Hamia kwenye habari

Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society Ni Nini?

Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society Ni Nini?

 Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania ni shirika lisilo la kibiashara lililoanzishwa mnamo 1884 chini ya sheria za Jumuiya ya Madola ya Pennsylvania, Marekani. Shirika hilo linatumiwa na Mashahidi wa Yehova kutegemeza kazi yao ya ulimwenguni pote, ambayo inatia ndani kuchapisha Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia.

 Kulingana na mkataba wake, malengo ya shirika hilo ni ya “kidini, kielimu, na ya kutoa msaada,” na hasa “kuhubiri na kufundisha injili ya Ufalme wa Mungu ulio chini ya Kristo Yesu.” Mtu yeyote anapewa mwaliko kuwa mshiriki wa shirika hilo haidhuru amechangia pesa kiasi gani. Washiriki na wasimamizi wa shirika hilo hulisaidia Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Mashirika Mengine ya Kisheria

 Mbali na Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, Mashahidi wa Yehova hutumia mashirika mengine mengi ya kisheria katika nchi mbalimbali. Majina ya baadhi ya mashirika hayo yana neno “Watch Tower,” “Watchtower,” au tafsiri ya maneno hayo.

 Mashirika hayo yametuwezesha kutimiza mambo mengi tangu yalipoanzishwa, kutia ndani:

  •   Uandikaji na Uchapishaji. Tumechapisha Biblia milioni 220 hivi na karibu machapisho bilioni 40 yenye ujumbe wa Biblia katika zaidi ya lugha 900. Tovuti ya jw.org inawawezesha watu kusoma Biblia kwenye mtandao bila malipo katika zaidi ya lugha 160 na wanaweza kupata majibu ya maswali ya Biblia kama vile, “Ufalme wa Mungu ni nini?

  •   Elimu. Tunaendesha shule mbalimbali za elimu ya Biblia. Kwa mfano, tangu 1943, zaidi ya Mashahidi 9,000 wa Yehova wameelimishwa katika Shule ya Gileadi, na hilo limewawezesha kutumika wakiwa wamishonari au kuimarisha kazi yetu ya ulimwenguni pote. Na kila juma, mamilioni ya watu, kutia ndani watu ambao si Mashahidi, wanaelimishwa katika mikutano inayofanywa katika kila kutaniko. Pia tunakuwa na madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika na tuna kitabu kinachowafunza watu kusoma na kuandika kilichotafsiriwa katika lugha 120.

  •   Msaada. Tumewapa msaada watu wanaokabili majanga​—iwe yamesababishwa na wanadamu, kama yale mauaji ya jamii nzima yaliyotukia nchini Rwanda katika mwaka wa 1994, au iwe ni misiba ya asili, kama lile tetemeko la nchi lililotukia nchini Haiti katika mwaka wa 2010.

 Ingawa mambo mengi yametimizwa kupitia kwa mashirika ya kisheria tunayotumia, kazi yetu haitegemei yoyote ya mashirika hayo. Kila Mkristo ana daraka la kutimiza kazi aliyopewa na Mungu ya kuhubiri na kufundisha habari njema. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Tunaamini kwamba Mungu anategemeza kazi yetu na kwamba ataendelea ‘kuikuza.’—1 Wakorintho 3:6, 7.