hilo halimaanishi kwamba lazima Orodha hiyo iwe inategemeka kihistoria.” Profesa Depuydt anaongeza hivi kuhusu orodha hiyo ya wafalme: “Kuhusiana na watawala wa kale [ambao wanatia ndani wafalme wa Milki Mpya ya Babiloni], Orodha hiyo inahitaji kulinganishwa na maandishi ya kikabari ili kujua wakati ambao kila mfalme alitawala.”6

‘Maandishi hayo ya kikabari’ ambayo yanatusaidia kuchunguza usahihi wa orodha ya kihistoria ya Ptolemy ni nini? Yanatia ndani mfuatano wa matukio ya Wababiloni, orodha ya wafalme, na mambo ya kiuchumi—ambayo yaliandikwa na waandishi walioishi wakati wa Milki Mpya ya Babiloni, au karibu na wakati huo.7

Orodha ya Ptolemy inalingana jinsi gani na maandishi ya kikabari? Sanduku lenye kichwa  “Orodha ya Ptolemy Inatofautiana Jinsi Gani na Mabamba ya Kale?” (lililo hapa chini) linaonyesha sehemu ya orodha hiyo na kuilinganisha na hati nyingine za kale za maandishi ya kikabari. Ona kwamba Ptolemy anaorodhesha wafalme wanne tu katikati ya watawala wa Babiloni, Kandalanu na Nabonido. Hata hivyo Orodha ya Wafalme ya Uruk—ambayo ni sehemu ya maandishi ya kikabari—inaonyesha kwamba kulikuwa na wafalme saba katikati ya wafalme hao wawili wa Babiloni. Je, wafalme hao saba walitawala kwa vipindi vifupi visivyo na umaana wowote? Kulingana na maandishi ya kikabari kuhusu mambo ya kiuchumi, mmoja wao alitawala kwa miaka saba.8

Pia, kuna uthibitisho mkubwa kwenye hati za maandishi ya kikabari kwamba kabla ya utawala wa Nabopolasa (mfalme wa kwanza katika kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni), mfalme mwingine (Ashur-etel-ilani) alitawala milki ya Babiloni kwa miaka minne. Pia, kwa zaidi ya mwaka mmoja, hakukuwa na mfalme katika nchi hiyo.9 Hata hivyo, habari hizo zote hazipo katika orodha ya Ptolemy.

Kwa nini Ptolemy hakuorodhesha watawala fulani? Inaelekea kwamba hakuwaona kuwa watawala halali wa Babiloni.10 Kwa mfano, hakuorodhesha Labashi-Marduk, ambaye alikuwa mfalme katika Milki Mpya ya Babiloni. Lakini kulingana na maandishi ya kikabari, kwa kweli wafalme ambao hawakuorodheshwa na Ptolemy walitawala milki ya Babiloni.

Kwa ujumla, orodha ya Ptolemy inaonwa kuwa sahihi. Lakini kwa kufikiria habari ambazo haikutaja, je, inapaswa kutumiwa kama msingi hakika wa mfuatano wa matukio ya kihistoria?

Uamuzi Tunaofikia Kutokana na Uthibitisho Huo

Kwa ufupi: Biblia inasema waziwazi kwamba kulikuwa na miaka 70 ya uhamisho. Kuna uthibitisho mkubwa, na wasomi wengi wanakubaliana nao, kwamba Wayahudi waliopelekwa uhamishoni walikuwa wamerudi katika nchi yao kufikia mwaka 537 K.W.K. Tukihesabu kurudi nyuma kuanzia mwaka huo, tunaona kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Ingawa orodha ya Ptolemy na pia wanahistoria wa kale wanapinga mwaka huo, maswali yanayofaa yanaweza kuzushwa kuhusu usahihi wa maandishi yao. Kwa kweli, vyanzo hivyo viwili vya uthibitisho haviwezi kutoa ushahidi wa kutosha kupinga mfuatano wa matukio katika Biblia.

Hata hivyo, bado kuna maswali zaidi. Je, ni kweli kwamba hakuna uthibitisho wa kihistoria unaounga mkono mwaka ambao unategemea Biblia, yaani, 607 K.W.K.? Ni uthibitisho gani unaotolewa na hati za maandishi ya kikabari, ambazo ziliandikwa na watu walioishi zamani, na ambao walijionea mambo yaliyotukia? Tutazungumzia maswali hayo katika makala yetu itakayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Miaka yote miwili inatajwa katika vitabu vya kihistoria. Hata hivyo, ili iwe rahisi, tutatumia mwaka wa 587 K.W.K. katika makala hii na makala itakayofuata. Herufi K.W.K. zinamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.”

^ fu. 5 Mashahidi wa Yehova wanachapisha tafsiri inayotegemeka ya Biblia ambayo inaitwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo, ikiwa wewe si mmoja wa Mashahidi wa Yehova, unaweza kuamua kutumia tafsiri nyingine unapochunguza habari za Biblia. Makala hii inanukuu tafsiri nyingi za Biblia ambazo zinakubaliwa na wengi.

