Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA MOJA

Alikesha, na pia Alingojea

Alikesha, na pia Alingojea

1, 2. Ni kazi gani isiyopendeza ambayo Eliya anapaswa kwanza kutimiza, na namna gani yeye na Ahabu ni watu wawili walio tofauti kabisa?

ELIYA anatamani sana kuwa peke yake ili kusali kwa Baba yake wa mbinguni. Lakini watu wengi wanamuzunguka nabii huyo wa kweli; wametoka tu kujionea namna alivyosali na kufanya moto ushuke kutoka mbinguni, na wengi wao bila shaka wanataka sana awabariki. Eliya anataka kupanda juu kwenye Mulima Karmeli ili aweze kumukaribia Yehova Mungu katika sala kwa kipekee, lakini mbele ya kufanya hivyo ana kazi fulani isiyopendeza ambayo anapaswa kwanza kutimiza: anapaswa kuzungumuza na Mufalme Ahabu.

2 Eliya na Ahabu ni watu wawili walio tofauti kabisa. Ahabu, anayevalia mavazi ya kifalme, ni muasi-imani anayeshawishiwa upesi, mutu mwenye tamaa sana. Eliya anavalia vazi linaloonyesha kama yeye ni nabii, vazi lisilo na mambo mengimengi, lakini lenye kuwa nguvu, labda limetengenezwa kwa ngozi ya munyama ao kwa manyoya ya ngamia ao ya mbuzi. Ni mwanaume hodari sana, mwaminifu na mwenye imani. Mambo ambayo yanafanyika siku hiyo yamefunua sana tofauti kati ya wanaume hao wawili.

3, 4. (a) Sababu gani siku hiyo ni siku mbaya kwa Ahabu na waabudu wengine wa Baali? (b) Tutapata majibu ya maulizo gani?

3 Siku hiyo Ahabu na waabudu wengine wa Baali wanapatishwa haya sana. Dini ya kipagani inayotetewa na Ahabu na pia bibi yake, Malkia Yezebeli, katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi, imepigwa pigo kali. Imeonyeshwa wazi kwamba Baali ni mungu wa uongo. Mungu huyo asiye na uzima alishindwa kabisa kuwasha tu moto kidogo ili kujibu sala ya manabii wake waliocheza​-cheza kama watu wa wazimu, na kufanya sherehe za kujikata​-kata na kujitoa damu. Baali hakuwalinda wale makuhani wake 450 wasipatwe na hukumu waliostahili, ni kusema, kuuawa. Mungu huyo wa uongo alikuwa mwenye kushindwa kuhusu jambo lingine pia, na kushindwa huko kulikuwa karibu kuonyeshwa wazi. Kwa miaka zaidi ya mitatu, manabii wa Baali walimuomba mungu wao huyo afanye mvua inyeshe ili taabu imalizike katika inchi, lakini Baali alishindwa kufanya hivyo. Lakini, bila kukawia, Yehova ataonyesha kuwa yeye ndiye Mungu wa kweli kwa kufanya mvua inyeshe.—1 Fal. 16:30–17:1; 18:1-40.

4 Lakini, Yehova atafanya hivyo wakati gani? Eliya atajiendesha namna gani anapongojea Yehova atende? Na namna mwanaume huyo mwenye imani anavyojiendesha, inaweza kutufundisha nini? Acha tupate majibu ya maulizo hayo tunapochunguza habari hii.—Soma 1 Wafalme 18:41-46.

Alingojea Katika Sala

5. Eliya anamuambia Ahabu afanye nini, na je, matukio ya siku hiyo yamemufundisha Ahabu somo fulani?

5 Eliya anamukaribia Ahabu na kumuambia hivi: ‘Panda, kula na kunywa; kwa sababu kuna kishindo cha machafuko ya mvua kubwa.’ Je, matukio ya siku hiyo yamemufundisha mufalme huyo muovu somo fulani? Biblia haiseme waziwazi juu ya jambo hilo, hata hivyo, hatuone maneno yoyote yanayoonyesha kwamba anatubu, wala kwamba anamuomba nabii Eliya amusaidie kumukaribia Yehova ili amuombe musamaha. Habari inasema tu kwamba, Ahabu ‘alipanda zake ili kula na kunywa.’ (1 Fal. 18:41, 42) Sasa Eliya naye anafanya nini?

6, 7. Eliya anasali kuhusu nini, na sababu gani?

