Hamia kwenye habari

Mwongozo wa Misamiati

Mwongozo wa Misamiati

Asante kwa kuwa na hamu ya kujua mengi zaidi unaporipoti juu ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Mwongozo ufuatao wa misamiati umeandaliwa ili kukusaidia kuelewa matumizi ya maneno katika shirika letu la kidini. Ikiwa una maswali yoyote kuhusu habari fulani ambayo haijazungumziwa katika mwongozo huu, tafadhali wasiliana na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova.

kusanyiko. Ona: kusanyiko la mzunguko, kusanyiko la eneo, na kusanyiko la kimataifa.

Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Eneo kubwa linalotumiwa kwa ajili ya ibada. Linamilikiwa na Mashahidi wa Yehova na linatumiwa mara kwa mara kufanya mikutano mikubwa inayojumuisha makutaniko kadhaa katika eneo hususa. Linaweza kuitwa “Jumba la Kusanyiko.”

Amkeni! Ni gazeti linalochapishwa na kusambazwa na Mashahidi wa Yehova. Lilianza kuchapishwa mwaka wa 1919 ambapo liliitwa The Golden Age, kisha katika mwaka wa 1937 likabadilishwa jina kuwa Consolation. Jina Amkeni! lilianza kutumiwa katika toleo la Agosti 22, 1946. Jina Amkeni! lilichaguliwa ili kukazia kwamba wasomaji wanapaswa kutambua umuhimu wa matukio ya ulimwengu. Ni mojawapo ya magazeti yaliyosambazwa zaidi duniani.

Betheli, Mwanabetheli, Familia ya Betheli. “Betheli” ni neno la Kiebrania linalomaanisha “Nyumba ya Mungu.” Neno hilo linatumiwa kurejelea majengo yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ili kuongoza na kutegemeza utendaji wao wa kiroho unaotegemea Biblia katika kila nchi au eneo fulani. Mashahidi wanaotumikia katika sehemu hizo ni washiriki wa kikundi cha kidini na wanaitwa “Wanabetheli.” Hawalipwi mshahara. Kwa ujumla, wanarejelewa kuwa “Familia ya Betheli” kwa sababu kama familia inavyokuwa, wanaishi, wanaabudu, na kufanya kazi pamoja katika sehemu hizo. Neno “Mwanabetheli” halitumiwi kama jina la cheo.

Halmashauri ya Tawi. Ofisi ya tawi inapoanzishwa, Halmashauri ya Tawi yenye wazee watatu au zaidi inateuliwa ili kusimamia utendaji unaofanywa katika nchi hiyo au nchi zote zitakazokuwa chini ya ofisi hiyo ya tawi.

ofisi ya tawi. Ni kituo cha usimamizi cha Halmashauri ya Tawi kinachotumiwa kutegemeza na kuongoza utendaji wa kiroho wa Mashahidi wa Yehova katika nchi moja au zaidi.

ndugu. Ni mwanamume aliyebatizwa kuwa Shahidi wa Yehova. Herufi ndogo hutumiwa neno hilo linaporejelea akina ndugu kwa ujumla. Herufi kubwa hutumiwa neno hilo linapoambatana na jina la ukoo la mwanamume ambaye ni Shahidi (mf., Ndugu Smith). Halitumiwi kama jina la cheo. Matumizi hayo yanahusika inapowahusu wanawake ambao ni Shahidi (mf., Dada Smith).

undugu. Hutumiwa kurejelea ushirika mzima wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote (wa kiume na wa kike).​—1 Petro 5:9.

mzunguko. Ni kikundi cha makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yaliyo katika eneo lililoteuliwa.

kusanyiko la mzunguko. Ni mkutano wa makutaniko kadhaa ya Mashahidi wa Yehova unaofanywa kwa siku moja, mara mbili kwa mwaka. Kusudi la makusanyiko ya mzunguko ni kuwasaidia watu wamkaribie Mungu na wote wanakaribishwa. Programu hiyo ina mapendekezo mazuri yanayoweza kuwasaidia wahudhuriaji wa umri wote kunufaika kutokana na ushauri wa Biblia. Kuna maigizo mafupi yanayohusu maisha ya kila siku na jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. Mara nyingi makusanyiko hayo yanafanyiwa katika Majumba ya Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Pia yanaweza kufanyiwa katika eneo lililokodiwa au yanaweza kutazamwa mtandaoni. Kwa kawaida, yanafanywa mwisho-juma. Vipindi vyote vinafanywa bila malipo na hakuna sadaka zinazokusanywa.

