Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SOMO LA 6

Wakati Mutoto Anazaliwa, Mambo Yanabadilika

Wakati Mutoto Anazaliwa, Mambo Yanabadilika

‘Wana ni uriti kutoka kwa Yehova.’​—Zaburi 127:3

Kuzaliwa kwa mutoto kunaweza kuleta furaha kubwa na wasiwasi kwa bibi na bwana. Kwa sababu ninyi ni wazazi wapya, munaweza kushangaa kuona kwamba munatumia wakati na nguvu zenu nyingi ili kumutunza mutoto ambaye mumezaa. Kukosa usingizi na mabadiliko katika hali ya moyoni, mambo hayo yanaweza kuleta matatizo katika ndoa yenu. Ninyi wote wawili munapaswa kufanya mabadiliko fulani ili kumutunza mutoto wenu na kulinda ndoa yenu. Namna gani kanuni za Biblia zinaweza kuwasaidia?

1 JUA KAMA MUTOTO ANALETA MABADILIKO KATIKA NDOA

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: ‘Upendo ni wenye [uvumilivu] na wenye fazili.’ Tena, upendo ‘hautafute faida zake wenyewe, hauchokozeki.’ (1 Wakorintho 13:4, 5) Ni kawaida wewe kama mama mupya umuhangaikie sana mutoto wako. Lakini, bwana yako anaweza kuanza kufikiri kama haumuhangaikie tena, kwa hiyo usisahau kama yeye pia anahitaji umuhangaikie. Kwa uvumilivu na upole, unaweza kumufanya ajisikie kuwa yeye ni wa lazima na kwamba yeye pia anaweza kusaidia kumutunza mutoto wenu.

‘Enyi waume, muendelee kukaa nao vivyo hivyo kulingana na ujuzi.’ (1 Petro 3:7) Jua kama bibi yako atatumia nguvu nyingi ili kumutunza mutoto wenu. Sasa ana madaraka mapya na yanaweza kumuchokesha, kumuhangaisha katika akili, na hata anaweza kushuka moyo. Wakati fulani, anaweza hata kukukasirikia, lakini jaribu kutulia, kwa sababu ‘asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanaume mwenye nguvu.’ (Methali 16:32) Onyesha utambuzi, na umutegemeze.​—Methali 14:29.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Wewe Baba: Saidia bibi yako kumutunza mutoto wenu, hata wakati wa usiku. Punguza wakati ambao unapitisha katika mambo mengine ili uweze kupitisha wakati wa kutosha pamoja na bibi yako na mutoto wenu

  • Wewe Mama: Wakati bwana yako anataka kukusaidia kumutunza mutoto, kubali akusaidie. Ikiwa hafanye muzuri kabisa, usimuchambue-chambue, lakini umuonyeshe kwa upole namna angepaswa kufanya

2 FANYA UHUSIANO WENU UWE NGUVU

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: ‘Watakuwa mwili mumoja.’ (Mwanzo 2:24) Hata ikiwa mumekuwa na mushiriki mupya katika familia yenu, ni kusema, mutoto wenu, usisahau kama wewe na bibi ao bwana yako mungali ‘mwili mumoja.’ Kwa hiyo, fanya uhusiano wenu uendelee kuwa guvu.

Wewe bibi, umushukuru bwana yako wakati anakusaidia na kukutegemeza. Maneno yako ya shukrani yanaweza kuwa dawa yenye ‘kuponya.’ (Methali 12:18) Wewe bwana, umuambie bibi yako kama unamupenda sana na kwamba ni mutu wa lazima sana kwako. Umusifu kwa sababu ya mambo ambayo anafanya ili kutunza familia.​—Methali 31:10, 28.

‘Kila mumoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mutu mwingine.’ (1 Wakorintho 10:24) Umutendee mema bibi ao bwana yako sikuzote. Mutafute wakati wa kuzungumuza, kila mumoja apongeze mwengine na kumusikiliza. Musinyimane kitendo cha ndoa. Fikiria mahitaji ya bibi ao bwana yako. Biblia inasema hivi: ‘Musiwe mukinyimana haki hiyo, ila kwa makubaliano.’ (1 Wakorintho 7:3-5) Kwa hiyo, muzungumuzie waziwazi jambo hilo ninyi wawili. Kuwa muvumilivu na kumuelewa mwenzako kutafanya uhusiano wenu uwe nguvu.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Usisahau kupitisha wakati pamoja na bibi ao bwana yako

  • Fanya mambo madogo-madogo yanayomufanya bibi ao bwana yako ajisikie kuwa anapendwa, kama vile kumutumia ujumbe mufupi ao kumupatia zawadi ndogo

3 MUZOEZE MUTOTO WAKO MUDOGO

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: ‘Tangu utoto muchanga umeyajua maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.’ (2 Timotheo 3:15) Panga namna utamufundisha mutoto wako. Yeye ana uwezo mukubwa wa kujifunza, hata mbele ya kuzaliwa. Wakati angali ndani ya tumbo, mutoto wako anaweza kutambua sauti yako na kujisikia namna unajisikia. Musomee habari fulani wakati angali mudogo. Hata ikiwa haelewe mambo ambayo unamusomea, hilo linaweza kumusaidia afurahie kusoma wakati atakuwa mukubwa.

Hata ikiwa ni mudogo, anaweza kusikia wakati unazungumuza juu ya Mungu. Muache asikilize sala zako. (Kumbukumbu la Torati 11:19) Hata wakati munacheza pamoja, zungumuza naye juu ya mambo ambayo Mungu ameumba. (Zaburi 78:3, 4) Kadiri mutoto wako anaendelea kukomaa, ataona namna unamupenda Yehova na yeye pia atajifunza kumupenda.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Muombe Mungu akupatie hekima ili kumufundisha mutoto wako

  • Rudilia-rudilia maneno na mawazo kwa mutoto wako, kwa hiyo ataanza kujifunza mbele ya wakati