6 “Naye Eliya akapanda juu ya Mulima Karmeli na kuanza kuchutama chini, akaweka uso wake katikati ya magoti yake.” Wakati Ahabu anaenda kula na kunywa, Eliya yeye anapata nafasi ya kusali kwa Baba yake wa mbinguni. Eliya anainamisha kichwa chake chini sana, hivi kwamba uso wake unakaribia magoti yake, jambo hilo linaonyesha unyenyekevu kabisa. Kwa nini anainama hivyo? Jibu haliko mbali. Katika andiko la Yakobo 5:18, Biblia inatuambia kwamba Eliya alikuwa anasali ili mvua inyeshe. Bila shaka, yeye yuko juu ya Mulima Karmeli anaposali.

Sala za Eliya zilionyesha kama tamaa yake ilikuwa kwamba maopenzi ya Mungu yafanyike kwanza

7 Yehova alikuwa amekwisha kumuambia hivi: ‘Nimeazimia kuleta mvua juu ya uso wa inchi.’ (1 Fal. 18:1) Kwa hiyo, Eliya anasali mapenzi ya Yehova yatimie; miaka elfu moja hivi baadaye, Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivyohivyo.—Mt. 6:9, 10.

8. Mufano wa Eliya unatufundisha nini kuhusu sala?

8 Mufano wa Eliya unatufundisha mambo mengi kuhusu sala. Katika sala yake, Eliya anahangaikia kwanza kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu. Sisi pia tunaposali, ni vizuri tukumbuke kwamba, ‘Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake [Mungu], yeye anatusikia.’ (1 Yoh. 5:14) Kwa hiyo, ni lazima tujue kwanza mapenzi ya Mungu ni nini ili sala zetu zikubaliwe. Hiyo ni sababu inayopaswa kutusukuma kujifunza Biblia kila siku katika maisha yetu. Kwa kuwa watu wa inchi yake walikuwa wanateseka kwa sababu ya hali hiyo ya kukosa mvua, Eliya pia anataka hali hiyo imalizike. Inaonekana Eliya ni mwenye shukrani sana moyoni kisha kuona muujiza ambao Yehova ametimiza siku hiyo. Sisi pia sala zetu zinapaswa kuonyesha kwamba tunawahangaikia wengine na kwamba sisi ni wenye shukrani sana moyoni.​—Soma 2 Wakorintho 1:11; Wafilipi 4:6.

Alikuwa na Imani na Alikesha

9. Eliya anamutuma mutumishi wake kufanya nini, na Eliya anaonyesha sifa gani mbili ambazo tutazungumuzia?

9 Eliya ni mwenye kuwa na imani kwamba Yehova atafanya mvua inyeshe, lakini hajue ikiwa atafanya hivyo wakati gani. Kwa hiyo, anafanya nini anapongojea? Habari inasema hivi: “Akamuambia mutumishi wake: Enda juu, tafazali. Tazama upande wa bahari. Basi akaenda juu, akatazama na kisha akasema: ‘Hakuna kitu chochote.’ Naye [Eliya] akaendelea kusema, ‘Rudi,’ mara saba.” (1 Fal. 18:43) Mufano huo wa Eliya unatufundisha mambo mawili. Jambo la kwanza, nabii huyo alikuwa na imani kabisa. Na jambo la pili, aliendelea kukesha, na pia alingojea.

Eliya anaendelea kutafuta sana alama yoyote inayoonyesha kwamba Yehova iko karibu kutenda

10, 11. (a) Namna gani Eliya anaonyesha kama iko hakika kwamba Yehova atatimiza ahadi yake? (b) Namna gani tunaweza kuwa na imani kama hiyo?

10 Kwa kuwa Eliya ni mwenye kuwa na imani kama Yehova atatimiza ahadi yake, anaendelea kutafuta sana alama yoyote inayoonyesha kwamba Yehova iko karibu kutenda. Ndio sababu anamutuma mutumishi wake aende mahali pa juu zaidi, atazame mbali zaidi ili kuona ikiwa kuna alama yoyote yenye kuonyesha kama mvua inataka kunyesha. Lakini, mutumishi huyo anaporudi, anamutolea ripoti hii isiyofurahisha: “Hakuna kitu chochote.” Anga halina mawingu. Lakini, unaona jambo fulani la kushangaza? Kumbuka, tayari Eliya alikuwa amekwisha kumuambia Mufalme Ahabu kwamba “Kuna kishindo cha machafuko ya mvua kubwa.” Sababu gani nabii huyo alisema hivyo ingawa hakukuwa na mawingu yoyote ya mvua yenye kuonekana?

11 Eliya anajua kwamba ahadi hiyo ni neno la Yehova, na pia anajua kwamba yeye ni nabii wake. Kwa hiyo, yeye iko hakika kabisa kwamba Mungu wake atatimiza Neno lake, ni kusema ahadi yake. Eliya ni mwenye uhakika sana hivi kwamba kwake ni kama tayari amekwisha kusikia kishindo cha mvua kubwa. Hilo linatukumbusha yale Biblia inasema juu ya Musa: ‘Aliendelea kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana.’ Je, wewe pia unamuona Mungu kuwa si mutu wa kuwazia tu? Mungu anatupatia sababu za kutosha ili tuweze kumuamini yeye na kuamini ahadi zake kama Eliya.​—Ebr. 11:1, 27.

