Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Misiba ya Asili

Kukabiliana na Misiba ya Asili

Kwa kuwa misiba ya asili inatokea mara nyingi na kusababisha uharibifu mkubwa, mtu anaweza kufanya nini ili kukabiliana nayo? Acheni tuzungumzie hatua fulani ambazo mtu anaweza kuchukua.

Epuka maeneo hatari.

Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Shauri hilo la hekima linaweza kutumiwa kuhusiana na misiba. Onyo linapotolewa kuhusu mlima wa volkano unaokaribia kulipuka, mafuriko, au kimbunga kinachokuja, wale wanaoishi katika eneo linalokabili hatari wanapaswa kutenda kwa hekima kwa kuhamia maeneo yaliyo salama. Uhai ni wenye thamani kuliko nyumba au vitu vya kimwili.

Huenda inawezekana kwa watu fulani kuamua kwamba hawataishi katika eneo hatari. Ripoti fulani ya utafiti inasema: “Maeneo fulani yanakabili hatari kubwa zaidi ya kukumbwa na misiba. Ni sehemu ndogo sana ya Dunia ambayo ina maeneo hayo hatari na misiba mingi mikubwa ya wakati ujao itatokea katika maeneo hayo.” Kwa mfano, inaweza kuwa hivyo katika maeneo tambarare ya pwani au maeneo yanayokabili hatari ya matetemeko ya ardhi. Ikiwa unaweza kuepuka kuishi katika maeneo hayo au kuhamia eneo lililo salama zaidi, huenda ukapunguza sana hatari ya kupatwa na misiba.

Jitayarishe kwa ajili ya msiba.

Hata ingawa unaweza kuchukua hatua zote zinazohitajiwa, huenda bado ukapatwa na msiba usiotazamia. Unaweza kukabiliana kwa urahisi na msiba huo ikiwa umejitayarisha mapema. Hatua hiyo inapatana pia na shauri ambalo limetajwa kwenye Methali 22:3. Je, una mfuko wa dharura ulio na vitu vya kutumia wakati wa msiba? Kitabu kimoja (1-2-3 of Disaster Education) kinapendekeza kwamba mfuko huo uwe na vitu vifuatavyo: Vifaa vya huduma ya kwanza, chupa zilizo na maji, vyakula visivyoharibika upesi, na hati muhimu. Huenda pia ikawa jambo la hekima kuzungumzia pamoja na familia yako aina ya misiba ambayo inaweza kutokea na hatua mnazoweza kuchukua msiba ukitokea.

Dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

Hilo linaweza kukusaidia katika hali yoyote ile. Biblia inamwita Mungu “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” Andiko lingine linamfafanua kuwa Mungu “ambaye huwafariji wale walioshushwa chini.”—2 Wakorintho 1:3, 4; 7:6.

Ndiyo, Mungu anaelewa vizuri hali zinazowapata wote wanaomwamini. Ni Mungu mwenye upendo na anatutia moyo kwa njia mbalimbali. (1 Yohana 4:8) Tunaposali kwa Mungu ili tupate roho takatifu, bali si miujiza, roho hiyo inaweza kutusaidia katika hali yoyote ile. Roho takatifu inaweza kutukumbusha masimulizi ya Biblia ambayo yanaweza kutufariji na kututuliza tunapopatwa na misiba. Kwa kweli, watumishi waaminifu wa Mungu wanaweza kuhisi kama Daudi, mfalme wa Israeli la kale, aliyesema: “Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.”—Zaburi 23:4.

Tunaposali kwa Mungu ili tupate roho takatifu, bali si miujiza, roho hiyo inaweza kutusaidia katika hali yoyote ile

Wakristo husaidiana.

Katika karne ya kwanza nabii Mkristo aliyeitwa Agabo alisema kwamba “njaa kali ilikuwa karibu kuja juu ya dunia nzima inayokaliwa; ambayo, kama ilivyo, ilitukia wakati wa Klaudio.” Njaa hiyo iliwaathiri sana wanafunzi wengi wa Yesu huko Yudea. Wanafunzi waliokuwa katika maeneo mengine walifanya nini waliposikia kuhusu hali ngumu iliyowapata Wakristo wenzao? Simulizi linasema: “Wanafunzi wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.” (Matendo 11:28, 29) Kwa upendo, walitoa misaada ili kushughulikia hali hiyo.

Leo, misiba mibaya inapotokea, watumishi wa Mungu wanatenda kwa njia hiyohiyo. Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kuwasaidia waamini wenzao. Kwa mfano, tetemeko kubwa la ardhi lilipotokea huko Chile, mnamo Februari 27, 2010, Mashahidi wa Yehova walichukua hatua haraka ili kuwasaidia wale walioathiriwa. Karla, ambaye nyumba yake ilisombwa na tsunami, anaeleza: “Nilifarijiwa na kutiwa moyo kuona kwamba asubuhi iliyofuata [Mashahidi wenzetu] waliwasili kutoka maeneo mengine ili kutusaidia. Bila shaka, Yehova alitufariji kupitia wema tulioonyeshwa na wajitoleaji hao. Nilihisi kwamba ninapendwa na kulindwa.” Babu yake, ambaye si Shahidi, aliona msaada uliotolewa. Alisema: “Wametenda kwa njia tofauti kabisa na jinsi ambavyo nimeona kwa miaka mingi katika kanisa langu.” Jambo hilo lilimchochea kuwaomba Mashahidi wa Yehova wajifunze Biblia pamoja naye.

Wakristo husaidiana ili wakabiliane na madhara yanayosababishwa na misiba

Kushirikiana na watu wanaompenda Mungu kunaweza kutusaidia sana wakati wa taabu. Hata hivyo, je, kuna wakati ambapo watu hawatateseka tena duniani kwa sababu ya misiba? Acheni tuone Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo.