Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | BIBLIA INA UJUMBE GANI?

“Tumempata Masihi”!

“Tumempata Masihi”!

Miaka mia nne hivi baada ya kitabu cha mwisho cha maandiko ya Kiebrania katika Biblia kuandikwa, unabii wa Mika kumhusu Masihi ulitimia: Yesu alizaliwa katika mji wa Bethlehemu. Miaka 30 hivi baadaye, katika mwaka wa 29 W.K., sehemu ya kwanza ya unabii wa Danieli kuhusu Masihi aliyeahidiwa ilitimia. Yesu alibatizwa kisha Mungu akamtia mafuta kwa roho takatifu. Ule Uzao yaani Masihi aliyesubiriwa kwa muda mrefu, alifika kwa wakati barabara!

Mara moja Yesu alianza huduma yake “[aki]tangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Kama tu ilivyotabiriwa, Yesu alikuwa mwenye fadhili, mpole, na aliwajali watu kikweli. Aliwafundisha watu kwa sababu aliwapenda na mafundisho yake yaliwanufaisha. Pia, aliwaponya “kila namna ya udhaifu,” na hivyo akathibitisha Mungu alikuwa pamoja naye. (Mathayo 4:23) Watu wa kila umri walimwendea Yesu na kusema: “Tumempata Masihi”!Yohana 1:41.

Yesu alitabiri kwamba kabla Ufalme wake haujaanza kutawala dunia, kungetokea vita, matetemeko ya ardhi, na matatizo mengine mengi. Aliwasihi watu wote “[waendelee] kukesha.”Marko 13:37.

Yesu alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyemtii Mungu, lakini alikuwa na maadui ambao hatimaye walimuua. Kupitia kifo chake tunaweza kuwa na tumaini la kupata uzima wa milele ambao Adamu na Hawa walipoteza.

Kifo cha Yesu kilitimiza unabii. Pia, Mungu alitimiza unabii alipomfufua Yesu akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu siku tatu baadaye. Kisha Yesu akawatokea zaidi ya wanafunzi wake 500. Kabla hajarudi mbinguni, Yesu aliwaamuru wafuasi wake watangazie “watu wa mataifa yote” habari njema kumhusu yeye na Ufalme wake. (Mathayo 28:19) Walitangaza habari njema kwa kadiri gani?

Habari hii inategemea Mathayo, Marko, Luka, Yohana, 1 Wakorintho.