Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waroma 10:13​—“Anayeliitia Jina la Bwana

Waroma 10:13​—“Anayeliitia Jina la Bwana

 “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”—Waroma 10:13, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka.”—Warumi 10:13, Union Version.

Maana ya Waroma 10:13

 Mungu hana ubaguzi, anawapa watu wote fursa ya kuokolewa na kupata uzima wa milele, bila kuzingatia taifa lao, rangi yao, au uwezo wao wa kifedha. Lakini ili kuokolewa, ni lazima tuliitie jina la Yehova, ambalo ndilo jina la kibinafsi la Mungu Mweza-Yote. aZaburi 83:18.

 Katika Biblia, maneno ‘kuliitia jina la Yehova’ yana maana kubwa zaidi ya kujua jina la Mungu tu na kulitumia katika ibada. (Zaburi 116:12-14) Kunatia ndani kumwamini na kumtegemea Mungu tunapohitaji msaada.—Zaburi 20:7; 99:6.

 Jina la Mungu lilikuwa muhimu kwa Yesu Kristo. Maneno ya kwanza kabisa katika sala ya kielelezo aliyofundisha yalikuwa: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe,” au litukuzwe. (Mathayo 6:9) Yesu hata alionyesha kwamba tunahitaji kumjua, kumtii na kumpenda anayemiliki jina hilo ikiwa tunataka kupata uzima wa milele.—Yohana 17:3, 6, 26.

 Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye “Bwana” aliyetajwa kwenye Waroma 10:13 katika Union Version? Kwa sababu mstari huo umenukuliwa kutoka Yoeli 2:32, ambapo kuna jina la Mungu na si jina la cheo “Bwana,” katika Kiebrania cha awali. b

Muktadha wa Waroma 10:13

 Katika Waroma sura ya 10, Biblia inaonyesha kwamba ili mtu awe na uhusiano mzuri na Mungu lazima awe na imani katika Yesu Kristo. (Waroma 10:9) Wazo hilo linapatana na manukuu kadhaa kutoka katika Agano la Kale. Mtu huonyesha imani kwa kutoa “tangazo la hadharani,” linalotia ndani kuwahubiria habari njema kuhusu wokovu watu ambao si waamini. Kwa njia hiyo, wengine wanapata fursa ya kusitawisha imani inayoongoza kwenye uzima.—Waroma 10:10, 14, 15, 17.

Soma Waroma sura ya 10 pamoja na maelezo ya chini na marejeo ya pambizoni.

a Jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika hati za kale za Biblia. Katika Kiebrania, jina hilo takatifu linapatikana katika herufi nne tu, zinazoitwa Tetragramatoni. Kwa kawaida jina hilo linatamkwa “Yehova” katika Kiswahili; hata hivyo, wasomi fulani hupendelea kutumia “Yahweh.”

b Inawezekana kwamba waandishi wa Biblia Wakristo walitumia jina la Mungu waliponukuu maandishi ya “Agano la Kale” yaliyokuwa na jina hilo. Kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba Tetragramatoni, Jina la Mungu, Yahweh ilipatikana katika baadhi ya manukuu ya A[gano] la K[ale] katika A[gano] J[ipya] wakati maandiko ya [Agano Jipya] yalipokuwa yakiandikwa kwa mara ya kwanza.” (Buku la 6, ukurasa 392) Ili kupata habari zaidi, ona Nyongeza A5 yenye kichwa “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo” katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Nyongeza ya C2 katika Toleo la funzo la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya la Kiingereza, ina orodha ya tafsiri za Biblia zinazotumia jina hilo takatifu kwenye Waroma 10:13.