12. Ni nini inayoonyesha kwamba Eliya anaendelea kukesha, na anafanya nini anapopewa habari ya wingu ndogo linalopanda kutoka katika bahari?

12 Sasa acha tuone namna Eliya alivyokesha. Anatuma mutumishi wake aende kutazama alama, si mara moja ao mara mbili tu, lakini mara saba! Labda mutumishi huyo anachoka kwa kutumwa tena na tena, lakini Eliya yeye anatamani sana kuona alama, na havunjike moyo. Mwishowe, kisha safari ya saba, mutumishi wake anakuja kumuambia: ‘Tazama! Kuna wingu ndogo kama kiganja cha mukono wa mwanadamu linalopanda kutoka katika bahari.’ Unaweza kuona katika akili yako namna mutumishi huyo anavyonyoosha mukono wake na kuonyesha kiganja chake ili kupima ukubwa wa wingu ndogo ambalo lilikuwa linapanda kutoka katika ile Bahari Kubwa? Labda mutumishi huyo anaona kuwa wingu hilo si jambo la maana kabisa. Lakini, Eliya yeye, anaona jambo hilo tofauti. Na sasa bila kukawia anamuambia mutumishi wake hivi: ‘Panda, umuambie Ahabu, Funga gari! Nawe ushuke ili mvua kubwa isikuzuie!’—1 Fal. 18:44.

13, 14. (a) Eliya aliendelea kukesha, namna gani tunaweza kumuiga? (b) Ni sababu gani tulizo nazo zinazopaswa kutuchochea kutenda kwa haraka?

13 Katika jambo hili pia, Eliya alituwekea mufano muzuri sana. Sisi pia tunaishi wakati ambapo Mungu anakaribia kutenda ili kutimiza kusudi lake. Eliya alingojea mwisho wa kipindi cha kukosa mvua; leo watumishi wa Mungu wanangojea mwisho wa ulimwengu huu muovu. (1 Yoh. 2:17) Tunapaswa kuendelea kukesha kama Eliya mupaka Yehova Mungu atakapotenda. Yesu, Mwana wa Mungu, anashauri wafuasi wake hivi: ‘Kwa hiyo, muendelee kukesha kwa sababu hamujue ni siku gani Bwana yenu atakuja.’ (Mt. 24:42) Je, Yesu alitaka kusema kwamba wafuasi wake hawangejua hata kidogo kama mwisho unakaribia? Hapana, kwa kuwa alifasiria kwa kirefu namna hali za ulimwengu zingekuwa mbele ya mwisho. Kila mumoja wetu anaweza kujionea utimizo wa alama hiyo yenye mambo mengi ya ‘mwisho wa ulimwengu huu muovu.’—Soma Mathayo 24:3-7.

Wingu ndogo tu lilitosha ili kumusadikisha Eliya kwamba Yehova anakaribia kutenda. Alama yenye mambo mengi ya siku za mwisho inatupatia sababu zinazotuchochea kutenda kwa haraka

14 Kila sehemu ya ishara hiyo inatutolea ushahidi wenye nguvu na wenye kusadikisha. Je, alama hizo zinatosha ili kutuchochea tutende kwa haraka katika utumishi wa Yehova? Wingu ndogo tu lililoonekana kwa mbali lilitosha ili kumusadikisha Eliya kwamba Yehova anakaribia kutenda. Je, nabii huyo mwaminifu alivunjika moyo?

Yehova Analeta Kitulizo na Baraka

15, 16. Ni mambo gani yanaanza kutokea kwa haraka sana, na labda Eliya anatumainia Ahabu afanye nini?

15 Biblia inatuambia hivi: “Na ikawa kwamba wakati huo mbingu zikatiwa giza kwa mawingu na upepo na mvua kubwa sana ikaanza kunyesha. Na Ahabu akaendelea kupanda gari, akaenda zake Yezreeli.” (1 Fal. 18:45). Mambo yanaanza kutokea kwa haraka sana. Mutumishi wa Eliya anapomutolea Ahabu ujumbe wa nabii huyo, lile wingu ndogo linaongezeka kuwa mawingu mengi, yanajaa anga na kunakuwa giza. Upepo mukali unavuma. Aah! kisha miaka mitatu na nusu, mvua inanyeshea tena udongo wa Israeli! Udongo wenye kukauka unakunywa kabisa. Mvua inapokuwa kubwa kabisa, muto wa Kishoni unajaa, bila shaka maji yake yanasafisha damu ya manabii wa Baali waliouawa. Waisraeli waasi wanapewa pia nafasi ya kuondoa na kusafisha uchafu wa ibada ya Baali katika inchi.

