Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwanafunzi Akabili Uamuzi Mgumu

Mwanafunzi Akabili Uamuzi Mgumu

Peter ana wasiwasi mwingi. Mwalimu wake, mwanamke ambaye Peter anamheshimu, amemaliza tu kueleza jinsi Charles Darwin, kupitia nadharia ya mageuzi alivyofanya maendeleo katika uelewaji wa sayansi na kuwakomboa wanadamu kutoka katika imani za kishirikina. Sasa anawaomba wanafunzi wake watoe maoni yao kuhusu mada hiyo.

Peter anakabili uamuzi mgumu. Wazazi wake wamemfundisha kwamba Mungu aliumba dunia na vyote vilivyomo. Wanasema kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji ni yenye kutegemeka na kwamba mageuzi ni nadharia tu isiyo na uthibitisho. Mwalimu na wazazi wa Peter wanamtakia mema. Hata hivyo, Peter anapaswa kumwamini nani?

Kila mwaka, hali kama hizo hutokea katika shule nyingi ulimwenguni. Peter na wanafunzi wengine kama yeye wanapaswa kufanya nini? Je, hukubali kwamba wanapaswa kufanya utafiti na kujifanyia uamuzi wao wenyewe? Wanapaswa kuchunguza uthibitisho wa fundisho la mageuzi na fundisho la uumbaji, kisha wajiamulie kile watakachoamini.

Biblia huonya dhidi ya kuamini tu mambo ambayo watu wanafundisha. Mwandikaji mmoja wa Biblia anasema: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Biblia huwatia moyo Wakristo watumie ‘nguvu zao za kufikiri’ ili wajithibitishie wenyewe mambo wanayofundishwa.—Waroma 12:1, 2.

Habari zilizo katika broshua hii hazikusudiwi kuunga mkono jitihada za vikundi vya kidini vinavyotaka fundisho la uumbaji lifundishwe shuleni. Badala yake, broshua hii inachunguza madai yanayotolewa na wale wanaofundisha kwamba uhai ulijitokeza wenyewe na kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji ni hadithi tu.

Tutakazia fikira chembe kwa sababu hiyo ndiyo sehemu ya msingi ya uhai. Utaweza kuchanganua baadhi ya mambo yenye kustaajabisha kuhusu jinsi chembe zinavyofanyizwa. Pia utaombwa uchanganue dhana zinazounga mkono nadharia ya mageuzi.

Sote tunapaswa kufikiria swali hili, uhai ulitokana na Muumba au ulijitokeza wenyewe? Huenda tayari umefikiria jambo hilo kwa uzito. Broshua hii itatoa baadhi tu ya uthibitisho ambao umewafanya wengi waamini kwamba uhai ulitokana na Muumba.