Kulingana na Luka 6:1-49

  • Yesu ndiye “Bwana wa Sabato” (1-5)

  • Mtu aliyepooza mkono aponywa (6-11)

  • Mitume 12 (12-16)

  • Yesu afundisha na kuponya (17-19)

  • Furaha na ole (20-26)

  • Kuwapenda adui (27-36)

  • Acheni kuhukumu (37-42)

  • Mti hujulikana kwa matunda yake (43-45)

  • Nyumba iliyojengwa vizuri; nyumba isiyo na msingi imara (46-49)

6  Siku moja ya Sabato Yesu alipokuwa akipita katika mashamba ya nafaka, wanafunzi wake walikuwa wakivunja na kula masuke ya nafaka, + wakiyapukusa kwa mikono yao.+  Ndipo baadhi ya Mafarisayo wakauliza: “Kwa nini mnafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato?”+  Lakini Yesu akawajibu: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi wakati yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+  Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu akapokea mikate ya toleo,* akala na pia akawapa wanaume waliokuwa pamoja naye, mikate ambayo si halali kwa yeyote kula ila makuhani tu?”+  Kisha akawaambia: “Mwana wa binadamu ndiye Bwana wa Sabato.”+  Siku nyingine ya Sabato+ aliingia katika sinagogi, akaanza kufundisha. Kulikuwa na mtu aliyepooza mkono wa kulia.+  Waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimwangalia Yesu kwa makini ili waone kama angeponya katika siku ya Sabato, ili wapate sababu ya kumshtaki.  Hata hivyo, alijua mawazo yao,+ basi akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Inuka usimame hapa katikati.” Naye akainuka na kusimama hapo.  Kisha Yesu akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuuangamiza?”+ 10  Baada ya kuwatazama wote waliokuwapo, Yesu akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukapona. 11  Lakini wakakasirika sana, wakaanza kushauriana kuhusu jambo ambalo wangemtendea Yesu. 12  Siku moja, Yesu alienda mlimani kusali,+ naye akasali kwa Mungu usiku wote.+ 13  Kulipokucha akawaita wanafunzi wake na kuchagua 12 kati yao, ambao pia aliwaita mitume:+ 14  Simoni, ambaye pia alimwita jina Petro, Andrea ndugu yake, Yakobo, Yohana, Filipo,+ Bartholomayo, 15  Mathayo, Tomasi,+ Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni anayeitwa “mwenye bidii,” 16  Yuda mwana wa Yakobo, na Yuda Iskariote, aliyegeuka kuwa msaliti. 17  Yesu akashuka pamoja nao akasimama mahali tambarare, na kulikuwa na umati mkubwa wa wanafunzi wake, na umati mkubwa wa watu kutoka Yudea yote na Yerusalemu na eneo la pwani la Tiro na Sidoni, waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa. 18  Hata aliwaponya wale waliosumbuliwa na roho waovu. 19  Umati wote ulikuwa ukijaribu kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka+ na kuwaponya wote. 20  Akainua macho na kuwatazama wanafunzi wake na kusema: “Wenye furaha ni ninyi maskini, kwa sababu Ufalme wa Mungu ni wenu.+ 21  “Wenye furaha ni ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba.+ “Wenye furaha ni ninyi mnaolia sasa, kwa sababu mtacheka.+ 22  “Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia,+ wanapowatenga,+ wanapowashutumu, na kuwachafulia jina* kwa ajili ya Mwana wa binadamu. 23  Siku hiyo shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa maana tazama! thawabu yenu ni kubwa mbinguni, kwa kuwa mababu zao waliwatendea manabii mambo hayohayo.+ 24  “Lakini ole wenu ninyi matajiri,+ kwa sababu mnapata faraja yenu kikamili.+ 25  “Ole wenu ninyi mlioshiba sasa, kwa sababu mtakuwa na njaa. “Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa sababu mtaomboleza na kulia.