Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

UIGE IMANI YAO | ELIYA

Alivumilia Ukosefu wa Haki

Alivumilia Ukosefu wa Haki

ELIYA alitembea katika Bonde la Yordani. Alikuwa amekwisha kusafiri kwa majuma fulani, akijielekeza kaskazini mbali sana na Mulima Horebu. Sasa, aliporudia Israeli mwishowe, angeona mabadiliko katika inchi yake. Matokeo mabaya ya kipindi kirefu cha ukosefu wa mvua yalikuwa yameanza kupunguka. Mvua ndogo​-ndogo za wakati wa kuchipuka kwa majani zilianza kunyesha, na walimaji walikuwa inje wakilima mashamba yao. Inawezekana jambo hilo lilimufariji nabii huyo alipoona inchi yake imerudi katika hali nzuri. Lakini ni watu wake ndio alihangaikia zaidi. Watu hao hawakuishi kulingana na sheria za Mungu. Waliendelea kuabudu mungu Baali, na Eliya alikuwa na kazi kubwa ya kufanya. *

Karibu na muji wa Abel​-mehola, Eliya alikuta kikundi kikubwa cha walimaji waliokuwa wanalima. Kulikuwa ngombe 24 zilizokuwa zinafanya kazi zikiwa zenye kufungwa mbili​-mbili, na vikundi 12 vya ngombe hizo vilikuwa vinalima kwa wakati uleule, vikichimba mifereji katika udongo wenye majimaji. Mwanaume aliyekuwa anaongoza kikundi cha mwisho ndiye ambaye Eliya alikuwa anatafuta. Mwanaume huyo aliitwa Elisha, Yehova alikuwa amemuchagua ili achukue nafasi ya Eliya. Wakati fulani, Eliya alifikiri alibaki yeye peke yake mushikamanifu kwa Mungu katika inchi yote. Kwa hiyo, alikuwa na hamu ya kumuona mwanaume huyo.​—1 Wafalme 18:22; 19:14-19.

Je, Eliya alisita kumupatia Elisha madaraka yake fulani, ni kusema, kugawa mapendeleo yake, ao kuogopa kwamba siku fulani atachukua nafasi yake? Hatuwezi kusema hivyo; na pia hatuwezi kukataa kwamba inawezekana alifikiri hivyo. Kwa kweli, alikuwa ‘mutu mwenye hisia kama zetu.’ (Yakobo 5:17) Iwe ilikuwa hivyo ao hapana, Biblia inasema hivi: ‘Eliya akavuka mupaka pale alipokuwa, akalitupa vazi lake rasmi juu yake.’ (1 Wafalme 19:19) Vazi ao nguo ya pekee ya Eliya, ambayo inawezekana ilitengenezwa kwa manyoya ya kondoo ao ya mbuzi, ilivaliwa kama nguo ya inje na ilifananisha cheo cha pekee alichopewa na Yehova. Kwa hiyo, kutupa nguo hiyo juu ya mabega ya Elisha, ilikuwa ishara yenye maana sana. Eliya alitii bila kulazimishwa amri ya Yehova ya kumuweka Elisha ili achukue nafasi yake. Eliya alimutumaini Mungu wake na alimutii.

Kwa unyenyekevu, Eliya alimuweka Elisha ili achukue nafasi yake

Kwa upande wake, kijana huyo alikuwa na hamu sana ya kumusaidia nabii huyo aliyezeeka. Elisha hangechukua nafasi ya Eliya mara moja. Lakini, kwa muda wa miaka sita hivi, alimusindikiza kwa unyenyekevu nabii huyo muzee na kumusaidia. Mwishowe Elisha alijulikana kuwa mutu “aliyemimina maji juu ya mikono ya Eliya.” (2 Wafalme 3:11) Eliya alifarijiwa sana kuwa na musaidizi kama huyo mwenye uwezo na mwenye kumuhangaikia! Inawezekana wanaume hao wawili walikuja kuwa marafiki wazuri. Bila shaka, kutiana kwao moyo kuliwasaidia wote wawili waendelee kuvumilia hata ikiwa waliona ukosefu mwingi wa haki ulioenea katika inchi yote, hasa, ukosefu wa haki wa mufalme muovu Ahabu aliyeendelea kuwa muovu sana.

