Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yeremia 29:11—​“Ninajua Mambo Niliyowapangia”

Yeremia 29:11—​“Ninajua Mambo Niliyowapangia”

 “‘Ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, a ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.”—Yeremia 29:11, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “‘Mimi Mwenyezi-Mungu ninajua mambo niliyowapangia. Nimewapangieni mema na si mabaya, ili mpate kuwa na tumaini la baadaye.’”—Yeremia 29:11, Biblia Habari Njema.

Maana ya Yeremia 29:11

 Yehova Mungu aliwaahidi waabudu wake kwamba alikuwa akiwaza jinsi watakavyokuwa na wakati ujao wenye amani. Ingawa mstari huo uliandikwa kwa ajili ya watu walioishi zamani, maneno hayo bado yanafafanua mawazo ya Mungu leo. Yeye ni “Mungu anayetoa tumaini.” (Waroma 15:13) Aliweka ahadi hizo katika Biblia ili “tuwe na tumaini” la wakati ujao mzuri zaidi.—Waroma 15:4.

Muktadha wa Yeremia 29:11

 Maneno hayo ni sehemu ya barua iliyotumwa kwa Waisraeli waliokuwa wakiishi Babiloni, ambao walikuwa wamechukuliwa mateka kutoka Yerusalemu. b (Yeremia 29:1) Mungu aliwaambia mateka hao kwamba wangeendelea kukaa mateka kwa muda mrefu na kwamba wangejenga nyumba, wapande bustani, na kuwa na familia. (Yeremia 29:4-9) Hata hivyo, Mungu alisema hivi pia: “Miaka 70 itakapotimia huko Babiloni nitawakazia ninyi fikira, nami nitatimiza ahadi yangu kwa kuwarudisha [Yerusalemu].” (Yeremia 29:10) Hivyo, Mungu aliwahakikishia kwamba hatawasahau na kwamba tumaini lao la kurudi nyumbani lingetimia.—Yeremia 31:16, 17.

 Mungu aliwatimizia Waisraeli ahadi yake. Kama alivyokuwa ametabiri, Babiloni lilishindwa na Mfalme Koreshi wa Uajemi. (Isaya 45:1, 2; Yeremia 51:30-32) Baada ya hapo, Koreshi aliwaruhusu Wayahudi warudi nyumbani kwao. Baada ya miaka 70 ya utekwa, walirudi tena Yerusalemu.—2 Mambo ya Nyakati 36:20-23; Ezra 3:1.

 Unabii uliotimizwa wa Yeremia 29:11 unawapa uhakika wale wanaotazamia kwa hamu kuona utimizo wa ahadi za Mungu leo. Ahadi hizo zinatia ndani, amani ulimwenguni pote kupitia kwa Ufalme wa Mungu chini ya Kristo Yesu.—Zaburi 37:10, 11, 29; Isaya 55:11; Mathayo 6:10.

Maoni Yasiyo Sahihi Kuhusu Yeremia 29:11

 Maoni yasiyo sahihi: Mungu ana “mpango” hususa kwa ajili ya kila mwanadamu.

 Ukweli: Mungu huwaacha wanadamu wajiamulie watafanya nini maishani. Maneno yake kwenye Yeremia 29:11 yaliandikwa kwa ajili ya Waisraeli waliokuwa Babiloni wakiwa kikundi, na aliwataka wote wakiwa kikundi wawe na wakati ujao wenye amani. (Yeremia 29:4) Hata hivyo, Mungu alimruhusu kila mmoja wao achague ikiwa alitaka kunufaika kutokana na ahadi hiyo au la. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Yeremia 29:32) Wale waliochagua kumtafuta Mungu walifanya hivyo kwa kusali kwake wakiwa na moyo mnyoofu.—Yeremia 29:12, 13.

 Maoni yasiyo sahihi: Mema ambayo Mungu atawapa waabudu wake ni mali za kimwili.

 Ukweli: Neno “mema” ambalo hutumiwa kwenye Yeremia 29:11 katika Biblia fulani limetafsiriwa kutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “amani, afya, na hali njema.” Kulingana na muktadha, Mungu aliahidi kuwapa Waisraeli waliokuwa utekwani amani na hali njema, si utajiri. Wangeendelea kuwepo wakiwa taifa na siku moja wangerudi Yerusalemu.—Yeremia 29:4-10.

Soma Yeremia sura ya 29 pamoja na maelezo ya chini na marejeo ya pambizoni.

a Yehova ndilo jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.

b Kuhusu Yeremia 29:11, The Expositor’s Bible Commentary inasema: “Ni vigumu kupata ahadi yenye kupendeza kama hii popote katika Maandiko inayoonyesha huruma za Yahweh [Yehova] kuwaelekea mateka hao na hatimaye kuwapa sababu ya kuwa na tumaini.”—Buku la 7, ukurasa wa 360.