mwangalizi wa mzunguko. Ni mzee mwenye uzoefu anayetumikia chini ya mwongozo wa ofisi ya tawi ya eneo hilo. Kwa kawaida, anatembelea (pamoja na mke wake, ikiwa ameoa) kila kutaniko katika mzunguko fulani mara mbili kwa mwaka. Zaidi ya kumtia moyo mtu mmoja-mmoja katika kutaniko, anawatia moyo wazee na watumishi wa huduma na kuwapa mapendekezo mbalimbali. Waangalizi wa mzunguko huongoza programu ya pekee kwa ajili ya kila kutaniko ili kuwapa maagizo. Maneno hayo hayatumiwa kama jina la cheo chenye heshima.

kutaniko. Ni kikundi kilichopangwa cha Mashahidi ambao hukutana pamoja mara kwa mara ili kuabudu pamoja. Baraza la wazee lina jukumu la kusimamia programu mbalimbali zinazofanywa kwa ajili ya kutaniko zima au mtu mmoja-mmoja ili kuwapa mwongozo wa kiroho unaotegemea Biblia.

mzee. Ni mwanamume Shahidi aliyekomaa kiroho aliyewekwa rasmi kufundisha na kuandaa utunzaji wa kiuchungaji kwa washiriki wa kutaniko. Mzee anapaswa kutimiza sifa za kustahili zinazoonyeshwa katika Maandiko kwenye 1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9; Yakobo 3:17, 18; na 1 Petro 5:2. Wazee si wahudumu wanaolipwa na si wafanyakazi wa kutaniko wanaloshiriki wala wa shirika lolote la Mashahidi wa Yehova. Wazee wengi hufanya kazi za kimwili ili kujitegemeza wao na familia zao. Wazee hawafanyizi jamii ya makasisi wala hawana tofauti yoyote na washiriki wengine wa kutaniko. Neno mzee halitumiwi kama jina la cheo au la utukuzo.

utumishi wa shambani. Inarejelea huduma ya Mashahidi wa Yehova kwa kufuata amri ya Yesu ya kuwaeleza watu “habari njema ya Ufalme” walio “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”​—Mathayo 24:14; 28:19.

Gileadi, Shule ya Gileadi. Inarejelea Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower iliyoanzishwa mwaka wa 1943 kwa kusudi la kuwazoeza wamishonari. Sasa wanafunzi ambao ni Mashahidi wa Yehova wanaoalikwa wanafundishwa masomo fulani hususa yanayotegemea Biblia kwa kipindi cha miezi mitano. Neno “shule” linapotumiwa bila maneno “ya Gileadi” linaandikwa kwa herufi ndogo.

Baraza Linaloongoza. Ni kikundi kidogo cha wazee walioteuliwa ili kushughulikia mahitaji ya kiroho ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wanahusika moja kwa moja katika kazi ya kutayarisha machapisho yanayotegemea Biblia. Ingawa washiriki wa Baraza Linaloongoza wanaratibu utendaji wa kimataifa wa Mashahidi, Baraza Linaloongoza lina maoni ya kwamba Yesu Kristo ndiye Kiongozi wa Mashahidi wa Yehova. Ofisi za Baraza Linaloongoza zipo katika Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova yaliyo Warwick, New York, Marekani.

kusanyiko la kimataifa. Ni mkutano wa siku tatu wa ibada na wa kujifunza Biblia ambao unatayarishwa na Mashahidi wa Yehova ili kutoa mafundisho yanayotegemea Biblia. Unafanywa mara moja kila baada ya miaka kadhaa katika majiji mbalimbali yaliyoamuliwa mapema duniani pote. Mashahidi kutoka nchi mbalimbali hualikwa kama wajumbe. Watu wote wanakaribishwa kuhudhuria kusanyiko hili lililokusudiwa kuwasaidia watu huku likiimarisha pia umoja wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Makusanyiko haya hufanyiwa katika maeneo yaliyokodishwa na yanaanza Ijumaa na kuendelea hadi Jumapili.

Yehova. Ni jina la kibinafsi la Mungu Mweza-Yote na Muumba kama inavyofunuliwa katika Maandiko. (Zaburi 83:18) Jina “Yehova” halitumiwi kama neno la badala (mf., “Myehova”) ili kurejelea Shahidi wa Yehova.