Umekwisha kutendewa bila haki? Wengi kati yetu wamekwisha kutendewa bila haki katika ulimwengu huu muovu. Kupata rafiki anayemupenda Mungu kunaweza kukusaidia uvumilie. Unaweza pia kujifunza mambo mengi kupitia imani ya Eliya unapotendewa bila haki.

‘ONDOKA, ENDA UKUTANE NA AHABU’

Eliya na Elisha walitumika sana ili kuwasaidia watu wawe na hali nzuri ya kiroho. Kwa kweli, walichukua uongozi katika kuzoeza manabii wengine, ambao pengine walipangwa katika masomo ya aina fulani. Hata hivyo, kisha muda fulani, Eliya alipata mugawo mupya kutoka kwa Yehova: ‘Ondoka, enda ukutane na Ahabu mufalme wa Israeli.’ (1 Wafalme 21:18) Ahabu alikuwa amefanya nini?

Mufalme alikuwa tayari muasi​-imani, yeye ndiye alikuwa mufalme muasi-imani zaidi kati ya wafalme wote wa Israeli. Alikuwa amemuoa Yezebeli na alifanya ibada ya Baali ienee kotekote katika inchi, na yeye mwenyewe alishiriki katika ibada hiyo. (1 Wafalme 16:31-33) Ibada ya Baali ilitia ndani sherehe za uzazi, ukahaba na kutoa watoto kuwa zabihu. Zaidi ya hayo, Ahabu alikuwa amepinga amri ya Yehova ya kumuua Ben-hadadi, Mufalme muovu wa Siria. Ni wazi kwamba Ahabu alikataa kumuua mufalme huyo ili apate faida za kifeza. (1 Wafalme, sura ya 20) Lakini sasa, Ahabu na Yezebeli wakaendelea kuwa wabaya sana, waliendelea kuwa wenye pupa, wenye kupenda vitu vya kimwili, na wenye jeuri.

Ahabu alikuwa na nyumba ya kifalme katika Samaria, na nyumba hiyo ilikuwa kubwa kabisa! Alikuwa na nyumba nyingine katika muji wa Yezreeli, uliokuwa kwenye kilometa 37 mbali na Samaria. Kulikuwa shamba kubwa la mizabibu karibu na nyumba ya huko Yezreeli. Ahabu alitamani sana shamba hilo ndogo, ambalo lilikuwa la mwanaume anayeitwa Nabothi. Ahabu alimuitisha Nabothi na akasema kwamba atamupatia feza kwa ajili ya shamba hilo ao kubadilishana naye na shamba lingine. Nabothi akasema hivi: ‘Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba mimi nikupe fungu la uriti la mababu zangu.’ (1 Wafalme 21:3) Je, Nabothi alikuwa mutu mwenye kiburi na asiyehangaikia kitu? Watu wengi wanafikiri hivyo. Kwa kweli, alikuwa mutiifu kwa Sheria ya Yehova, ambayo haikuwaruhusu Waisraeli kuuzisha shamba ambalo lilikuwa uriti wa familia yao. (Mambo ya Walawi 25:23-28) Nabothi aliona kwamba haingewezekana kuvunja Sheria ya Mungu. Alikuwa mwanaume mwenye imani na mwenye bidii, kwa sababu alijua kwamba kumupinga Ahabu kungehatarisha maisha yake.

Kwa kweli, Ahabu hakufikiria jambo lolote juu ya Sheria ya Yehova. Alirudi nyumbani kwake, “akiwa mwenye kinyongo na mwenye huzuni” kwa sababu hakupata kitu alichotaka. Habari hiyo inasomeka hivi: ‘Kisha akalala kitandani pake, akakaa akiwa amegeuza uso wake, naye hakula mukate.’ (1 Wafalme 21:4) Wakati Yezebeli alimuona bwana yake akinuna-nuna kama mutoto mudogo, akafanya mupango ili kumupatia kitu alichohitaji na pia akatunga njama ya kuua familia ambayo haikuwa na kosa.

Mutu hawezi kusoma juu ya ujanja wa Yezebeli bila kushangazwa na uovu wake. Malkia Yezebeli alikuwa anajua kwamba Sheria ya Mungu iliomba ushahidi wa watu wawili ili kuhakikisha jambo ngumu. (Kumbukumbu la Torati 19:15) Kwa hiyo, akaandika barua kwa jina la Ahabu. Katika barua hiyo aliwaamuru wanaume wenye vyeo wa muji wa Yezreeli watafute wanaume wawili ambao watamushitaki Nabothi jambo la uongo, ni kusema, kukufuru, ambako kungeleta azabu ya kifo. Mupango wake ulipata matokeo mazuri. Wanaume wawili “wasiofaa kitu” wakatoa ushahidi wa uongo juu ya Nabothi, na akauawa kwa kupigwa majiwe. Na mambo hayakuishia pale, watoto wa Nabothi nao wakauawa! * (1 Wafalme 21:5-14; Mambo ya Walawi 24:16; 2 Wafalme 9:26) Ahabu aliacha kutumia ukichwa wake na akamuruhusu bibi yake afanye analotaka na kuwaua watu wasiokuwa na kosa.

Wazia namna Eliya alijisikia moyoni wakati Yehova alimufunulia mambo ambayo mufalme na malkia Yezebeli walikuwa wamefanya. Linaweza kuwa jambo lenye kuvunja moyo sana wakati watu waovu wanapata ushindi juu ya watu wasio na kosa. (Zaburi 73:3-5, 12, 13) Leo, tunaona mara kwa mara matendo mabaya ya ukosefu wa haki yakifanywa, wakati fulani yanafanywa hata na watu wenye uwezo wanaojidai kuwa wanatenda kama wawakilishi wa Mungu. Hata hivyo, habari hii inaweza kututia moyo. Kupitia habari hii, Biblia inatukumbusha kwamba hakuna kitu kinachofichwa machoni pa Yehova. Anaona mambo yote. (Waebrania 4:13) Yehova anafanya nini juu ya matendo maovu anayoona?

“JE, UMENIPATA, EWE ADUI YANGU?”

Yehova alimutuma Eliya kwa Ahabu. Mungu alisema waziwazi hivi: “Tazama, yupo katika shamba la mizabibu la Nabothi.” (1 Wafalme 21:18) Wakati Yezebeli alimuambia Ahabu kwamba shamba hilo la mizabibu linakuwa sasa lake, alilamuka palepale na akaenda kufurahia shamba hilo mupya. Hakuwazia hata kidogo kwamba Yehova alikuwa anaona. Fikiria uso wake alipokuwa katika shamba hilo la mizabibu, akifikiria bustani nzuri sana ambazo angefanya katika shamba hilo. Lakini, bila kutazamia, Eliya akatokea! Uso wa Ahabu wenye furaha ukabadilika, akajaa hasira na chuki, na kusema hivi: “Je, umenipata, ewe adui yangu?”​—1 Wafalme 21:20.

“Je, umenipata, ewe adui yangu?”

Maneno ya Ahabu yanaonyesha upumbavu wa aina mbili. Upumbavu wa kwanza: Kwa kumuambia Eliya, “Umenipata,” Ahabu alionyesha kwamba hakuwa anamufikiria Yehova. Yehova alikuwa tayari “amemupata.” Aliona Ahabu akitumia vibaya zawadi yake ya uhuru wa kuchagua na kufurahia matokeo ya mupango mubaya wa Yezebeli. Mungu aliona katika moyo wa Ahabu kwamba upendo wa vitu vya kimwili ulikuwa wa maana sana kwa Ahabu kuliko kuonyesha rehema, haki, ao huruma. Upumbavu wa pili: Kwa kumuambia Eliya, “Ewe adui yangu,” Ahabu alionyesha chuki kwa mutu aliyekuwa rafiki ya Yehova Mungu na ambaye angemusaidia ageuke na kuacha matendo yake mabaya.

Tunaweza kujifunza mambo ya maana kutokana na upumbavu wa Ahabu. Tunapaswa kukumbuka sikuzote kwamba Yehova anaona mambo yote. Kwa kuwa yeye ni Baba mwenye upendo, anaona wakati tunaacha kufanya mambo yaliyo sawa, na anataka sana kutuona tunabadilisha matendo yetu mabaya. Ili kutusaidia, anatumia mara nyingi marafiki wake, ni kusema, wanadamu waaminifu ambao, kama vile Eliya, wanawapelekea wanadamu wenzao maneno ya Mungu. Linaweza kuwa kosa kabisa kuwaona marafiki wa Mungu kuwa maadui wetu!​—Zaburi 141:5.

Umufikirie Eliya katika akili yako akimujibu Ahabu hivi: “Nimekupata.” Alimupata Ahabu katika maana ya kwamba alijua alikuwa mutu wa namna gani, ni kusema, mwizi, muuaji, na muasi mbele za Yehova Mungu. Iliomba ujasiri mukubwa ili kubishana uso kwa uso na mutu huyo muovu! Eliya aliendelea kumutangazia Ahabu hukumu ya Mungu. Yehova aliona mambo yote yaliyokuwa yakitendeka, uovu wa familia ya Ahabu ulikuwa unaenea kwa watu wote. Kwa hiyo, Eliya alimuambia Ahabu kwamba Mungu aliamuru ‘kufagia kabisa,’ ni kusema, kuharibu kabisa familia ya kifalme ya Ahabu. Yezebeli naye angehukumiwa.​—1 Wafalme 21:20-26.

Eliya hakusema kwa muzaha kwamba watu wageuke na kuacha mwenendo wao mubaya wa ukosefu wa haki. Lakini leo, ni jambo jepesi kuambia watu kwa muzaha waache kutenda mambo mabaya. Habari hiyo ya Biblia inatukumbusha kwamba Yehova Mungu anaona mambo yanayotendeka lakini pia analeta hukumu ya haki kwa wakati wake wenye kufaa. Neno lake linatuhakikishia kwamba siku inakuja ambayo atamaliza ukosefu wa haki milele! (Zaburi 37:10, 11) Lakini unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, Mungu anahukumu watu kwa kuwaazibu tu? Je, anawaonyesha pia rehema anapowahukumu?’

“JE, UMEONA JINSI AMBAVYO AHABU AMEJINYENYEKEZA?”

Inawezekana Eliya alishangaa na namna Ahabu alivyotenda alipoambiwa juu ya hukumu ya Mungu. Habari hiyo inasema hivi: “Mara tu Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa nguo za magunia mwilini mwake; naye akaanza kufunga, akaendelea kulala katika nguo za magunia, akatembea kwa huzuni.” (1 Wafalme 21:27) Je, Ahabu alionyesha kwamba ametubu kwa kufanya hivyo?

Tunaweza kusema kwamba kwa kufanya hivyo, alionyesha alama fulani za kutubu. Ahabu alijinyenyekeza, mutu mwenye kiburi na mwenye majivuno hawezi kufanya hivyo. Lakini, je, alitubu kwelikweli? Fikiria Mufalme Ahabu kwa kumulinganisha na Manase, mufalme aliyetawala baadaye na aliyekuwa muovu zaidi kumupita. Wakati Yehova alimuazibu Manase, mwanaume huyo alijinyenyekeza, na akamuomba Yehova amusaidie. Lakini alifanya zaidi ya hilo. Alibadilisha kabisa njia yake ya kuishi kwa kuondoa sanamu zote alizokuwa amesimamisha, akafanya bidii kumutumikia Yehova, na hata akawatia watu moyo wafanye kama yeye. (2 Mambo ya Nyakati 33:1-17) Je, tunafikiri Ahabu naye alitenda hivyo? Jambo la kuhuzunisha ni kwamba hakutenda hivyo.

Je, Yehova aliona kwamba Ahabu alionyesha huzuni ya waziwazi kama vile Manase? Yehova alimuambia Eliya hivi: ‘Je, umeona jinsi ambavyo Ahabu amejinyenyekeza kwa ajili yangu? Kwa sababu amejinyenyekeza kwa ajili yangu, sitauleta ule musiba katika siku zake. Katika siku za mwana wake nitauleta musiba ule juu ya nyumba yake.’ (1 Wafalme 21:29) Je, Yehova alimusamehe Ahabu? Hapana, angepata rehema ya Mungu ikiwa tu angetubu kwelikweli. (Ezekieli 33:14-16) Lakini kwa sababu Ahabu alijuta kwa kiasi fulani, Yehova alimuonyesha rehema kwa kiasi kilicholingana na kujuta kwake. Ahabu angeepushwa kuona namna familia yake yote ingeweza kuharibiwa.

Lakini, hukumu ya Yehova juu ya mutu huyo haikubadilika. Baadaye Yehova alizungumuza na malaika zake juu ya njia nzuri ya kumudanganya Ahabu ili aende katika vita ambako angekufia. Muda mufupi kisha hapo, hukumu ya Yehova juu ya Ahabu ilitimizwa. Ahabu aliumizwa kwenye vita, akatokwa na damu nyingi katika gari lake mupaka akakufa. Habari hiyo inatoa maelezo haya yenye kuhuzunisha: Wakati gari la kifalme lilioshwa, imbwa fulani walilamba damu ya mufalme. Damu ya mufalme ilipolambwa hivyo waziwazi, maneno haya ya Yehova ambayo Eliya alimuambia Ahabu yalitimia: ‘Mahali ambapo imbwa waliilamba damu ya Nabothi, imbwa watailamba damu yako.’​—1 Wafalme 21:19; 22:19-22, 34-38.

Kufa kwa Ahabu kulimuhakikishia Eliya, Elisha, na waaminifu wengine wote kati ya watu wa Mungu kwamba Yehova hakusahau ujasiri na imani ya Nabothi. Mungu wa haki hakose kuleta hata kidogo azabu juu ya watu waovu, hata akawie ao asikawie; na hakose kuonyesha rehema katika hukumu zake ikiwa kuna musingi wa kufanya hivyo. (Hesabu 14:18) Hilo lilikuwa somo kubwa kwa Eliya, ambaye alikuwa amevumilia ukosefu wa haki kwa makumi ya miaka katika utawala wa mufalme huyo muovu! Je, wewe pia umekwisha kutendewa bila haki? Je, unatamani sana kuona wakati ambapo Mungu atarekebisha mambo? Ni vizuri uige imani ya Eliya. Yeye na rafiki yake Elisha, waliendelea kutangaza ujumbe mbalimbali wa Mungu, wakivumilia ukosefu wa haki.

^ Yehova alitokeza miaka tatu na nusu ya ukosefu wa mvua ili kuonyesha kwamba Baali hakuwa na uwezo wowote. Watu walikuwa wanaabudu Baali kuwa mungu aliyeleta mvua na aliyefanya udongo utoe chakula kingi. (1 Wafalme, sura ya 18) Soma habari yenye kichwa “Igeni Imani Yao” katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 1 Mwezi wa 1 na la tarehe 1 Mwezi wa 4, 2008.

^ Labda Yezebeli aliogopa kwamba watoto wa Nabothi ndio wangeriti shamba hilo la mizabibu, ndiyo maana alisukumwa kuwaua pia. Ili kujua sababu gani Mungu anaruhusu matendo kama hayo ya kuwaonea wengine, soma habari yenye kichwa “Wasomaji Wetu Wanauliza” katika gazeti hili.