Hamia kwenye habari

Kusamehe Kunamaanisha Nini?

Kusamehe Kunamaanisha Nini?

Jibu la Biblia

 Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kusamehe” linamaanisha kihalisi “kuachilia,” kama wakati ambapo mtu anaamua kutodai malipo ya deni. Yesu alitumia ulinganisho huo alipowafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Luka 11:4) Vivyo hivyo, alipotoa mfano kuhusu yule mtumwa asiye na rehema, Yesu alilinganisha msamaha na kufuta deni.​—Mathayo 18:23-​35.

 Tunawasamehe wengine tunapoepuka kuweka kinyongo na kutodai malipo kwa sababu ya uchungu au hasara tuliyopata. Biblia inafundisha kwamba upendo usio na ubinafsi ndio msingi wa msamaha wa kweli, kwa kuwa upendo, “hauweki hesabu ya ubaya.”​—1 Wakorintho 13:4, 5.

Kusamehe hakumaanishi

  •   Kupuuza kosa. Biblia inawashutumu wale wanaosema kuwa matendo yasiyofaa hayana madhara au yanakubalika.​—Isaya 5:​20.

  •   Kutenda kana kwamba kosa halijafanywa. Mungu alimsamehe Mfalme Daudi dhambi nzito, lakini hakumlinda Daudi kutokana na madhara ya matendo yake. Mungu alimwongoza Daudi aandike kuhusu dhambi zake hivi kwamba zinakumbukwa hadi leo.​—2 Samweli 12:​9-​13.

  •   Kuwaruhusu wengine wakutumie vibaya. Kwa mfano, tuseme umemkopesha mtu pesa, naye anazitumia vibaya halafu anashindwa kukulipa kama alivyoahidi. Anasikitika sana na kuomba msamaha. Unaweza kumsamehe kwa kutoweka kinyongo, kutomkumbusha-kumbusha jambo hilo, na labda hata kufuta deni hilo. Hata hivyo, unaweza kuamua kutomkopesha pesa tena.​—Zaburi 37:21; Methali 14:15; 22:3; Wagalatia 6:7.

  •   Kusamehe bila msingi halali. Mungu hawasamehi watu wanaotenda dhambi kimakusudi na kwa ukatili na ambao hukataa kukubali makosa yao, kubadilika, na kuwaomba msamaha wale ambao wameumizwa. (Methali 28:13; Matendo 26:20; Waebrania 10:26) Watu hao wasiotubu huwa maadui wa Mungu, naye hatazamii tuwasamehe watu ambao yeye hawasamehi.​—Zaburi 139:21, 22.

     Namna gani ikiwa umetendewa kwa ukatili na mtu anayekataa kukuomba msamaha au hata kukubali kuwa amekosa? Biblia inatushauri hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Ingawa hutapuuza kosa lake, unaweza kukataa kuendelea kukasirika. Uwe na hakika kwamba Mungu atamtoza hesabu mtu huyo. (Waebrania 10:30, 31) Unaweza pia kufarijika kujua kwamba Mungu ataleta wakati ambapo hatutahisi tena maumivu au uchungu kwa sababu ya mambo yanayotulemea sasa.​—Isaya 65:17; Ufunuo 21:4.

  •   “Kusamehe” makosa ya kudhaniwa. Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kukubali kuwa hatukuwa na sababu ya kukasirika. Biblia inasema: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako, kwa maana kuudhika hukaa katika kifua cha wajinga.”​—Mhubiri 7:9.

Jinsi ya kusamehe

  1.   Kumbuka msamaha unahusisha nini. Si kupuuza kosa au kutenda kana kwamba hakuna kosa lililotendeka​—ni kuliachilia tu.

  2.   Tambua manufaa ya kusamehe. Kuondoa hasira na kutoweka kinyongo kunakusaidia kuwa mtulivu, kunaboresha afya yako, na kufanya uwe na furaha zaidi. (Methali 14:30; Mathayo 5:9) Jambo muhimu zaidi ni kwamba kuwasamehe wengine ndio msingi wa kusamehewa na Mungu makosa yetu wenyewe.​—Mathayo 6:​14, 15.

  3.   Uwe mwenye hisia mwenzi. Sisi sote si wakamilifu. (Yakobo 3:2) Kwa kuwa tunathamini sana tunaposamehewa, tunapaswa kuwasamehe wengine makosa yao.​—Mathayo 7:​12.

  4.   Uwe na usawaziko. Tunapokuwa na sababu ndogo ya kulalamika, tunaweza kufuata shauri hili la Biblia: “Endeleeni kuvumiliana.”​—Wakolosai 3:13.

  5.   Tenda upesi. Jitahidi kusamehe haraka iwezekanavyo badala ya kuacha hasira yako iendelee.​—Waefeso 4:26, 27.