Hamia kwenye habari

Kukabiliana na Moto kwa Ustadi

Kukabiliana na Moto kwa Ustadi

“Moto! Moto!” Sandra alikuwa akila kiamsha-kinywa nyumbani kwa wakwe zake alipoona miale ya moto ikitokea chini ya kibanda kilichokuwa kando ya nyumba hiyo. Yeye na mume wake Thomas, walisimama na kuanza kushughulikia hali hiyo mara moja. Sandra alienda kuchukua kifaa cha kuzima moto huku Thomas akikimbia kwenye kibanda hicho kuchunguza hali ilivyokuwa. Sandra alifika upesi na kumpa Thomas kifaa hicho, naye akazima moto huo. Sandra anakumbuka hivi: “Ikiwa hatungetenda upesi kama tulivyofanya kibanda chote kingeteketea.”

Thomas na Sandra walifauluje kutenda kwa kasi hivyo na bila woga? Kwa sababu wao pamoja na wengine 1,000 hivi wanaofanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Selters, Ujerumani, wamefundishwa jinsi ya kukabiliana na moto unapotokea.

Ofisi hiyo ya Selters, iliyojengwa katika eneo lenye ukubwa wa ekari 70, ina ofisi, eneo la makazi, dobi, kiwanda cha uchapishaji, na karakana mbalimbali. Maeneo hayo yote yanatokeza changamoto za pekee kuhusiana na moto. Kwa sababu hiyo, Idara ya Usalama na Mazingira ya ofisi hiyo ilianzisha programu ya kuwafundisha watu kuhusu usalama wa moto. Kwanza, kikundi kinachoitwa Kikosi cha Kushughulikia Hali za Dharura kilifanya mazoezi pamoja na wazima-moto wa serikali. Pili, wajitoleaji wote katika ofisi ya tawi hufanya mambo yafuatayo kwa ukawaida:

  • Wanafanya mazoezi ya kuondoka upesi katika jengo wanaposikia king’ora cha moto.

  • Wanashiriki katika masomo ya kushughulikia moto kwa njia salama.

  • Wanajifunza jinsi ya kuzima moto kabla haujaenea.

Kwa njia hiyo, wajitoleaji hao hupata ustadi muhimu sana wa kutumia kunapokuwa na hali ya dharura.

Mazoezi ya Kuzima Moto kwa Njia Salama

Wakati wa vipindi vya mazoezi, wahusika hujifunza kuzima moto kwa njia salama. Christin, ambaye mara ya mwisho alijifunza kuhusu usalama wa moto ni wakati alipokuwa shule ya msingi, anasema hivi kuhusu vipindi hivyo vya mafunzo katika ofisi ya tawi: “Nilichukua kifaa cha kuzima moto, nikakifungua, na kukaribia moto kutokea upande ambao upepo unavuma. Ikiwa ningetoka upande ule mwingine, miale ingekuwa ikielekea usoni mwangu. Kisha nikauzima moto huo​—bila kusaidiwa na mtu! Pia nilijifunza jinsi ya kuzima moto nikiwa katika kikundi cha watu wanne au watano.”

Daniel anayefanya ofisi ya tawi akiwa mwalimu wa usalama wa moto, anasema kwamba vipindi vya mazoezi “hupunguza woga wa moto. Moto unapotokea, mara nyingi watu hushtuka. Wanapatwa na hofu na kuanza kujiuliza, ‘Sasa tutafanya nini? Tutatumiaje kifaa cha kuzima moto?’ Lakini wanapojua jambo la kufanya, wanaweza kwa urahisi kuzuia moto mdogo usiongezeke na kuwa mkubwa zaidi.” Anasema kwamba wakati wa mazoezi, “wahusika hujifunza ujuzi wa kushika kifaa cha kuzima moto kwa njia inayofaa kunapokuwa na dharura na jinsi ya kuuzima moto. Wanapata uhakika na ujasiri wa kutenda haraka inapohitajika.”

