Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Imani

Imani

Baadhi ya watu hudai kuwa wao ni waumini wa dini, hata hivyo, wanashindwa kuelewa maana ya “imani.” Imani ni nini, na kwa nini ni muhimu kuwa na imani?

Imani ni nini?

WATU HUSEMA NINI?

Wengi hufikiri kwamba mtu mwenye imani huamini jambo kwa urahisi bila kuwa na uthibitisho kamili. Kwa mfano, fikiria mtu fulani wa dini anayesema, “Ninamwamini Mungu.” Iwapo anaulizwa, “Kwa nini unaamini?” huenda akajibu, “Nimelelewa hivyo” au, “Nimefundishwa hivyo tangu utoto.” Katika visa hivyo, inaweza kuonekana kwamba kuna tofauti dogo kati ya kuwa na imani na kuamini bila msingi.

BIBLIA INASEMA NINI?

“Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Ili kuwa na tarajio hakika, ni lazima kuwepo na sababu za msingi za kuamini jambo. Kihalisi, neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “tarajio lililohakikishwa” lina maana pana zaidi ya kuwa na hisia za ndani tu au kupenda jambo fulani. Hivyo imani inahusisha uhakikisho unaotegemea uthibitisho hakika.

“Kwa maana sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.”Waroma 1:20.

Kwa nini ni muhimu kuwa na imani?

BIBLIA HUSEMA NINI?

“Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Kama ilivyotajwa awali, watu wengi wanamwamini Mungu kwa sababu wamefundishwa kufanya hivyo. Huenda wakasema ‘nimelelewa kwa njia hiyo.’ Lakini Mungu anataka wale wanaomwabudu wawe na uhakika kabisa kuwa yeye yupo na kwamba anawapenda. Hiyo ni sababu moja Biblia inatuhimiza tumtafute kwa bidii, ili tumjue vizuri.

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”Yakobo 4:8.

Unaweza kuipata imani jinsi gani?

BIBLIA INASEMA NINI?

“Imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Hivyo, hatua ya kwanza ili kujenga imani kuelekea Mungu ni ‘kusikia’ yale ambayo kwa kweli Biblia inafundisha kumhusu. (2 Timotheo 3:16) Kujifunza Biblia kutakusaidia kupata majibu ya maswali muhimu zaidi, kama vile: Mungu ni nani? Kuna mambo gani yanayothibitisha kwamba kuna Mungu? Je, kweli Mungu ananijali? Kusudi la Mungu ni nini kuhusu wakati ujao?

Kuna mambo mengi tunayoona yanayothibitisha kwamba Mungu yupo

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza Biblia. Kama vile inavyoelezwa katika tovuti yao ya jw.org/sw “Mashahidi wa Yehova wanapenda kuwafundisha watu Biblia, hata hivyo hawamlazimishi mtu yeyote kujiunga na dini yao. Badala yake, tunaheshimu yale ambayo Biblia inasema, tunajua kwamba kila mtu ana haki ya kuamua kile atakachoamini.”

Hatimaye, imani yako ni lazima itegemee uthibitisho wa kweli ambao wewe mwenyewe umejifunza katika Biblia. Kwa njia hiyo, utakuwa unaiga mfano wa wanafunzi wa Biblia wa karne ya kwanza ambao, “walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:11.

“Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”Yohana 17:3.