Hamia kwenye habari

Vigari vya Kukokotwa “Vyaenda Likizo” Nchini Ujerumani

Vigari vya Kukokotwa “Vyaenda Likizo” Nchini Ujerumani

Katika majiji makubwa ulimwenguni pote, wapita njia wamezoea kuona vigari vya kukokotwa vilivyo na machapisho yanayotegemea Biblia yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, nchini Ujerumani Mashahidi wanatoa machapisho kwa njia hiyo katika majiji makubwa kama vile Berlin, Cologne, Hamburg, Munich, na pia katika majiji mengine.

Lakini je, vigari hivyo vilivyo na machapisho yenye kuvutia vinaweza pia kuwa na matokeo katika miji midogo ambako Wajerumani husafiri kwa ajili ya likizo? Watu watakuwa na maoni gani wakiona vigari hivyo katika miji ya kaskazini, katika jamii za pwani, na kwenye visiwa vya Baltiki na bahari ya Kaskazini? Katika mwaka wa 2016, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Ulaya ya Kati ilifanya mpango wa pekee ili kupata majibu ya maswali hayo. Kuanzia Mei hadi Oktoba, Mashahidi 800 hivi ambao hutumia vigari vya kukokotwa katika miji mikubwa, walijitolea kwenda na vigari katika maeneo 60 hivi ya Ujerumani kaskazini. Baadhi ya Mashahidi hao walitoka Vienna, Austria.

“Sehemu ya Mji”

Mashahidi hao walikaribishwa kwa uchangamfu. Mjitoleaji mmoja anaripoti hivi: “Watu walipendezwa. Walikuwa na urafiki, udadisi, na walikuwa tayari kuzungumza nasi.” Heidi, ambaye alisafiri hadi mji wa Plön, anasema hivi: “Baada ya siku kadhaa watu walianza kutuona kuwa sehemu ya mji wao. Baadhi ya wale waliotutambua walitupungia mkono walipotuona.” Mwanamume mmoja kiziwi aliwaambia: “Mko kila mahali!” Yeye na rafiki zake walikuwa wakitoka kwenye mkutano wa viziwi uliofanywa kusini mashariki mwa Ujerumani, ambako pia alikuwa amekutana na Mashahidi wa Yehova.

Baadhi ya wakazi walijitolea kusaidia. Kwenye kisiwa cha Wangerooge, ofisa wa polisi aliwafikia Mashahidi na kuwapendekezea jinsi ambavyo wangeweza kuwapata watu wengi zaidi. Katika eneo la Waren an der Müritz, kapteni wa mashua ya watalii aliwaonyesha abiria wake mambo fulani wanayoweza kupendezwa nayo. Akinyoosha kidole chake kuelekea kigari cha kukokotwa kilichokuwa na machapisho akawaambia: “Na pale mnaweza kujifunza mambo fulani kumhusu Mungu.” Baadhi ya watalii walifika na kusoma mabango ya vigari.

Watalii pamoja na wakazi wa maeneo hayo walipendezwa na broshua hizi tatu:

  • Je, Kweli Mungu Anatujali? Mtalii mmoja alisema hivi: “Nimekuwa nikijiuliza swali hilo kwa muda mrefu. Inashangaza kwamba sasa nikiwa likizo ndipo nitapata nafasi ya kusoma kulihusu.”

  • Habari Njema Kutoka kwa Mungu! Mwanamume mmoja mzee aliwaambia Mashahidi kwamba amekatishwa tamaa na dini. Walimsaidia kuelewa kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumsaidia kutatua matatizo yake; ni Mungu tu anayeweza. Mwanamume huyo alikubali broshua hiyo na akaahidi kuisoma.

  • Masomo Yangu ya Biblia. Baba mmoja alimruhusu binti yake achukue broshua hiyo, ambayo imetayarishwa hasa kwa ajili ya watoto wadogo. Isitoshe, alichukua nakala ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na akasema: “Nina hakika kitabu hiki kitaifaa familia yangu.”

Wapita njia walijipatia zaidi ya machapisho 3,600. Baadhi ya watu waliwaomba Mashahidi wawatembelee ili kuendeleza mazungumzo.

Mashahidi walioshiriki kazi hiyo walifurahia sana nafasi hiyo. Jörg na mke wake, Marina, walisafiri hadi kwenye eneo fulani karibu na Bahari ya Baltiki. Walisema hivi: “Ilikuwa zawadi nzuri. Tulifurahia uumbaji wa Mungu, na wakati huohuo tuliwaeleza kumhusu.” Lukas, aliye na umri wa miaka 17 anasema: “Nilifurahia sana. Mbali na kufurahia niliweza pia kuwapa wengine kitu chenye thamani.”