+ 26  “Ole wenu watu wote wanapowasifu,+ kwa maana hivyo ndivyo mababu zao walivyowatendea manabii wa uwongo. 27  “Lakini ninawaambia ninyi mnaosikiliza: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kuwatendea mema wale wanaowachukia,+ 28  kuwabariki wale wanaowalaani, na kusali kwa ajili ya wale wanaowatukana.+ 29  Anayekupiga kwenye shavu moja, mgeuzie pia shavu lingine; na anayechukua vazi lako la nje, usimzuilie hata vazi la ndani.+ 30  Mpe kila mtu anayekuomba,+ na yule anayechukua vitu vyako, usimwombe akurudishie. 31  “Pia, kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.+ 32  “Mkiwapenda wale wanaowapenda, mnapata faida gani? Kwa maana hata watenda dhambi huwapenda wale wanaowapenda.+ 33  Na mkiwatendea mema wale wanaowatendea mema, mnapata faida gani? Hata watenda dhambi hufanya vivyo hivyo. 34  Pia, mkiwakopesha* wale tu ambao mnatumaini watawalipa, mnapata faida gani?+ Hata watenda dhambi huwakopesha watenda dhambi ili warudishiwe kiasi kilekile. 35  Badala yake, endeleeni kuwapenda adui zenu, kutenda mema, na kukopesha bila kutumaini kurudishiwa;+ nanyi mtapata thawabu kubwa, na mtakuwa wana wa Aliye Juu Zaidi, kwa sababu yeye huwaonyesha fadhili hata watu wasio na shukrani na waovu.+ 36  Endeleeni kuwa wenye rehema, kama Baba yenu alivyo mwenye rehema.+ 37  “Zaidi ya hayo, acheni kuhukumu, nanyi hamtahukumiwa kamwe;+ na acheni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa kamwe. Endeleeni kusamehe,* nanyi mtasamehewa.*+ 38  Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa.+ Watawamwagia kwenye mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa, na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.” 39  Kisha akawaambia mfano huu: “Je, kipofu anaweza kumwongoza kipofu mwenzake? Wote watatumbukia shimoni, sivyo?+ 40  Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, lakini kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake. 41  Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako lakini hutambui boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?+ 42  Unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Ndugu, niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako,’ wakati wewe mwenyewe huoni boriti lililo katika jicho lako? Mnafiki! Kwanza toa boriti katika jicho lako, kisha utaona vizuri jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako. 43  “Kwa maana hakuna mti mzuri unaozaa matunda yaliyooza, wala hakuna mti uliooza unaozaa matunda mazuri.+ 44  Kwa maana kila mti hujulikana kwa matunda yake.+ Kwa mfano, watu hawachumi tini kwenye miiba, wala kukata zabibu kwenye miti ya miiba. 45  Mtu mwema hutoa mambo mema kwenye hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutoa maovu kwenye hazina yake mbovu; kwa maana kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.+ 46  “Basi kwa nini mnaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamfanyi mambo ninayosema?+ 47  Nitawaonyesha jinsi alivyo kila mtu anayekuja kwangu na kusikia maneno yangu na kisha kuyatenda:+ 48  Ni kama mtu aliyejenga nyumba kwa kuchimba kina kirefu na kuweka msingi kwenye mwamba. Baadaye, mafuriko yalipotokea, mto ukaipiga nyumba hiyo, lakini haikutikisika, kwa sababu ilikuwa imejengwa vizuri.+ 49  Kwa upande mwingine, yule anayesikia na hatendi,+ ni kama mtu aliyejenga nyumba juu ya udongo, bila msingi. Mto ukaipiga nyumba hiyo, nayo ikaporomoka mara moja, na kuharibika kabisa.”

Maelezo ya Chini

Au “mikate ya wonyesho.”
Au “nafsi.”
Au “kukataa jina lenu.”
Yaani, mkiwakopesha bila faida.
Au “mtaachiliwa.”
Au “kuachilia.”