Hamia kwenye habari

Yesu Huokoa​—Jinsi Gani?

Yesu Huokoa​—Jinsi Gani?

Jibu la Biblia

 Yesu aliwaokoa wanadamu waaminifu alipotoa uhai wake kuwa dhabihu ya fidia. (Mathayo 20:28) Hivyo, Biblia inamwita Yesu “mwokozi wa ulimwengu.” (1 Yohana 4:​14) Pia inasema hivi: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo tunaweza kuokolewa.”​—Matendo 4:​12.

 Yesu ‘alionja kifo kwa ajili ya kila mtu’ anayemwamini. (Waebrania 2:9; Yohana 3:​16) Baada ya hapo, “Mungu alimfufua kutoka kwa wafu,” na Yesu akarudi mbinguni akiwa kiumbe wa roho. (Matendo 3:​15) Akiwa huko, Yesu anaweza “kuwaokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu sikuzote yuko hai ili kuwaombea.”​—Waebrania 7:​25.

Kwa nini tunahitaji Yesu atuombee?

 Sisi sote ni watenda dhambi. (Waroma 3:​23) Dhambi hututenganisha na Mungu, nayo hutokeza kifo. (Waroma 6:​23) Lakini Yesu hutenda kama “wakili” kwa ajili ya wale wanaodhihirisha imani katika dhabihu yake ya fidia. (1 Yohana 2:1, maelezo ya chini) Anawaombea, akimsihi Mungu asikilize sala zao na kuwasamehe dhambi kwa msingi wa dhabihu ya kifo cha Yesu. (Mathayo 1:​21; Waroma 8:​34) Mungu anatenda kupatana na maombi hayo yanayotolewa na Yesu kwa sababu yanapatana na mapenzi Yake. Mungu alimtuma Yesu duniani ili “ulimwengu uokolewe kupitia kwake.”​—Yohana 3:​17.

Je, tunahitaji tu kumwamini Yesu ili tuokolewe?

 Hapana. Ingawa lazima tumwamini Yesu ili tuokolewe, mengi zaidi yanahitajika. (Matendo 16:30, 31) Biblia inasema hivi: “Kama vile mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo, imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:​26) Ili tuokolewe tunapaswa:

  •   Kujifunza kumhusu Yesu na Baba yake, Yehova.​—Yohana 17:3.

  •   Kuwa na imani katika Yehova na Yesu.​—Yohana 12:44; 14:1.

  •   Kuonyesha imani kwa kutii amri zao. (Luka 6:​46; 1 Yohana 2:​17) Yesu alifundisha kwamba si kila mtu anayemwita “Bwana” atakayeokolewa bali ni wale tu ‘wanaofanya mapenzi ya Baba yake aliye mbinguni.’​—Mathayo 7:​21.

  •   Kuendelea kudhihirisha imani licha ya hali ngumu. Yesu alionyesha hilo ni muhimu aliposema: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—Mathayo 24:13.