Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Kushinda Kizuizi cha Lugha—Kuchunguza Nyuma ya Pazia

Kushinda Kizuizi cha Lugha—Kuchunguza Nyuma ya Pazia

“Nyakati fulani imesemwa kwamba hakuna kazi ngumu kama kutafsiri.” —“The Cambridge Encyclopedia of Language.”

KABLA ya kutafsiri, machapisho ya Mashahidi wa Yehova huandaliwa mapema, hufanyiwa utafiti, na kuandikwa. Katika hatua hiyo, Halmashauri ya Uandikaji iliyo katika makao makuu huko New York, hupitia kwa uangalifu makala yote ili kuchunguza ikiwa ni sahihi na kuhakikisha kwamba imetumia lugha inayoeleweka kwa urahisi. *

Kisha, Halmashauri ya Uandikaji hutuma makala hiyo kwa mamia ya vikundi vya watafsiri duniani kote, ambao wengi huishi na kufanya kazi katika eneo ambalo lugha wanayotafsiri huzungumzwa. Watafsiri wengi hutafsiri katika lugha zao za asili. Wanapaswa kuelewa vizuri lugha chanzi na vilevile lugha wanayotafsiri.

Watafsiri hufanya kazi yao jinsi gani?

Geraint, ambaye ni mtafsiri huko Uingereza, anaeleza hivi: “Ninafanya kazi na kikundi cha watafsiri, kwa hiyo ushirikiano mzuri ni muhimu. Kwa pamoja tunafanya utafiti ili kutatua matatizo katika kazi ya utafsiri. Hatufanyi hivyo kwa kufikiria neno moja tu bali tunafikiria sentensi nzimanzima. Tunachunguza kwa makini maana na kusudi la makala, wakati wote tukiwafikiria watu waliokusudiwa katika kila makala.”

Una lengo gani ukiwa mtafsiri?

“Lengo letu ni kumsaidia msomaji ahisi kana kwamba makala iliandikwa kwa lugha yake ya asili. Hapaswi kuiona kama habari iliyotafsiriwa. Ili kutimiza hilo, tunajitahidi kutumia lugha ya kawaida. Kwa njia hiyo, tunafanya msomaji avutiwe na habari, naye ataendelea kufurahia kama vile kula chakula chenye ladha nzuri mdomoni.”

Kuna faida gani kuishi katika eneo ambalo lugha inazungumzwa?

“Kuishi katika eneo ambalo watu huzungumza lugha kuna faida nyingi. Tunasikia lugha hii kila siku. Kwa kuongezea, tunaweza kujaribu maneno na mawazo ili kujua ikiwa tunatumia lugha ya kawaida, inayoeleweka, na inayovutia. Hilo hutusaidia kuwasilisha maana halisi iliyo katika lugha ya kwanza.”

Kazi yako hupangwa jinsi gani?

“Kikundi hupangwa ili kufanya kazi kwa kila mradi. Kwanza kabisa, kila mshiriki husoma makala ili kujua kusudi na kufikiria wasomaji waliokusudiwa na mpangilio wa habari yenyewe. Tunajiuliza hivi: ‘Lengo la makala hii ni nini? Jambo kuu na kusudi la makala hii ni nini? Ninatarajia kujifunza nini katika makala hii?’ Hatua hii hutusaidia kuelewa habari kabla ya kuanza kutafsiri.

“Kisha, kikundi hukutana ili kujadili mawazo yao kwa pamoja, wakijifunza kutoka kwa mmoja na mwingine. Je, tuna uhakika kwamba tumeelewa makala? Tunawezaje kuwasilisha ujumbe kwa njia na mtindo kama ulio katika makala ya lugha chanzi? Lengo letu ni kuwasaidia wasomaji wetu kupata hisia zilizokusudiwa na mwandishi wa makala.”

Kikundi hufanyaje kazi pamoja?

“Lengo letu ni kuwasaidia wasomaji kuelewa habari mara tu wanapoisoma mara ya kwanza. Ili kufanya hivyo, mara kadhaa tunasoma kwa sauti kila kifungu cha maneno tulichotafsiri.

“Mtafsiri huchapa maandishi katika lugha lengwa, na sisi hutazama kwenye kompyuta zetu. Sisi huhakikisha kwamba hakuna wazo lililoachwa au kuongezwa. Pia tunachunguza ikiwa lugha, herufi na sarufi ni sahihi. Kisha, mmoja husoma fungu hilo kwa sauti. Ikiwa anakwama anaposoma tunachunguza sababu. Baada ya kumaliza kutafsiri makala yote, mshiriki mmoja huisoma makala hiyo kwa sauti na wengine humsikiliza na kuweka alama mahali penye tatizo ili kulishughulikia.”

Inaonekana ni kazi ngumu!

“Bila shaka! Mwishoni mwa siku, sisi huwa tumechoka. Hivyo tunapumzika na siku inayofuata tunapitia tena makala hiyo. Majuma kadhaa baadaye, tunapokea marekebisho ya mwisho ya makala ya kwanza kutoka kwa Halmashauri ya Uandikaji. Kisha tunaisoma tena makala hiyo tukiwa macho kuona sehemu yoyote ile inayohitaji kuboreshwa zaidi.”

Ni programu gani za kompyuta mnazotumia?

“Kompyuta haiwezi kufanya kazi kwa niaba ya mtafsiri. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wamebuni programu zinazorahisisha kazi yetu. Programu moja ni kamusi yenye maneno na semi ambazo sisi hutumia kwa ukawaida. Programu nyingine hutuwezesha kufanya utafiti katika machapisho yote yaliyotafsiriwa na timu yetu, hivyo hutusaidia kutatua matatizo ya utafsiri wa lugha yetu.”

Unaionaje kazi yako?

“Tunaiona kazi yetu kuwa zawadi kwa watu wote. Nasi tunataka zawadi hiyo iwavutie sana. Tunasisimuka tunapoona makala fulani ya gazeti au habari iliyo katika mtandao ikigusa moyo wa msomaji na kumsaidia kuboresha maisha yake.”

Faida Inayodumu Milele

Duniani kote, mamilioni ya watu hufaidika kwa kusoma machapisho ya Mashahidi wa Yehova katika lugha zao. Hekima bora inayopatikana katika machapisho, video, na tovuti yao ya jw.org hutegemea Biblia. Zaidi ya yote, katika Biblia, Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, anatuambia kwamba anataka ujumbe wake uenezwe kwa “kila taifa na kabila na lugha.”—Ufunuo 14:6. *

^ fu. 4 Makala ya kwanza hutayarishwa kwa Kiingereza.

^ fu. 25 Tembelea www.mt711.com/sw kupata machapisho, rekodi za kusikiliza, na video kwa lugha yako na katika mamia ya lugha nyinginezo.