Hamia kwenye habari

Kusanyiko la Kitagalogi Jijini Rome​—“Muungano Mkubwa wa Familia!”

Kusanyiko la Kitagalogi Jijini Rome​—“Muungano Mkubwa wa Familia!”

Zaidi ya kilomita 10,000 kutoka Filipino​—wanakoishi watu wanaozungumza Kitagalogi​—maelfu ya Mashahidi wa Yehova wanaozungumza Kitagalogi walikusanyika jijini Rome, Italia, kwa ajili ya kusanyiko la pekee lililofanyika Julai 24-​26, 2015.

Kulingana na kadirio moja, zaidi ya Wafilipino 850,000 wanaishi Ulaya. Hii ndiyo sababu makutaniko 60 na vikundi vidogo vya Mashahidi wa Yehova barani Ulaya wanafanya mikutano katika Kitagalogi na kuwahubiria Wafilipino wanaoishi katika jamii zao.

Hata hivyo, katika kusanyiko hilo la jijini Rome, makutaniko na vikundi hivyo vyote vilikusanyika pamoja kwa mara ya kwanza kwa ajili ya kusanyiko la siku tatu lililofanywa kwa lugha yao. Watu 3,239 waliohudhuria walifurahi sana kumsikiliza Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova ambaye aliwahi kutumikia nchini Filipino, akitoa hotuba ya mwisho kila siku.

“Yamenigusa Moyo Sana”

Kuna tofauti kubwa mtu anapohudhuria kusanyiko la lugha yake ya asili na anapohudhuria kusanyiko la lugha yake ya pili. Mzazi mmoja asiye na mwenzi anayeitwa Eva anasema hivi: “Ninaelewa Kiingereza kidogo, lakini nashukuru kwa kusanyiko hili la Kitagalogi, mafundisho ya Biblia yamenigusa moyo sana.” Ili kupata pesa kwa ajili ya kusafiri kutoka nyumbani kwake Hispania hadi Italia, yeye pamoja na watoto wake wawili waliamua kutoenda kula hotelini kila juma kama walivyokuwa wakifanya kwa ukawaida, badala yake waliamua kufanya hivyo mara moja kwa mwezi. Eva anasema hivi: “Jitihada nilizofanya hazikuwa za bure kwa kuwa nimeelewa kila kitu katika kusanyiko hili!”

Jasmin, anayeishi Ujerumani, aliomba likizo kazini ili ahudhurie kusanyiko. Anaeleza hivi; “Lakini kabla sijaondoka, niliambiwa kwamba nisingeweza kuondoka kwa sababu kulikuwa na kazi ya kufanya. Nilitulia, nikasali kwa Yehova, na kuzungumza na mwajiri wangu. Tuliweza kupanga upya ratiba ya kazi ili niweze kuhudhuria kusanyiko! Nilifurahi sana kupata fursa ya kukutana na ndugu na dada wengine Wafilipino kutoka sehemu mbalimbali za bara la Ulaya.”

Bila shaka, Wafilipino wengi wanaoishi Ulaya hukumbuka si tu nchi yao ya asili bali pia huwakosa marafiki wao waliohamia sehemu zingine za Ulaya. Kusanyiko limewasaidia marafiki wengi kukutana tena wakiwa ndugu na dada wa kiroho. (Mathayo 12:48-​50) Fabrice anasema, “Nimefurahi sana kuwaona watu ninaowajua!” Mwishoni mwa kusanyiko hilo, dada mmoja alikuwa akisema hivi kwa mshangao, “Umekuwa muungano mkubwa wa familia!”