Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Sijisikie Tena Kuwa Ninapaswa Kubadilisha Dunia”

“Sijisikie Tena Kuwa Ninapaswa Kubadilisha Dunia”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1966

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA FINLANDE

  • ALIKUWA MUTU ALIYECHOCHEA WATU KWA AJILI YA MABADILIKO

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilipenda sana kutazama uumbaji tangu nilipokuwa mutoto. Mara nyingi, familia yetu ilifurahia kufanya matembezi kwenye misitu yenye kuvutia na pia kwenye bahari mbalimbali nzuri zilizozunguka muji wetu wa Jyväskylä, uliokuwa katika sehemu ya kati ya inchi ya Finlande. Pia, ninapenda sana wanyama. Nilipokuwa mutoto, nilipenda kukumbatia kila paka na kila mbwa niliona! Wakati nilikuwa ninakomaa, nilisumbuliwa akili kwa sababu ya namna watu waliwatendea wanyama vibaya. Baada ya muda, nilijiunga na shirika linalotetea haki za wanyama. Katika shirika hilo nilikutana na watu wengine ambao walikuwa na mawazo kama yangu kuhusu wanyama.

Tulifanya kampanye kwa bidii ili kutetea haki za wanyama. Tulisambaza habari na tulipanga maandamano ili kupinga maduka yanayouzisha manyoa ya wanyama na vyumba ambamo wanyama wanafanyiwa uchunguzi wa kisayansi. Tuliunda hata shirika mupya la kulinda wanyama. Kwa sababu tulichukua hatua kali mbalimbali ili kujaribu kuendeleza muradi wetu, mara nyingi tulisumbuliwa na wenye mamlaka. Mara nyingi, nilifungwa na kupelekwa kwenye mahakama.

Zaidi ya kuwahangaikia wanyama, nilivurugika pia kwa sababu ya matatizo mengine ambayo yanawapata wanadamu. Mwishowe, nilijiunga na mashirika mbalimbali, kutia ndani shirika la Amnesty International na la Greenpeace. Nilitumia nguvu zangu zote ili kuunga mukono kazi za mashirika hayo. Nilitetea haki za maskini, watu wanaosumbuliwa na njaa, na watu wengine wasiojiweza.

Hata hivyo, nilianza kuelewa polepole kwamba singeweza kubadilisha dunia. Ijapokuwa mashirika hayo yaliweza kurekebisha matatizo fulani madogo, matatizo makubwa yaliendelea kuwa magumu zaidi. Ilikuwa kama vile nguvu za uovu zilikuwa zimeambukiza dunia nzima na hakuna mutu aliyehangaika juu ya jambo lolote. Nilijisikia kuwa sina uwezo wa kufanya jambo lolote.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Kujisikia kuwa sina uwezo wa kufanya jambo lolote kuliniletea huzuni sana, kwa hiyo nilianza kufikiri juu ya Mungu na Biblia. Zamani nilikuwa nimejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Ijapokuwa nilifurahia Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya wema wao na kwa sababu walipendezwa na mimi kipekee, sikuwa tayari kubadilisha namna yangu ya kuishi. Lakini wakati huu, mambo yalikuwa tofauti.

Nilichukua Biblia yangu na nikaanza kuisoma. Kwa kweli, kusoma Biblia kulinifariji sana. Niliona maandiko mengi ya Biblia ambayo yanafundisha kuwatendea wanyama vizuri. Kwa mufano, andiko la Methali 12:10 linasema kwamba ‘Mwadilifu anatunza nafsi ya munyama wake wa kufugwa.’ Pia, nilitambua kwamba si Mungu ambaye analeta matatizo yaliyo katika dunia. Lakini, matatizo yetu yanaendelea kuwa mabaya zaidi kwa sababu watu wengi hawafuate muongozo wa Mungu. Niliguswa moyo sana wakati nilijifunza kuhusu upendo wa Yehova na uvumilivu wake.​—Zaburi 103:8-14.

Karibu na wakati huo, nilijaza nafasi iliyokuwa wazi kwenye kichapo fulani ili kuomba kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? Kisha, Mashahidi wa Yehova wawili ambao walikuwa bibi na bwana walikuja nyumbani na wakaniomba nijifunze Biblia pamoja nao, na nikakubali. Pia, nilianza kuhuzuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme. Kwa hiyo, nikaanza kupenda sana mambo ambayo nilikuwa ninajifunza katika Biblia.

Kwa musaada wa Biblia, niliweza kufanya mabadiliko mengi. Niliacha kuvuta tumbaku na kunywa pombe sana. Nilitengeneza hali yangu ya inje na namna yangu ya kusema. Na nilianza kuheshimu wenye mamlaka. (Waroma 13:1) Katika maisha yangu nilikuwa ninafanya jambo lolote ambalo nilitaka, lakini nikaachana pia na mwenendo huo mubaya.

Badiliko ambalo lilikuwa ngumu sana kwangu lilikuwa kuachana na mashirika ya kutetea haki za wanadamu na za wanyama. Ilinichukua muda murefu ili kufanya badiliko hilo. Mwanzoni, nilijisikia kuwa ikiwa ninaachana na mashirika hayo itakuwa kama vile ninayasaliti. Hata hivyo, nilielewa kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini moja tu la kweli kwa matatizo ya wanadamu. Niliamua kutumia nguvu zangu zote ili kuunga mukono Ufalme huo na kuwasaidia watu wengine wajifunze kuhusu Ufalme huo.​—Mathayo 6:33.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA:

Nilipokuwa mutu aliyechochea mabadiliko, nilizoea kugawanya watu katika vikundi viwili, ni kusema, kikundi cha watu wazuri na kikundi cha watu wabaya, na nilikuwa tayari kutenda ili kuwapinga wale ambao niliona kuwa ni wabaya. Lakini kwa musaada wa Biblia, sina tena tabia ya kuwachukia watu wengine. Lakini kwa sababu sasa mimi ni Mukristo, ninajikaza kuwapenda watu wote. (Mathayo 5:44) Kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu ni moja kati ya njia ambazo ninatumia ili kuwaonyesha watu upendo huo. Mimi ni mwenye furaha kuona namna kazi hiyo nzuri inavyosaidia watu kuwa na amani na furaha na kuwatolea tumaini la kweli.

Nimepata amani ya akili kwa kuacha mambo katika mikono ya Yehova. Nina uhakika kwamba, kwa kuwa yeye ndiye Muumbaji, hataacha wanyama na wanadamu waendelee kutendewa vibaya milele, wala kuacha dunia yetu nzuri iharibiwe. Lakini, hivi karibuni kupitia Ufalme wake, atarekebisha mambo yote mabaya ambayo yamefanywa juu ya dunia. (Isaya 11:1-9) Ninapata furaha kubwa kwa kujua mambo hayo na pia kwa kusaidia wengine wayaamini. Sijisikie tena kuwa ninapaswa kubadilisha dunia.