Mazoezi Yana Matokeo Mazuri

Wengi wameshukuru sana kwa mazoezi hayo. Christin, aliyetajwa mapema, anasema hivi: “Nilishika kifaa cha kuzima moto kwa mara ya kwanza maishani. Nafikiri kila mtu anapaswa kupata mazoezi haya.” Nadja, ambaye anajitolea kwa muda katika ofisi ya tawi na anafanya kazi pia katika uwanja wa ndege, anasema hivi: “Katika miaka kumi ambayo imepita, kwenye uwanja wa ndege nimefundishwa tu kwa mdomo kuhusu kukabiliana na moto. Lakini mazoezi halisi ambayo nimepata kwenye ofisi ya tawi yamenisaidia kuwa na uhakika zaidi. Moto ukitokea, sasa ninajua ninachopaswa kufanya.”

Sandra anaamini kwamba mazoezi aliyopata kwenye ofisi ya tawi yalimsaidia kutenda upesi alipokuwa nyumbani kwa wakwe zake. Anasema hivi: “Nimepunguza woga wa kutumia kifaa cha kuzima moto. Mazoezi hayo ya kila mwaka yanafaa sana. Yalinisaidia sana.”

Kufanya Mazoezi na Wazima-Moto wa Serikali

Wazima-moto hufanya mazoezi kwa ukawaida kwenye ofisi ya tawi. Theo Neckermann, msimamizi wa wazima-moto anaeleza sababu ya kufanya hivyo: “Idara yetu ya wazima-moto ndiyo inayosimamia manispaa ya Selters. Hili ni eneo la vijijini. Kwa kawaida sisi huzima moto katika nyumba za familia au katika nyumba zenye orofa. Majengo ya ofisi hii ya tawi ni ya pekee katika eneo hili kwa sababu ya eneo lake kubwa, majengo makubwa, na viwanda vilivyomo. Tunahitaji kuwa na ujuzi wa ziada kushughulikia hali za dharura katika majengo haya. Kwa hiyo, tunafurahi na kushukuru kwamba tunapata nafasi ya kufanyia mazoezi hapa.”

Washiriki zaidi ya 100 walio katika Kikosi cha Kushughulikia Hali ya Dharura cha ofisi ya tawi hufanya mazoezi ya kuokoa uhai na ya kuzima moto pamoja na wazima-moto hao wa serikali. Bw. Neckermann anasema hivi: “Tunathamini sana Kikosi chenu cha Kushughulikia Hali ya Dharura. Bila msaada na mwongozo wao, mazoezi ya kuzima moto na kushughulikia dharura nyingine zinazohusiana na moto hayangefanikiwa.”

Kuonyesha hatari ya kujaribu kuzima moto wa mafuta kwa kutumia maji

Ustadi wa wazima-moto hao pamoja na Kikosi cha Kushughulikia Hali ya Dharura ulijaribiwa jioni moja mnamo Februari 2014. Jengo moja kati ya majengo ya makazi ya ofisi ya tawi lilijawa na moshi. Daniel, aliyenukuliwa awali, anakumbuka hivi: “Moshi ulikuwa mwingi sana hivi kwamba hatungeweza kuona chochote. Mara moja tuliwataarifu wazima-moto na tukaanza kuwatoa wakaaji katika vyumba vyote 88. Kufikia wakati wazima-moto walipowasili, tayari tulikuwa tumewatoa watu wote katika jengo hilo.” Bw. Neckermann anasema: “Siwezi kuwazia kuwatoa watu upesi kama mlivyofanya katika jengo kubwa kama hili katika jiji kama la Frankfurt. Ninyi mna nidhamu sana, na Kikosi chenu cha Kushughulikia Hali ya Dharura ni stadi kabisa!” Wazima-moto walitambua tatizo lilikuwa nini na wakaliondoa. Hakuna mtu aliyejeruhiwa, na hakuna uharibifu mkubwa uliotokea.

Wote katika ofisi ya tawi ya Selters wanatumaini kwamba moto kubwa hautawahi kutokea kamwe. Hata hivyo, ikiwa utatokea, wajitoleaji wako tayari kwa sababu wamejifunza jinsi ya kukabiliana na moto kwa ustadi.