Hamia kwenye habari

Kazi ya Kutafsiri Nchini Mexico na Amerika ya Kati

Kazi ya Kutafsiri Nchini Mexico na Amerika ya Kati

Huko Mexico na Amerika ya Kati, watafsiri 290 hivi, wanaoishi katika nchi sita mbalimbali, hutafsiri machapisho ya Biblia katika lugha zaidi ya 60. Kwa nini wanajitahidi kufanya hivyo? Kwa sababu watu wanapopata machapisho ya Biblia katika lugha wanayoelewa kwa urahisi, inaelekea wataguswa moyo zaidi.​—1 Wakorintho 14:9.

Ili kuboresha kazi hiyo, baadhi ya watafsiri waliokuwa wakifanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico City wamehamishiwa kwenye ofisi zilizo katika maeneo ambayo lugha zao zinazungumzwa. Kumekuwa na matokeo gani? Watafsiri wanashirikiana na wenyeji wanaozungumza lugha ambazo wanatafsiri, na hivyo imekuwa rahisi kwao kutafsiri machapisho yanayoeleweka zaidi.

Watafsiri wana maoni gani kuhusu mabadiliko hayo? Federico, mtafsiri wa lugha ya Guerrero Nahuatl, anasema hivi: “Kwa miaka kumi hivi niliyokuwa Mexico City, nilipata familia moja tu iliyozungumza lugha yangu. Lakini sasa, kwenye miji iliyo karibu na ofisi ya utafsiri, karibu kila mtu huzungumza lugha hiyo!”

Karin, anayetafsiri lugha ya Low German katika ofisi iliyo kwenye jimbo la Chihuahua nchini Mexico anasema hivi: “Kuishi miongoni mwa Wameno kumenisaidia kujua mambo ya karibuni zaidi kuhusu lugha yao. Tunaishi na kufanya kazi katika mji mdogo, na ninapotazama dirishani, ninaweza kuona watu watakaonufaika kutokana na kazi ya kutafsiri tunayofanya hapa.”

Neyfi, anayeishi katika ofisi ya utafsiri huko Mérida, Mexico, anasema: “Tunapoongoza mafunzo ya Biblia katika Kimaya, tunatambua maneno ambayo hayaeleweki kwa urahisi na Wamaya. Hivyo, tunatafuta njia za kutafsiri maneno hayo ili yaeleweke kwa urahisi zaidi.”

Wale wanaopata machapisho hayo wananufaikaje? Fikiria mfano mmoja: Kwa miaka 40 hivi, Elena, ambaye lugha yake ya asili ni Tlapanec, alikuwa akihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida. Lakini kwa sababu mikutano ilifanywa kwa Kihispania, hakuelewa kilichokuwa kikizungumzwa. Anasema hivi: “Nilichojua tu ni kwamba nilitaka kuwepo mikutanoni.” Hata hivyo, baada ya Elena kujifunza Biblia kwa kutumia broshua za lugha ya Tlapanec, upendo wake kwa Mungu uliongezeka kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa mwaka wa 2013. Elena anasema: “Namshukuru Yehova kwa kuniruhusu nielewe Biblia.”