Mashahidi wa Yehova. Ni kikundi cha kidini cha Wakristo ambao wanamwabudu Yehova Mungu na wanaotumia muda wao kutegemeza elimu ya Biblia katika njia mbalimbali. Lengo halisi la kazi yao ya kufundisha watu Biblia ni kushiriki habari njema ya Ufalme au serikali ya Mungu. (Mathayo 24:14) Jina hilo linawatofautisha na dini nyingine kwa kuwa linamrejelea yule wanayemwakilisha na pia kazi wanayojitolea kufanya katika jina la Mungu. Mtu haonwi kuwa Shahidi wa Yehova hadi tu anapokuwa na uelewa wa kutosha wa mafundisho ya msingi ya Biblia, anapostahili kushiriki katika huduma ya hadharani pamoja na kutaniko la Mashahidi wa Yehova, na anapobatizwa ili kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Mungu. Kikundi hiki kinaporejelewa katika makala, jina kamili linapaswa kutumiwa mara ya kwanza. Baada ya hapo, makala hiyo inaweza kutumia ufupisho kwa kuandika “Mashahidi.” Ili kurejelea mtu mmoja-mmoja, tumia “Shahidi,” “Shahidi wa Yehova,” au “mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” Kutumia maneno “Mjehova,” “wa Jehova,” “Wayehova,” au “Mshahidi,” si sahihi.​—Isaya 43:10.

 Yesu Kristo. Mzaliwa mzaliwa pekee wa Mungu. (Yohana 3:16) Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Yesu Kristo ndiye Kiongozi wao na wanajitahidi kuiga mfano wake na kuishi kupatana na mafundisho yake. Mashahidi wanamwona Yesu kuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, Shahidi wa kwanza wa Yehova, na yule ambaye Yehova Mungu atamtumia ili kuwaokoa wanadamu wote.​—Isaya 9:6, 7; Ufunuo 1:5.

Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Ni sehemu ambayo inatumiwa kwa ajili ya ibada na kutaniko moja au zaidi. Linaweza kuitwa “Jumba la Ufalme” kwa ufupi. Tafadhali epuka kutumia neno “kanisa.”

Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Ni mwadhimisho unaofanywa kila mwaka ili kukumbuka kifo cha Kristo. Jina lingine ni Mlo wa Jioni wa Bwana, Mlo wa Mwisho, Ukumbusho, au Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kwa Mashahidi wa Yehova hili ndilo tukio muhimu zaidi katika mwaka mzima na ndio mwadhimisho pekee ambao Kristo aliwaamuru wafuasi wake wazingatie.​—Luka 22:19, 20.

mkutano wa katikati ya juma. Ni mkutano unaofanywa kila juma, kwa kawaida, ni jioni moja katikati ya juma. Mkutano huo wenye kichwa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo una sehemu tatu, na kusudi lake ni kuwasaidia Wakristo kuwa na matokeo mazuri katika huduma yao. Kama tu mikutano mingine ya Mashahidi wa Yehova, wale wanaohudhuria iwe ni uso kwa uso au kupitia mtandao hawadaiwi malipo yoyote na hakuna sadaka zinazokusanywa.

mtumishi wa huduma. Ni mwanamume anayependa sana mambo ya kiroho na aliyewekwa rasmi kuwasaidia wazee kufanya kazi nyingine ambazo hazihusishi utunzaji wa kiuchungaji wa washiriki wa kutaniko. Ili kutumika akiwa mtumishi wa huduma anapaswa kuendelea kuonyesha sifa za kustahili zinazoonyeshwa katika Maandiko kwenye 1 Timotheo 3:8-10, 12, 13 na Tito 2:2, 6-8. Watumishi wa huduma hushughulikia mambo mengi muhimu yanayofanywa katika tengenezo ili kutegemeza kazi inayofanywa katika kutaniko. Halipwi kwa kazi anayofanya na si mfanyakazi wa kutaniko analoshiriki wala wa shirika lolote la Mashahidi wa Yehova. Watumishi wengi wa huduma hufanya kazi za kimwili ili kujitegemeza wao na familia zao. Baadhi ya watumishi wa huduma wanaweza kustahili kuwa wazee baadaye. Maneno “mtumishi wa huduma” hayatumiwi kama jina la cheo.

mishonari. Shahidi aliyebatizwa aliyepewa mgawo na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kutumikia katika maeneo mbalimbali ulimwenguni pote. Wamishonari wako tayari kuondoka nyumbani kwao na labda kuhamia nchi nyingine ili kusaidia kueneza habari njema ya Ufalme.​—Mathayo 24:14.

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Ni kichwa kirefu cha Maandiko ya Kiebrania (Agano la Kale) na Maandiko ya Kigiriki (Agano Jipya) yaliyotafsiriwa na kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kwa kifupi, Biblia hiyo inaweza kuitwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

painia. Ni jina linalotumiwa kumrejelea mtu anayejitolea kutumia idadi fulani ya saa kila mwezi katika huduma yake ya hadharani. Kwa kawaida, neno “painia” hutumiwa kama kifupi cha maneno “painia wa kawaida,” ambaye hujitolea kutumia saa 600 kila mwaka (saa 50 kila mwezi). Mara nyingine, neno hilo linaweza kutumiwa kama kifupi cha maneno “painia msaidizi,” ambaye ni mtu anayejitolea kutumia saa 15 au 30 kwa mwezi mmoja au kwa miezi kadhaa mfululizo. Mapainia hawalipwi kwa kushiriki huduma ya hadharani na si wafanyakazi wa kutaniko wanaloshiriki wala wa shirika lolote la Mashahidi wa Yehova. Mapainia wengi hufanya kazi za kimwili ili kujitegemeza. Neno “painia” halitumiwi kama jina la cheo.

kuhubiri. Ona: utumishi wa shambani.

