Kulingana na Luka 18:1-43

  • Mfano wa mjane aliyeendelea kuomba (1-8)

  • Farisayo na mkusanya kodi (9-14)

  • Yesu na watoto (15-17)

  • Mtawala tajiri auliza swali (18-30)

  • Kifo cha Yesu chatabiriwa tena (31-34)

  • Kipofu aliyekuwa akiombaomba aponywa (35-43)

18  Kisha akawaambia mfano ili kuwaonyesha umuhimu wa kuendelea kusali bila kukata tamaa.+  Akasema: “Katika jiji fulani kulikuwa na mwamuzi ambaye hakumwogopa Mungu wala hakumheshimu mtu yeyote.  Pia, katika jiji hilo kulikuwa na mjane ambaye alikuwa akienda kwake na kumwomba, ‘Hakikisha kwamba kesi yangu itaamuliwa kwa haki.’  Kwa muda fulani yule mwamuzi alikataa, lakini baadaye akajiambia, ‘Ingawa simwogopi Mungu wala simheshimu mtu yeyote,  kwa sababu huyu mjane anaendelea kunisumbua, nitahakikisha amepata haki ili asiendelee kuja kunichosha na maombi yake.’”*+  Kisha Bwana akasema: “Sikieni alichosema mwamuzi huyo ingawa si mwadilifu!  Kwa hakika, je, Mungu hatawatendea haki watu wake waliochaguliwa ambao wanamlilia mchana na usiku,+ huku akiwaonyesha subira?+  Ninawaambia, atawatendea haki upesi. Hata hivyo, Mwana wa binadamu atakapofika, je, kweli ataipata imani hii* duniani?”  Pia, aliwaambia mfano huu wale waliojiona kuwa waadilifu na kuwadharau wengine: 10  “Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja alikuwa Farisayo na mwingine mkusanya kodi. 11  Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi si kama watu wengine—wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi—au hata kama mkusanya kodi huyu. 12  Mimi hufunga mara mbili kwa juma; ninatoa sehemu ya kumi ya mapato yangu yote.’+ 13  Lakini yule mkusanya kodi alikuwa amesimama mbali kidogo na hata hakutaka kutazama mbinguni, bali alijipigapiga kifuani akisema, ‘Ee Mungu, nihurumie* mimi mtenda dhambi.’+ 14  Ninawaambia, mtu huyu alishuka kwenda nyumbani akiwa mwadilifu mbele za Mungu kuliko yule Farisayo.+ Kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, lakini yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”+ 15  Sasa watu wakamletea Yesu watoto wao wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi walipoona hivyo wakaanza kuwakemea.+ 16  Lakini Yesu akawaita wale watoto, akisema: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, na msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama wao.+ 17  Kwa kweli ninawaambia, yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia kamwe ndani yake.”+ 18  Mtawala fulani akamuuliza: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 19  Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.+ 20  Unazijua amri hizi: ‘Usifanye uzinzi,+ usiue,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ mheshimu baba yako na mama yako.’”+ 21  Ndipo akasema: “Nimeyashika hayo yote tangu nilipokuwa kijana.” 22  Baada ya kusikia hilo, Yesu akamwambia, “Bado kuna jambo unalokosa: Uza kila kitu ulicho nacho na uwagawie maskini pesa hizo, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 23  Aliposikia hivyo, akahuzunika sana, kwa sababu alikuwa tajiri sana.+ 24  Yesu akamtazama na kusema: “Itakuwa vigumu sana kwa wale walio na pesa kuingia katika Ufalme wa Mungu!+ 25  Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+ 26  Wale waliosikia hilo wakauliza: “Ni nani anayeweza kuokolewa?”+ 27  Akasema: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”+ 28  Lakini Petro akamwambia: “Tazama! Tumeacha vitu vyetu na kukufuata.”+ 29  Akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna yeyote ambaye ameacha nyumba, au mke, au ndugu, au wazazi, au watoto kwa ajili ya Ufalme wa Mungu+ 30  ambaye hatapata mara nyingi zaidi wakati huu, na katika mfumo wa mambo* unaokuja, uzima wa milele.”+ 31  Ndipo akawaita kando wale 12 na kuwaambia: “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na mambo yote yaliyoandikwa kupitia manabii kuhusu Mwana wa binadamu yatatimia.*+ 32  Kwa mfano, atatiwa mikononi mwa watu wa mataifa+ naye atadhihakiwa,+ atatendewa kwa dharau, na kutemewa mate.+ 33  Watampiga mijeledi, kisha watamuua,+ lakini siku ya tatu atafufuka.”+ 34  Hata hivyo, hawakuelewa maana ya mambo hayo, kwa sababu walikuwa wamefichwa maneno hayo, nao hawakuelewa mambo yaliyosemwa. 35  Yesu alipokaribia Yeriko kipofu mmoja alikuwa ameketi kando ya barabara akiombaomba.+ 36  Aliposikia umati ukipita, akaanza kuuliza kilichokuwa kikiendelea. 37  Wakamjibu: “Yesu Mnazareti ndiye anayepita!”⁠ 38  Ndipo akasema kwa sauti kubwa: “Yesu, Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 39  Wale waliokuwa mbele wakaanza kumkemea wakimwambia anyamaze, lakini akazidi kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 40  Kisha Yesu akasimama na kuagiza mtu huyo aletwe kwake. Alipokaribia, Yesu akamuuliza: 41  “Unataka nikufanyie nini?” Akasema: “Bwana, naomba niweze kuona tena.” 42  Basi Yesu akamwambia: “Ona tena; imani yako imekuponya.”+ 43  Mara moja akaanza kuona tena, naye akaanza kumfuata Yesu+ huku akimtukuza Mungu. Pia, watu wote walipoona hayo, wakamsifu Mungu.+

Maelezo ya Chini

Au “kunishambulia mpaka animalize.”
Au “imani kama hii.” Tnn., “ile imani.”
Au “nionyeshe rehema.”
Angalia Kamusi.
Au “yatakamilika.”
Au “nionyeshe rehema!”
Au “nionyeshe rehema!”