“Mvua kubwa sana ikaanza kunyesha”

16 Bila shaka, Eliya anatumaini kwamba watafanya hivyo! Labda pia anajiuliza ikiwa Ahabu atafanya nini kwa sababu ya matukio hayo. Je, atatubu sasa na kujisafisha kutoka katika uchafu wa ibada ya Baali? Mambo yanayotokea siku hiyo yangemupa Ahabu sababu ya kufanya mabadiliko hayo. Kwa kweli, hatuwezi kujua ni nini Ahabu anafikiria kisha kuona mambo hayo yote. Habari inasema tu kwamba mufalme ‘aliendelea kupanda gari, akaenda zake Yezreeli.’ Je, amejifunza jambo fulani? Je, ameazimia kubadilika? Mambo yaliyotokea baadaye yanaonyesha kwamba hakufanya hivyo. Lakini, inaonekana kwamba kwa siku hiyo mambo hayajakwisha bado, iwe kwa Ahabu ao kwa Eliya.

17, 18. (a) Ni nini inayotokea kwa Eliya kwenye barabara ya Yezreeli? (b) Sababu gani kukimbia kwa Eliya kutoka Karmeli mupaka Yezreeli ni jambo la ajabu? (Soma pia maelezo yaliyo chini.)

17 Nabii wa Yehova anashika njia yake, anafuata barabara ileile ambayo Ahabu alipitia. Ni safari ndefu, ambayo anapaswa kufanya kwa miguu, katika giza na mvua. Lakini, jambo fulani la ajabu linatokea.

18 ‘Na mukono wa Yehova ukawa juu ya Eliya, hivi kwamba akajifunga viuno, naye akakimbia mbele ya Ahabu mupaka Yezreeli.’ (1 Fal. 18:46) Ni wazi kabisa, ‘mukono wa Yehova’ uko pamoja na Eliya na unatenda kwa njia inayopita uwezo wa mwanadamu. Fikiria jambo hili: Yezreeli inapatikana kwenye kilometre 30 hivi, na Eliya si kijana. * Wazia namna nabii huyo anafunga mavazi yake marefu kwenye kiuno ili miguu yake isizuiliwe na jambo lolote, kisha anakimbia kabisa katika barabara hiyo yenye kujaa maji ya mvua, anafikia gari la farasi la mufalme, analipita na kuliacha kabisa!

19. (a) Nguvu na uwezo ambao Mungu alimupatia Eliya vinatukumbusha unabii gani mbalimbali? (b) Wakati Eliya anakimbia kutoka Karmeli mupaka Yezreeli, ni jambo gani anajua kwa uhakika?

19 Eliya alijisikia kuwa mwenye kubarikiwa kabisa! Bila shaka alichangamuka sana kujisikia kuwa na nguvu hivyo, na afya na uwezo huo ambao labda hata ulipita ule aliokuwa nao alipokuwa kijana. Hilo linaweza kutukumbusha unabii mbalimbali unaohakikisha kwamba katika dunia Paradiso inayokuja, watu waaminifu watakuwa na nguvu na pia afya yenye kukamilika. (Soma Isaya 35:6; Lu. 23:43) Wakati Eliya alikuwa anakimbia katika barabara hiyo yenye maji ya mvua, bila shaka alijua kama anakubaliwa na Baba yake, yule Mungu wa kweli, Yehova!

20. Tunapaswa kufanya nini ili kupata baraka za Yehova?

20 Yehova anataka sana kutubariki. Acha basi tufanye yetu yote ili kupata baraka hizo; kujikaza hivyo si kwa bure. Tunapaswa kukesha kama Eliya, maana yake, kuchunguza kwa uangalifu alama zinazoonyesha kabisa kwamba karibuni Yehova atatenda katika nyakati hizi za hatari na za mwisho. Kama Eliya, tuna kila sababu ya kutumaini kabisa ahadi za Yehova, “Mungu wa ukweli.”—Zab. 31:5.

^ fu. 18 Muda mufupi kisha hapo, Yehova anamuomba Eliya amufundishe Elisha, ambaye ilisemekana baadaye kwamba ni yeye aliyekuwa ‘anamiminia Eliya maji kwenye mikono.’ (2 Fal. 3:11) Elisha alikuwa mutumishi wa Eliya, ni wazi kwamba alimusaidia nabii huyo muzee kwa kila jambo alilohitaji.

[Picha katika ukurasa wa 93]

Sala za Eliya zilionyesha kama tamaa yake ilikuwa kwamba mapenzi ya Mungu yafanyike kwanza