Mkutano wa Watu Wote. Ni mkutano unaofanywa kila juma kutanikoni. Kwa kawaida, hufanywa mwisho-juma ambapo hotuba ya dakika 30 inayotegemea Biblia iliyoandaliwa kwa ajili ya watu wote hutolewa. Hotuba hiyo hufuatwa na Funzo la Mnara wa Mlinzi, ambacho ni kipindi cha saa moja cha mazungumzo ya maswali na majibu kuhusu mada fulani katika Biblia inayotegemea makala iliyo katika toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi. Kama tu mikutano mingine ya Mashahidi wa Yehova, wale wanaohudhuria iwe ni uso kwa uso au kupitia mtandao hawadaiwi malipo yoyote na hakuna sadaka zinazokusanywa.

mhubiri. Ni mtu anayeshiriki huduma ya hadharani inayopangwa na kutaniko fulani la Mashahidi wa Yehova. Ili kustahili kuwa mhubiri mtu anahitaji kuelewa na kuamini mafundisho ya msingi ya Biblia na pia kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Wahubiri hawalipwi kwa kushiriki katika huduma na si wafanyakazi wa kutaniko wanaloshiriki wala wa shirika lolote la Mashahidi wa Yehova. Neno “mhubiri” halitumiwi kama jina la cheo.

kusanyiko la eneo. Mkutano wa siku tatu unaofanywa kila mwaka na makutaniko kadhaa katika eneo fulani, lengo ni kuchochea hali ya kiroho ya wote. Watu wote wanakaribishwa. Programu hiyo inatia ndani mapendekezo yanayowasaidia wahudhuriaji wa kila rika kunufaika na ushauri wa Biblia. Kuna maigizo yanayohusu maisha ya kila siku na ya masimulizi ya Biblia yanayowasaidia watu kutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Makusanyiko ya eneo huwa yanafanywa katika maeneo makubwa kama vile uwanja wa michezo, au vituo vya mikutano mikubwa (convention centers). Ikiwa kusanyiko la eneo halitakuwa na watu wengi linaweza kufanywa katika Jumba la Makusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililo karibu. Kwa kawaida, programu hiyo inaanza Ijumaa na kuisha Jumapili. Katika miaka ya karibuni, rekodi ya programu nzima zimewekwa mtandaoni. Kama tu mikutano mingine ya Mashahidi wa Yehova, wale wanaohudhuria hawadaiwi malipo yoyote na hakuna sadaka zinazokusanywa.

dada. Mwanamke aliyebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Ili kurejelea akina dada kwa ujumla herufi ndogo hutumiwa. Herufi kubwa hutumiwa neno hilo linapoambatana na jina la ukoo la mwanamke ambaye ni Shahidi (mf., Dada Smith). Halitumiwa kama jina la cheo. Linatumiwa kwa njia ileile kama tunapomrejelea mwanamume ambaye ni Shahidi (mf., Ndugu Smith).

Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Ni jina kamili la gazeti linalotumiwa zaidi kati ya magazeti yanayochapishwa na kusambazwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, linaweza kurejelea kama Mnara wa Mlinzi au Mnara. Jina hilo linatokana na wazo la kuendelea kukesha katika nyakati za Biblia. (Isaya 21:8; Ezekieli 33:7) Lengo la gazeti hili ni kuwasaidia wasomaji kuendelea kukesha wanaposubiri kuona utimizo wa kusudi la Mungu. (Mathayo 24:42) Watu wanaopendezwa wanapewa toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi bila malipo yoyote. Makutaniko yote ulimwenguni hutumia toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi kwenye mikutano ya mwisho-juma katika kipindi cha mazungumzo ya maswali na majibu. Gazeti Mnara wa Mlinzi limekuwa likichapishwa tangu mwaka wa 1879 na ndilo gazeti linalosambazwa kwa wingi zaidi kila mwezi ulimwenguni pote.

ZINGATIA: Unaporipoti kuwahusu Mashahidi wa Yehova, tafadhali tumia jina kamili kuwarejelea kwa mara ya kwanza katika kila makala. Ili upate habari zaidi, ona:  Mashahidi wa Yehova.