^ fu. 23 Milki Mpya ya Babiloni ilianza na utawala wa Nabopolasa, baba ya Nebukadneza, na ikaisha wakati wa utawala wa Nabonido. Kipindi hicho cha wakati kinawavutia wasomi kwa sababu kinatia ndani sehemu kubwa ya ile miaka 70 ya ukiwa.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 28]

 MWAKA MUHIMU KATIKA HISTORIA

Ili kupata mwaka wa 539 K.W.K., mwaka ambao Koreshi wa Pili alishinda Babiloni, tunafanya hesabu kwa kutumia:

Maandishi ya kale ya kihistoria na mabamba ya maandishi ya kikabari: Diodorus wa Sicily (m. 80-20 K.W.K.) aliandika kwamba Koreshi alianza kutawala Uajemi “mwanzoni mwa mwaka wa 55 wa michezo ya Olimpiki.” (Historical Library, Kitabu cha Tisa, 21) Huo ulikuwa mwaka wa 560 K.W.K. Mwanahistoria Mgiriki Herodoto (m. 485-425 K.W.K.) alisema kwamba Koreshi aliuawa “baada ya kutawala kwa miaka 29,” kumaanisha kwamba alikufa katika mwaka wa 30 wa utawala wake, yaani, mwaka wa 530 K.W.K. (Histories, Kitabu cha Kwanza, Clio, 214) na mabamba ya Maandishi ya Kikabari yanaonyesha Koreshi alitawala Babiloni kwa miaka tisa kabla ya kifo chake. Hivyo, tukihesabu miaka tisa kurudi nyuma kabla ya kifo chake mwaka wa 530 K.W.K. tunafika kwenye mwaka wa 539 K.W.K., ambapo Koreshi alishinda Babiloni.

Uthibitisho katika bamba lenye maandishi ya kikabari: Maandishi yaliyoandikwa na wataalamu wa nyota wa Babiloni kwenye bamba la udongo (BM 33066), yanathibitisha kwamba Koreshi alikufa mwaka wa 530 K.W.K. Ingawa bamba hilo lina makosa kadhaa kuhusu mpangilio wa nyota, sayari, na mwezi, lina maelezo kuhusu vipindi viwili vya kupatwa kwa mwezi ambavyo vilitukia katika mwaka wa saba wa Cambyses wa Pili, mwana wa Koreshi ambaye alitawala baada yake. Inaaminika kwamba vipindi hivyo viwili vya kupatwa kwa mwezi vilionekana huko Babiloni Julai 16, 523 K.W.K., na Januari 10, 522 K.W.K., jambo linaloonyesha kwamba majira ya kuchipuka ya mwaka wa 523 K.W.K. ndiyo yaliyokuwa mwanzo wa mwaka wa saba wa Cambyses. Hilo linamaanisha kwamba alianza kutawala mwaka wa 529 K.W.K. Kwa hiyo, mwaka wa mwisho wa Koreshi ulikuwa 530 K.W.K., hivyo, alianza kutawala Babiloni mwaka wa 539 K.W.K.

[Hisani]

Tablet: © The Trustees of the British Museum

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

MAELEZO MAFUPI

▪ Kwa kawaida wanahistoria wanasema kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K.

▪ Mfuatano wa matukio katika Biblia unaonyesha waziwazi kwamba uharibifu huo ulitokea mwaka wa 607 K.W.K.

▪ Mara nyingi wanahistoria hufikia maamuzi yao wakitegemea maandishi ya wanahistoria wa kale na orodha ya Ptolemy.

▪ Maandishi ya wanahistoria wa kale yana makosa mengi na mara nyingi hayapatani na rekodi kwenye mabamba ya udongo.

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

Marejeo

1. Babyloniaca (Chaldaeorum Historiae), Kitabu cha Kwanza, 1.1.

2. Kitabu Studies in Ancient Near Eastern World View and Society, ukurasa wa 295.

3. Kitabu The Babyloniaca of Berossus, ukurasa wa 8.

4. Kitabu Almagest, cha Tatu, 7, kilichotafsiriwa na G. J. Toomer, katika Ptolemy’s Almagest, kilichochapishwa mwaka wa 1998, ukurasa wa 166. Ptolemy alijua kwamba wataalamu wa nyota wa Babiloni walitumia mbinu fulani za “kuhesabu” wakati uliopita na wakati ambao ungefuata wa kupatwa kwa mwezi kwa sababu walitambua kwamba vipindi vinavyofanana vya kupatwa kwa mwezi vilitukia kila baada ya miaka 18.—Almagest, cha Nne, 2.

