Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Hasira?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Hasira?

Jibu la Biblia

 Biblia inafundisha kwamba hasira isiyodhibitiwa ina madhara kwa mtu mwenyewe na pia kwa watu wanaomzunguka. (Methali 29:22) Ingawa nyakati fulani huenda kukawa na sababu zinazofaa za kukasirika, Biblia inasema kwamba wale wanaoendelea kuwa na “milipuko ya hasira,” hawatapata wokovu. (Wagalatia 5:​19-​21) Biblia ina kanuni zinazoweza kumsaidia mtu kukabiliana na hasira.

 Je, hasira ni mbaya nyakati zote?

 Hapana. Kuna nyakati ambapo huenda kukawa na sababu zinazofaa za kukasirika. Kwa mfano, mwanamume mwaminifu Nehemia ‘alikasirika sana’ alipojua kwamba waabudu wenzake walikuwa wakikandamizwa.​—Nehemia 5:6.

 Nyakati fulani, Mungu hukasirika. Kwa mfano, watu wake wa kale walipovunja makubaliano ya kumwabudu yeye peke yake na wakaanza kutumikia miungu ya uwongo, ‘hasira ya Yehova iliwaka dhidi yao.’ (Waamuzi 2:​13, 14) Hata hivyo, hasira si sehemu kuu ya utu wa Yehova Mungu. Sikuzote hasira yake huwa ya haki, naye huidhibiti.​—Kutoka 34:6; Isaya 48:9.

 Ni wakati gani ambapo ni vibaya kuwa na hasira?

 Hasira ni mbaya wakati ambapo haidhibitiwi au hakuna sababu inayofaa ya kuionyesha, na mara nyingi inakuwa hivyo wanadamu wasio wakamilifu wanapokasirika. Kwa mfano:

  •   Kaini ‘aliwaka hasira’ Mungu alipokataa dhabihu yake. Kaini aliruhusu hasira yake ikue hivi kwamba akamuua ndugu yake.​—Mwanzo 4:​3-8.

  •   Nabii Yona ‘alikasirika sana’ Mungu alipowaonyesha Waninawi rehema. Mungu alimrekebisha Yona, akionyesha kwamba hakuwa na “sababu nzuri ya kuwaka hasira.”​—Yona 3:10–​4:​1, 4, 11. a

 Mifano hiyo inaonyesha kwamba kwa wanadamu wasio wakamilifu, “hasira ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.”​—Yakobo 1:​20.

 Unaweza kukabilianaje na hasira?

  •   Tambua hatari ya hasira isiyodhibitiwa. Huenda wengine wakafikiri kwamba kuonyesha hasira ni ishara ya kwamba wao si dhaifu. Hata hivyo, kwa kweli mtu ambaye hawezi kudhibiti hasira yake ana udhaifu mkubwa. “Kama jiji lililobomolewa, lisilo na ukuta, ndivyo alivyo mtu asiyeweza kuidhibiti hasira yake.” (Methali 25:28; 29:11) Kwa upande mwingine, tunapositawisha uwezo wa kudhibiti hasira tunaonyesha kwamba sisi si dhaifu na tuna ufahamu. (Methali 14:29) Biblia inasema hivi: “Mtu asiyekasirika upesi ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu.”​—Methali 16:32.

  •   Dhibiti hasira kabla haijakufanya utende kwa njia utakayojutia. Zaburi 37:8 inasema hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu; usikasirike na kuanza kutenda uovu.” Ona kwamba tunapokuwa na hasira, tunaweza kuchagua​—tunaweza kuchagua kuiacha kabla ituongoze “kutenda uovu.” Kama Waefeso 4:​26 inavyosema, “iweni na hasira, lakini msitende dhambi.”

  •   Ikiwezekana, ondoka unapoanza kupandwa na hasira. Biblia inasema hivi: “Kuanzisha vita ni kama kufungua lango la mafuriko; kabla ugomvi haujalipuka, ondoka.” (Methali 17:14) Ingawa ni jambo la hekima kutatua kutoelewana upesi, huenda wewe na yule mtu mwingine mkahitaji kupoa kwanza kabla ya kuzungumzia jambo hilo kwa utulivu.

  •    Pata habari kamili. “Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake,” inasema Methali 19:11. Ni jambo la hekima kupata habari kamili kabla ya kufikia mkataa. Tunaposikiliza kwa makini pande zote za jambo, kuna uwezekano mkubwa kwamba hatutakasirika bila sababu inayofaa.​—Yakobo 1:​19.

  •    Sali upate amani ya akili. Sala inaweza kukusaidia kupata “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” (Wafilipi 4:7) Sala ni moja kati ya njia kuu tunazopata roho takatifu ya Mungu, ambayo inaweza kutokeza sifa kama amani, subira, na kujizuia.​—Luka 11:13; Wagalatia 5:​22, 23.

  •   Chagua marafiki wako kwa uangalifu. Tuna mwelekeo wa kuwa kama watu tunaoshirikiana nao. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Biblia inaonya hivi kwa sababu nzuri: “Usiwe na urafiki na mtu mwenye hasira kali wala kushirikiana na mtu anayekasirika upesi.” Kwa nini? “Ili usijifunze kamwe njia zake na kujitia mtegoni.”​—Methali 22:24, 25.

a Inaonekana kwamba Yona alikubali kurekebishwa na akaacha kuwa na hasira, kwa kuwa Mungu alimtumia kuandika sehemu ya Biblia inayoitwa kwa jina lake.