Hamia kwenye habari

Ninaweza Kuipataje Dini ya Kweli?

Ninaweza Kuipataje Dini ya Kweli?

Jibu la Biblia

 Ili kuonyesha tofauti kati ya waabudu wa kweli na wa uwongo, Biblia inasema hivi: “Kwa matunda yao mtawatambua. Je, watu hukusanya zabibu kutoka kwenye miiba au tini kutoka kwenye michongoma?” (Mathayo 7:16) Kama tu unavyoweza kutofautisha kati ya mzabibu na mti wa miiba kutokana na mazao yake, ndivyo pia unavyoweza kutofautisha dini ya kweli na ya uwongo kwa matunda yake, au sifa zake.

  1.   Dini ya kweli inafundisha kweli inayotegemea Biblia, si falsafa za wanadamu. (Yohana 4:24; 17:17) Hiyo inatia ndani ukweli kuhusu nafsi na tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso. (Zaburi 37:29; Isaya 35:5, 6; Ezekieli 18:4) Pia, dini ya kweli haiogopi kufunua waziwazi uwongo wa kidini.—Mathayo 15:9; 23:27, 28.

  2.   Dini ya kweli inawasaidia watu wamjue Mungu, kutia ndani kuwafundisha kwamba jina lake ni Yehova. (Zaburi 83:18; Isaya 42:8; Yohana 17:3, 6) Haifundishi kwamba watu hawezi kumwelewa Mungu au kwamba hajali mambo ambayo wanadamu wanafanya; badala yake inafundisha kwamba yeye anataka tuwe na uhusiano naye.—Yakobo 4:8.

  3.   Dini ya kweli inakazia kwamba Mungu anamtumia Yesu Kristo kutupatia wokovu. (Matendo 4:10, 12) Wafuasi wake hutii amri za Yesu na wanajitahidi kufuata mfano wake.—Yohana 13:15; 15:14.

  4.   Dini ya kweli inakazia kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu. Wafuasi wake huwahubiria wengine kwa bidii kuhusu Ufalme huo.—Mathayo 10:7; 24:14.

  5.   Dini ya kweli huwatia moyo watu kuwapenda wenzao bila ubinafsi. (Yohana 13:35) Inawafundisha wafuasi wake kuwaheshimu watu wa makabila yote na inawakaribisha watu wa rangi, tamaduni, lugha, na malezi yote. (Matendo 10:34, 35) Wafuasi wake hawaendi vitani kwa kuwa wanawapenda wenzao.—Mika 4:3; 1 Yohana 3:11, 12.

  6.   Dini ya kweli haina viongozi wanaolipwa, na hakuna wafuasi wake wanaopewa majina ya cheo.—Mathayo 23:8-12; 1 Petro 5:2, 3.

  7.   Dini ya kweli haiungi mkono upande wowote wa mambo ya kisiasa. (Yohana 17:16; 18:36) Hata hivyo, wafuasi wake wanaheshimu na kutii serikali ya nchi yao, kupatana na amri hii ya Biblia: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.”—Marko 12:17; Waroma 13:1, 2.

  8.   Dini ya kweli ni sehemu ya maisha, si desturi tu. Wafuasi wake wanashikamana na viwango vya juu vya Biblia katika sehemu zote za maisha yao. (Waefeso 5:3-5; 1 Yohana 3:18) Hata hivyo, badala ya kuhisi kwamba wamenyimwa furaha, wafuasi wa dini ya kweli wanapata shangwe katika kumtumikia yule “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.

  9.   Wale walio katika dini ya kweli ni wachache. (Mathayo 7:13, 14) Mara nyingi, wafuasi wa dini ya kweli hupuuzwa, wanadhihakiwa, na kuteswa kwa kufanya mapenzi ya Mungu.—Mathayo 5:10-12.

Si lazima dini iwe ya kweli kwa sababu tu mimi ninaipenda

 Kuna hatari ya kuchagua dini kwa kutegemea tu jinsi ninavyohisi kuielekea. Biblia ilitabiri kuhusu wakati ambapo watu “watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.” (2 Timotheo 4:3) Tofauti na hilo, Biblia inatutia moyo tufuate “ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba,” hata ikiwa dini hiyo haipendwi na watu wengi.—Yakobo 1:27; Yohana 15:18, 19.