5. Kitabu Mesopotamia and Iran in the Persian Period, ukurasa wa 17-18.

6. Kitabu Journal of Cuneiform Studies, Buku la 47, 1995, ukurasa wa 106-107.

7. Maandishi ya kikabari yaliandikwa kwa kuweka alama mbalimbali kwenye bamba laini la udongo. Mwandishi aliandika kwa kifaa fulani kilichochongoka.

8. Sin-sharra-ishkun alitawala kwa miaka saba, na mabamba 57 ya udongo ya mfalme huyo yanayohusu mambo ya kiuchumi yalianza kuandikwa wakati alipoanza kutawala mpaka mwaka wa saba wa utawala wake. Ona kitabu Journal of Cuneiform Studies, Buku la 35, 1983, ukurasa wa 54-59.

9. Bamba la mambo ya kiuchumi C.B.M. 2152 liliandikwa mwaka wa nne wa utawala wa Ashur-etel-ilani. (Kitabu Legal and Commercial Transactions Dated in the Assyrian, Neo-Babylonian and Persian Periods—Chiefly From Nippur, cha A.T. Clay, 1908, ukurasa 74.) Pia, maandishi ya Harran Inscriptions of Nabonidus, (H1B), I, mstari wa 30, yanamworodhesha kabla ya Nabopolasa. (Anatolian Studies, Buku la Nane, mwaka wa 1958, ukurasa wa 35, 47.) Kwa habari kuhusu kipindi ambacho hakikuwa na mfalme, ona Chronicle 2, mstari wa 14, katika kitabu Assyrian and Babylonian Chronicles, ukurasa wa 87-88.

10. Wasomi fulani wanadai kwamba kuna wafalme ambao Ptolemy hakuwaorodhesha kwa sababu walikuwa na jina la cheo, “Mfalme wa Ashuru.” Wanasema aliorodhesha tu wafalme wa Babiloni. Hata hivyo, kama inavyoonyeshwa kwenye sanduku katika ukurasa wa 30, wafalme fulani walio katika orodha ya Ptolemy walikuwa pia na jina la cheo, “Mfalme wa Ashuru.” Mabamba yanayohusu mambo ya kiuchumi, barua za maandishi ya kikabari, na maandishi mengine yanaonyesha waziwazi kwamba wafalme Ashur-etel-ilani, Sin-shumu-lishir, na Sin-sharra-ishkun walitawala milki ya Babiloni.

[Chati/​Picha katika ukurasa wa 29]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

WAFALME WA MILKI MPYA YA BABILONI

Ikiwa wanahistoria hawa wanategemeka, kwa nini hawapatani?

Wafalme

Nabopolasa

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K.. (21)

POLYHISTOR 105-? K.W.K. (20)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (—)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (21)

Nebukadneza wa Pili

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K. (43)

POLYHISTOR 105-? K.W.K. (43)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (43)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (43)

Amel-Marduk

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K. (2)

 POLYHISTOR 105-? K.W.K. (12)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (18)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (2)

Neriglissar

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K. (4)

POLYHISTOR 105-? K.W.K. (4)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (40)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (4)

Labashi-Marduk

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K. (miezi 9)

POLYHISTOR 105-? K.W.K. (—)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (miezi 9)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (—)

Nabonido

BEROSSUS m. 350-270 K.W.K. (17)

POLYHISTOR 105-? K.W.K. (17)

JOSEPHUS 37-?100 W.K. (17)

PTOLEMY m. 100-170 W.K. (17)

(#) = Kipindi (cha miaka) ambacho wafalme walitawala kulingana na wanahistoria wa kale

[Hisani]

Photograph taken by courtesy of the British Museum

[Chati/​Picha katika ukurasa wa 30]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ORODHA YA PTOLEMY INATOFAUTIANA JINSI GANI NA MABAMBA YA KALE?

Ptolemy hataji wafalme fulani katika orodha yake. Kwa nini?

ORODHA YA PTOLEMY

Nabonassar

Nabu-nadin-zeri (Nadinu)

Mukin-zeri na Pul

Ululayu (Shalmanesa wa Tano) “Mfalme wa Ashuru”

Merodak-baladani

Sargoni wa Pili “Mfalme wa Ashuru”

Kipindi cha Kwanza Ambacho Hakikuwa na Mfalme

Shamash-shuma-ukin

Kandalanu

Nabopolasa

Nebukadneza

Amel-Marduk

Neriglissar

Nabonido

Koreshi

Cambyses

ORODHA YA WAFALME YA URUK INAYOPATIKANA KATIKA MABAMBA YA KALE

Kandalanu

Sin-shumu-lishir

Sin-sharra-ishkun

Nabopolasa

Nebukadneza

Amel-Marduk

Neriglissar

Labashi-Marduk

Nabonido

[Picha]

Mfuatano wa matukio ya Wababiloni ni sehemu ya maandishi ya kikabari ambayo yanatusaidia kuchunguza usahihi wa orodha ya Ptolemy

[Hisani]

Photograph taken by courtesy of the British Museum

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

Photograph taken by courtesy of the British Museum